Thursday, July 28, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 48

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0655 340572
 
MWANAMKE 48
 
ILIPOISHIA
 
Nilipobaki mle chumbani nilivua nguo nikaenda kuoga. Niliotoka bafuni nilivaa ile suti mpya aliyoninunulia Abdi. Nikajitazama kwenye kioo na kuona nilipendeza. Angalau ilinisahaulisha madhila niliyokuwa nayo moyoni.
 
Baada ya kuvaa nilishuka chini nikaingia katika eneo la mgahawa. Yule mhudumu aliyenipokea begi alinifuata.
 
 
Akanisemea kwa kisomali.
 
“Sijui hiyo lugha labda mnifundishe” nikamwambia.
 
“Unajua Kiswahili peke yake?” akaniuliza.
 
“Na kizigua”
 
“Unatoka Handeni Tanzania?”
 
“Umejuaje”
 
“Kule ndio kuna wazigua”
 
“Nasikia na nyinyi pia mna asili ya huko”
 
“Babu zetu wametoka huko lakini mimi unaniona mweupe mama yangu ni mbarawa”
 
“Mmejifundisha wapi Kiswahili?”
 
“Mimi nilizaliwa Garissa nchini Kenya, kule watu wanazungumza Kiswahili. Wenzangu wengine wametoka Mombasa”
 
SASA ENDELEA
 
“Nashukuru  kwa mazungumzo, ninahitaji chakula”
 
“Upatiwe menyu?”
 
“Kwani wewe si ndiye unayehusika”
 
“Mimi pia nahusika lakini kuna mhudumu maalum wa hapa. Ngoja nimuite”
 
Shamsa akamuita msichana mmoja na kumwambia.
 
“Mgeni wa bosi. Bosi ameagiza apatiwe kila atakachohitaji. Bili itakuwa juu yake”
 
“Sawa” Msichana alimkubalia kisha akaniuliza.
 
“Nikupatie menyu?”
 
“Ndio nipatie”
 
Menyu alikuwa anayo mkononi, akaniwekea juu ya meza.
 
Nikaishika na kutazama orodha ya vyakula. Nikachagua wali kwa samaki na juisi.
 
Wasichana wote wawili waliondoka na kuniacha.
 
Baada ya muda kidogo nililetewa chakula nilichoagiza. Wakati nakula nilianza kujiwazia mustakbali wangu kule Somalia. Nilijiuliza Abdi alikuwa na madhumuni gani kunichukua mimi Somalia, kuniweka hoteli na kunihudumia kama rafiki yake wakati tulikuwa hatujuani.
 
Pia nilijiuliza ningekaa Somalia hadi lini. Ingawa niliingia kienyeji lakini wakati ule Somalia ilikuwa na serikali. Nilitakiwa kuwa na paspoti. Nilijiambia kama ningekamatwa nitakuwa na kosa la kuingia nchi ya watu bila paspoti.
 
Nilishindwa kumuuliza Abdi kuwa ningekaa hapo Somali kwa siku ngapi, hasa nikikumbuka muda ule alionitolea bastola kwa kumhoji niende Somalia kufanya nini.
 
Niliogopa kuwa ningeweza kumkasirisha na hivyo akanipiga risasi na kwenda kuutupa mwili wangu jalalani. Mtu mwenyewe licha ya kuwa mchangafu, mkarimu na anayependa kutabasamu, alionekana kuwa katili na asiyejali kitu.
 
Mtu wa aina yake kuua ni kazi ndogo tu!
 
 
Nilipomaliza kula niliondoka nikarudi ghorofani. Niliingia chumbani nikaenda kusimama kando ya dirisha na kutazama mandhari ya nje.
 
Niliendelea kusimama hapo nikiangalia magari na watu waliokuwa wakipita barabarani huku akili yangu ikitafuta jibu la kwanini niko pale Somalia lakini sikupata jibu.
 
Nilipitisha kama nusu saa nikiwa hapo, nikaingia chumbani na kuvua koti kisha nikajilaza kitandani.
 
Nilikuwa nina uchovu na nilikuwa na usingizi. Kwa vile moyo wangu kidogo ulikuwa umetulia nikaona naweza kulala.
 
Na nililala. Nilipokuja kuzinduka niliona giza. Ilikuwa ni usiku. Kwa vile sikuwa na saa sikuweza kujua ilikuwa ni usiku wa saa ngapi.
 
Nikainuka kitandani na kuwasha taa. Pale mchagoni mwa kitanda palikuwa na simu. Nikainua mkono wa simu na kuzungumza na opereta.
 
“Abdi ameshafika?” nikamuuliza.
 
“Wewe nani?”
 
“Mimi ni mgeni wake, niko ghorofa ya kwanza”
 
“Alifika, akakupigia simu lakini haikupokelewa akajua umelala”
 
“Sasa yuko wapi?”
 
“Ameshaondoka, ametuambia tukuambie kuwa mtakutana asubuhi”
 
“Ni saa ngapi sasa?”
 
