Tuesday, July 19, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 55

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI
 
MWANAMKE 55
 
ILIPOISHIA
Chumba hicho kilikuwa kikubwa kuliko cha boti ya Mapama na kilikuwa kizuri kilichozungukwa na kuta za vioo. Ndani kilikuwa na sehemu ya kulala na makochi ya kukalia.
 
“Karibu, kaa hapo” Msomali akaniambia akinionesha moja ya makochi yaliyokuwa katika kile chumba.
 
Nikakaa.
 
“Asalaam alaykum” Msomali akaniambia huku akiketi upande wa pili wa chumba hicho.
 
“Waalaika Salaam” nikamjibu kwa sauti iliyonywea huku nikimtazama usoni kwake.
 
“Nimeelezwa na Nahodha kuhusu wewe na mkasa uliowatokea mlipokuwa mnakuja. Ameniambia kulitokea joka kama nondo na kuwaangamiza wenzake, ni kweli?”
 
“Ni kweli”
 
“Kwani walitaka  kukufanya nini?”
 
“Walitaka kuniua”
 
“Wapumbavu wale, mtu unaomba msaada wanataka kukuua. Sasa hilo joka lilitoka wapi?”
 
Nikabetua mabega yangu.
 
“Sijui”
 
“Bila shaka hilo ndilo lililokuokoa usiuawe, ungekuwa umeshatoswa na kuliwa na papa”
 
Hapo sikumjibu kitu.
 
“Wewe unaitwa Umar?” Msomali akaniuliza.
 
“Hapana”
 
“Unaitwa Amiri?”
 
“Hapana”
 
“Basi utakuwa unaitwa Amour”
 
Nikamkubalia.
 
“Ndio naitwa Amour, umejuaje?”
 
Msomali huyo akacheka. Badala ya kunijibu akaniambia.
 
“Nataka twende Somali mara moja”
 
Nikashituka na kumuuliza.
 
“Kwani hapa tuko wapi?’
 
SASA ENDELEA
 
“Hapa ni Somalia, nina maana nataka twende Mugadishu”
 
“Kufanya nini?”
 
“Nitakuwa na kazi na wewe”
 
“Mimi nataka kurudi. Nilishamwambia Nahodha akishafaulisha mzigo wake turudi”
 
“Sasa amri ni yangu mimi si ya Nahodha. Mimi nataka twende Mugadishu”
 
“Mimi sitakwenda huko”
 
Msomali huyo hakunisikiliza akainuka na kutoka katika  kile chumba. Na mimi nikainuka na kumfuata.
 
Alipoona nimetoka alihamaki akaniuliza.
 
“Unataka kuleta ubishi?”
 
“Hapana”
 
“Nani amekuamrisha utoke?”
 
“Nilikwambia sitakwenda Mugadishu, nahitaji kurudi”
 
Msomali huyo hakusema kitu tena, alitia mkono ndani ya shati lake akatoa bastola na kunielekezea.
 
“Sasa chagua moja, nikutoe roho au baki kwenye hii boti!” akaniambia kwa hasira.
 
Nikanywea hapo hapo.
 
“Nenda kakae”
 
Ikabidi nirudi kwenye kile chumba. Nilijua kama nitaendelea kubishana naye anaweza kuniramba risasi. Wasomali hawa hawana huruma, kuna wengine hawana utu kabisa.
 
Nikakaa kinyonge kwenye kohi huku macho yangu yakimtazama yule Msomali kwa macho ya kulaani. Nikamuona mapama akiingia kwenye ile boti.
 
Akasimama na yule Msomali na kuzungumza naye kwa kirefu. Sikuweza kusikia walichokuwa wanazungumza. Mara moja moja Mapama alikuwa akinitazama. Nilikuwa nikimuonesha ishara ya kumuita ili nimuulize mbona ananigeuka.
 
Lakini Mapama licha ya kuona kuwa nilikuwa ninaashiria kumuita hakunijali hata chembe.
 
Pembe za ndovu zilikuwa zikiendelea kingizwa kwenye boti hiyo. Kazi ilipokwisha, Msomali aliingia katika kile chumba akafungua dawati mojawapo na kutoa mfuko ambao alitoka nao.
 
Ule mfuko ulikuwa na pesa. Sikujua zilikuwa pesa za wapi isipokuwa niliona Msomali akitoa vitita vya noti na kumhesabia Mapama. Mapama naye alizitia pesa hizo kwenye mfuko wa ngozi aliokuwa ameushika kisha nikaona wanaagana kwa furaha.
 
Hapo ndipo nilipotoa sauti nikamuita.
 
“Nahodha!”
 
Nilimuita zaidi ya mara tatu lakini hakunipatiliza akatoka kwenye ile boti na kuingia kwenye boti yake. Yule Msomali akaingia kwenye kile chumba. Bastola yake ilikuwa bado mkononi ingawa aliishika kwenye mtutu.
 
Boti ya Mapama ikawashwa moto. Nikajua kuwa Mapama alikuwa ameshaniuza kwa wasomali hao. Kwa lugha nyingine ilikuwa sawa na kusema kuwa Nilikuwa nimetekwa nyara na kupelekwa mahali bila hiyari yangu.
 
Boti ya Mapama ikaondoka, ilikata kona ndefu na kugeuka ilikotoka. Nikaachwa mikononi mwa wasomali.
 
Nilikuwa nimetaharuki na akili yangu iliniruka. Boti ya wasomali ikawashwa, nayo ikaondoka kuelekea Somalia.
 
Sikujua Mapama alikuwa amezungumza nini na yule msomali na pia sikujua walikuwa wananipeleka Somalia kwa ajili gani.
 
