Sunday, July 31, 2016

SEKESEKE LA VYETI FEKI, SEKOMU MAMBO SAFI



Tanga.Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Sebastian Kolowa (Sekomu),kimesema hakitakumbwa na wimbi linaloendelea linalotokana na mchakato wa Serikali wa kuwafichua wasio na sifa kwa sababu tangu kilipoanzishwa kinajiendesha kwa umakini.

Mkuu wa Chuo hicho,Dr Stephen Munga alitoa maelezo hayo LEO  alipokuwa akizungumza na Tangakumekuchablog mara baada ya kuzindua maonesho ya shughuli zinazoendeshwa na Sekomu yanayofanyika katika tawi lake lililopo jijini Tanga.

Alisema msimamo wa Sekomu wa tangu kilipoanzishwa kutosajili wanafunzi wanapojiunga wasio na sifa ndiyo unaokiweka huru kipindi hiki ambacho Serikali inataka kila jambo liendeshwe kwa utaratibu unaohitajika kwa chuo kikuu.

“Upepo unaovikumba vyuo vikuu nchini hautatukumba Sekomu kwa sababu tumekuwa tukishirikiana na Serikali tangu tulipoanza na msimamo wetu wa kuzingatia kanuni na sheria ndiyo unaotuacha huru hivi sasa”alisema Dr Munga.

Akizungumzia kuhusu maonesho hayo,Mkuu huyo wa Sekomu alisema yana lengo la kukiweka karibu na jamii hasa katika kipindi hiki ambacho kinakaribia kufikisha miaka 10 tangu kuanzishwa kwake lakini pia ni kuonyesha upekee wake nchini na Afrika mashariki kwa ujumla hasa katika utoaji wa elimu maalumu.
“Sekomu ni chuo cha kwanza kwa nchi za Afrika Mashariki kutoa shahada ya kwanza ya elimu maalumu,wakati tukianza  tulionekana kama chuo cha ajabu lakini tunashukuru sasa hivi vyuo vingi vimeiga kutokana na umuhimu wake katika makundi maalumu”alisema Dr Munga.

Kaimu Makamu Mkuu wa Sekomu,mipango na biashara,Geofrey Kingazi alisema miongoni mwa yanayooneshwa katika maonesho hayo ni machapisho ya kazi za utafiti na kazi zinazofanyika chuoni ukiwamo  mbinu zinazotumika kuwajengea uwezo wanafunzi wa makundi maalumu.

Khalid  Mohamed anayechukua masomo shahada ya elimu katika chuo kikuu cha Sekomu aliupongeza uongozi wa chuo hicho kikuu kwa kuzingatia sheria na kanuni ambapo wakati hivi sasa wenzao wa vyuo vingine wanapohangaika wao hawana wasiwasi kutokana na kutimiza masharti yote yanayohitajika.

                      MWISHO

No comments:

Post a Comment