“Saa mbili inakwenda kwenye na nusu”
 
“Nitashuka sasa hivi kuja kupata chakula”
 
“Sawa, chakula kipo”
 
Nikauweka mkono wa simu mahali pake na kuvua nguo. Nilikwenda kuoga tena.
 
Nilipomaliza nilirudia kuvaa suti yangu kisha nikashuka chini. Niliingia katika ukumbi wa mkahawa wa hoteli hiyo.
Mhudumu aliponiona tu akanifuata na kunipa menyu.
 
“Nahtaji chai tu” nikamwambia.
 
“Chai na nini?”
 
“kama kuna sambusa nipatie tatu”
 
Mhudumu aliondoka. Baada ya muda kidogo alirudi akiwa na chano kilichokuwa na kisahani kilichokuwa na sambusa tatu, birika ndogo ya maziwa, kipakiti cha majani ya chai, jagi la sukari na kikombe kitupu kikiwa na kisahani chake.
 
Aliniwekea juu ya meza. Nikachukua birika na kumimina maziwa kwenye kikombe nikatia kijiko kimoja na nusu cha sukari na kukoroga.
 
Baada ya sukari kukolea, nilitumbukiza kile kipakiti cha majani ya chai ambacho kiliyafanya maziwa kuwa na rangi ya chai.
 
Nilitumia nusu saa nzima kunywa chai huku nikijiwazia. Mpaka muda ule sikuwa nimeitambua dhamira ya Abdi.
 
Nikajiambia baada ya siku tatu nitamwambia kuwa nahitaji kuondoka kurudi kwetu kwani sikuwa na sababu yoyote ya kuendelea kukaa Somalia huku ndugu zangu na mama yangu wakiwa hawajui niliko.
 
Baada ya kumaliza kunywa chai nilikwenda kujipumzisha kwenye eneo la wazi la hoteli ambapo palikuwa na upepo mwanana kutoka Bahari ya Hindi.
 
Pale nilipoteza dakika kadhaa kabla  ya kuamua kurudi chumbani kwangu.
 
Mawazo ya Zena yalinijia usiku ule. Nikajiambia msichana wa kijini aliamua kunisaliti kwenye kile kisiwa baada ya kukataa kuoana naye.
 
Kitendo cha kutoonana tena na Zena kilinipa picha kwamba Zena aliamua kuachana na mimi.
 
Nikajiambia kama kweli alikuwa ameamua hivyo lilikuwa jambo la kushukuru sana kwani msichana yule alikuwa ananisababishia matatizo makubwa.
 
Baada ya kuwaza sana nilipitiwa na usingizi. Sikujua nililala kwa muda gani lakini nilihisi kama nilishituka katikati ya usiku au nilikuwa katika ndoto. Nikaona kama mlango wa chumba nilichokuwa nimelala unafunguliwa taratibu.
 
Kitendo hicho kilitokea nikiwa na kumbukumbu kamili kichwani mwangu kwamba mlango wa chumba hicho niliufunga kwa ndani na kuhakikisha kuwa ulikuwa umefungika.
 
Mlango ulipokuwa wazi nilimuona mtu akiingia. Alikuwa mzee mwembamba na mrefu. Wembamba wake ulichanganyika na kukonda. Alikuwa na nywele ndefu, nyeupe tupu.
 
Alikuwa amejifunga shuka nyeupe kiunoni na mabegani alijitanda shuka nyingine nyeupe kuziba kifua na tumbo lake. Hata hivyo upande mmoja wa kifua chake ulikuwa ukionekana. Mbavu zake zilikuwa zimetokeza na kuhisabika.
 
Akaingia mle chumbani kwa kunyata. Wakati akiingia nilikuwa nikijiuliza nilikuwa ninaota au nilichokuwa nakiona kilikuwa ni kweli.
 
Muda huo niligundua kuwa  sikuwa sawa. Nilikuwa kama niliyepatwa na jinamizi. Mwili wangu haukuwa na uwezo wa kufanya chochote hata kupiga kelele.
 
Kadhalika akili yangu ilikuwa imepoteza uwezo wake na nilikuwa kama taahira au zezeta. Sikuweza kujua ni kwanini nilijihisi kuwa vile.
 
Yule mzee wa kisomali alikuja hadi karibu na kitanda nilichokuwa nimelala.
 
Nilimuona vizuri. Alikuwa na pua ndefu na macho makali na madogo. Akasimama na kuniita.
 
“Amour!”
 
Nikanyamaza kimya. Nikamuona anasema maneno fulani kwa lugha  ya kisomali kisha akanyoosha mkono wake na kupapasa kitanda nilichokuwa nimelalaa akashika mkono wangu na kuubana.
 
JE NI MZEE GANI TENA HUYO NA AMETOKEA WAPI? HAYA NI MAMBO YA KUTISHA SASA! DUH!
 

No comments:

Post a Comment