Pia nilikuwa nimeshangazwa na jinsi msomali huyo alivyolitambua jina langu ambalo sikuwahi kumtajia hata Mapama.
 
Kijana huyo wa kiosamali alikuja kukaa kando yangu na kuendelea kutafuna mirungi yake. Bastola yake aliipachika kiunoni. Bila shaka alifanya hivyo mbele yangu ili kunionya nisimletee ukaidi.
 
Lakini ukiacha muda ule aliponichomolea bastola hiyo ambapo alionesha kukasirika,  uso wake ulikuwa wa kirafiki wakati wote.
 
“Mimi naitwa Abdi” akaniambia wakati akiendelea kutafuna mirungi kisha akaniuliza.
 
“Unakula mirungi?”
 
Nikatikisa kichwa. Mdomo ulikuwa mzito kumjibu.
 
“Najua wewe ni mzaliwa wa Tanga lakini sijui unaishi sehemu gani?” akaniuliza.
 
Swali lake hilo nalo lilinishangaza. Alijuaje kuwa mimi ni mzaliwa wa Tanga?
 
“Ninaishi sehemu inayoitwa Msambweni” nikamjibu.
 
“Wazazi wakao wako wapi?”
 
“Baba yangu alikwishakufa, mama yangu ndio yupo”
 
Msomali huyo alinikubalia kwa kichwa.
 
“Unafanya shughuli gani?”
 
“Nimeajiriwa katika shirika moja linaloitwa CTC”
“Najisikia ni mwenye furaha sana kukutana na mtu kama wewe”
 
“Umelitambuaje jina langu pamoja na mahali nilipozaliwa?” nikamuuliza.
 
Badala ya kunijibu aliangua kicheko.
 
“Nilikuwa nakisia tu kumbe nilipatia”
 
“Haiwezekani ukisie halafu iwe sawa”
 
“Amour sina jibu jingine la kukupa kwa sasa”
 
“Uliwahi kufika Tanga?”
 
Abdi akatikisa kichwa.
 
“Sijawahi”
 
“Kwanini unalazimisha twende Somalia?”
 
“Ni kwa sababu za kiudugu na kiurafiki tu. Utakuwa huko kwa muda tu halafu utarudi kwenu na kama utapenda kuendelea kuishi huko huko nitakupatia nyumba, kazi na gari”
 
“Kwa vyovyote vile itabidi nirudi, mama yangu na ndugu zangu hawajui niko wapi”
 
“Basi utarudi”
 
Boti iliendelea kusonga mbele. Baada ya mwendo wa kilometa tano hivi tukakutana na meli iliyokuwa imetia nanga. Boti ilikwenda kusimama ubavuni mwa meli.
 
Abdi aliniacha akatoka kwenye kile chumba. Kuna ngazi iliyoshushwa kutoka kwenye meli. Abdi alipanda ngazi hiyo akaingia ndani ya meli. Baada ya muda kidogo alishuka akiwa na maafisa wawili wa meli hiyo ambao niliwatambua kutokana na mavazi yao.
 
Waliyakagua yale meno ya tembo kisha nikaona krini ya meli inashushwa kutoka kwenye meli. Yale meno ya tembo yalikuwa yamepangwa kwenye turubai. Turubai hilo lilikuwa na vipete vinne vilivyowekwa kwenye pembe nne za turubai hilo. Kamba ikapitishwa kwenye vipete hivyo kisha ikapachikwa kwenye mkono wa krini.
 
Turubai likavutwa juu pamoja na pembe zake. Zilivutwa juu kuupita usawa wa meli kisha zikaingizwa ndani ya meli.
 
Abdi pamoja na wale maafisa wawili wa meli walirudi melini. Walipoteza muda wa karibu saa nzima kabla ya Abdi kurudi akiwa peke yake.
 
Aliingia kwenye kile chumba akiwa na mfuko uliotuna ambao aliuweka kwapani. Akafungua dawati mojawapo na kuuweka.
 
“Hizi ni pesa” akaniambia bila kumuuliza.
 
Sikumjibu kitu. Akarudi kuketi pale alipokuwa.
 
“Zile pembe zinakwenda Oman kwa waarabu” akaniambia lakini mimi bado nilikuwa kimya. Kitendo kile cha kunipaleka Mogadishu kwa lazima kilikuwa kimenifadhaisha sana.
 
Sikuwa nimeamini zile sababu zake kwamba alinipeleka kwa sababu za kiudugu na kiurafiki. Sikuwa na udugu naye wala urafiki naye na hatukuwa tukijuana zaidi ya kukutana siku ile.
 
Nilihisi kuna kitu ambacho alizungumza na Mapama ndio wakapanga niende Mogadishu. Sasa sikujua kama walikuwa wanakwenda kuniua au kunifanya nini.
 
Wakati niko katika lindi la mawazo nilianza kuona mataa kwa mbali. Ilikuwa ni bandari ya Mogadishu. Tulifika katika gati moja boti ikasimama.
 
Abdi akasimama alifungua dawati akauchukua ule mfuko wake wa pesa akaniambia.
 
“Tushuke”
 
Tulishukia kwenye gati. Tulikuta gari ndogo ya kifahari ya rangi nyekundu ikitusubiri.
 
Abdi alifungua mlango wa nyuma wa gari hilo akaniambia nijipakie. Nikajipakia.
 
Yeye alifungua mlango wa mbele kando ya dereva akajipakia. Gari ikaondoka.
 
ITAENDELEA KESHO

No comments:

Post a Comment