Sunday, July 31, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 50

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI
 
MWANAMKE 50
 
ILIPOISHIA
 
Mzee mmoja akachungulia nje. Alimtazama Abdi kisha akanitazama mimi.
 
“Karibuni” akatuambia na kurudi ndani.
 
Abdi akaingia na kuniambia.
 
“”Karibu”
 
Na mimi nikaingia. Tulitokea katika ukumbi mpana kama  darasa. Harufu tuliyokutana nayo humo ndani ni ya udi na marashi.
 
Katikati ya ule ukumbi palitandikwa jamvi. Katika lile jamvi niliona  sinia iliyotiwa vitu mbalimbali kama vile ndizi mbivu, vipande vya miwa, mkate wa mchele, tende na vitu vingine.
 
Katika kila pembe ya lile jamvi kuliwekwa nazi moja. Jumla zilikuwa nazi nne.
 
Yule mzee wa kisomali alikuwa amesimama nyuma ya mlango.
 
Alimwambia Abdi maneno kwa lugha  ya kisomali. Abdi akaniambia mimi.
 
“Twende tukakae pale”
 
Alinionesha lile jamvi.
 
Tukaenda kukaa. Yule mzee wa kisomali alitoka uani. Baadaye akarudi tena akiwa ameshika kitabu kikubwa cha kiarabu na yeye akakaa kwenye lile jamvi.
 
Sasa niliweza kumuangalia vizuri. Nikajiuliza mbona amefanana na yule msomali niliyemuota akinichukua kule chumbani? Alikuwa  mrefu vile vile na pua yake pia ilikuwa ndefu.
 
Nikashangaa sana.
 
SASA ENDELEA
 
Mzee huyo wa kisomali akamtazama Abdi kisha akamuuliza maneno na kwa kisomali.
 
Abdi akanitazama kisha akamwambia.
 
“Amour”
 
Nikahisi labda alimuuliza jina langu.
 
Mzee wa kisomali akanitazama kisha akafungua kitabu chake. Karasa zilikuwa zimegandana akakigusisha kidole chake kwenye ulimi kukitia mate kisha akaufungua  ule ukurasa.
 
Akaanza kusoma maneno ya kiarabu. Sikuwezaa kujua alikuwa anasoma nini lakini nilisikia akitaja jina  la Zena Binti Jabal Keysi. Wakati mwingine akitaja jina langu.
 
Mara kwa mara nilikuwa nikimtazama Abdi kuona kama mwenzangu alikuwa anaelewa chochote. Abdi alikuwa amenyamaza kimya. Alikuwa ametulia kama aliyekuwa anaaguliwa.
 
Ghafla tukaona nazi iliyokuwa katika pembe moja ya lile jamvi inapasuka yenyewe. Mzee alikuwa akiendelea kusoma tu. Naizi ya pili ikapasuka. Ilipopasuka nazi ya tatu ukuta wa uliokuwa mbele yetu ulifanya ufa akatokea mtu.
 
Alikuwa mwanamke aliyevaa vizuri. Gauni alilovaa lilikuwa limedariziwa vimemeta vya dhahabu. Alikuwa amevaa mkufu wa dhahabu na bangili za dhahabu. Masikioni alikuwa amevaa vipuli vya dhahabu.
 
Kichwani kwake nywele zake zilibanwa kwa taji la dhahabu lililomfanya aonekane kama malikia wa visiwa vya Sheba.
 
Alipotokea sote tulishituka tukamtazama. Ilinichukua sekunde mbili au tatu kutambua kuwa alikuwa Zena!
 
Zena alikuwa amependeza kuliko siku zote nilizowahi kumuona. Alikuwa aking’ara kama mwezi mpevu! Sikuweza kujua ni kitu gani kilichomleta pale na kwanini alitokea katika hali tofauti na anavyotokea siku zote.
 
Siku zote nilizokutana naye alinitokea katika hali ya kawaida, si hali kama ile ya kuibuka kutoka kwenye  ufa wa ukuta. Ilikuwa hali ambayo si tu ilinitisha mimi, ilimtisha hata Abdi aliyekuwa ameketi karibu yangu. Nilimuona akimtazama kwa shauku iliyochanganyika na hofu.
 
Mzee wa Kisomali alimtazama kisha alimwambia maneno kwa lugha ya kiarabu.
 
Zena hakusema chochote. Akiwa miguu pekupeku alikuja taratibu hadi ilipokuwa ile sinia iliyokuwa na vitu akaipindua kwa miguu. Sinia ilipinduka, na vitu vyote vilimwagika chini.
 
Alipomaliza kuipindua ile sinia alimfuata yule mzee wa kisomali akampiga kibao cha shavu. Mzee alianguka chini. Hakuinuka tena. Sasa akamfuata Abdi. Abdi alipoona anafuatwa aliinuka haraka akatoka mbio. Na mimi nikainuka na kutoka mbio kumfuata Abdi.
 
Tulitoka kwenye mlango.  Abdi kama ambaye alibadili mawazo alirudi kwenye mlango huo na kuchungulia. Na mimi nikarudi kuchungulia.
 
Zena hatukumuona tena. Tulimuona yule mzee akijiinua na kukaa. Abdi akarudi. Mimi sikurudi.
 
Nilibaki kwenye mlango nikichungulia.
 
Nikawasikia Abdi na yule mzee wakizungumza kwa lugha ya kisomali. Mzee alikuwa akifoka na akimuashiria Abdi aondoke.
 
Abdi akatoka na kuniambia.
 
“Twenzetu”
 
Wakati tunatembea kurudi tulikoliacha gari Abdi hakunieleza chochote na mimi sikumuuliza chochote.
 
Nilibaki kujiuliza mwenyewe ni kitu gani kilichokuwa kimetendeka pale hadi Zena akatokea na kumwaga vile vitu na kisha kumpiga kibao yule mzee? Sikupata jibu.
 
Nilihisi kuwa jibu alikuwa analo Abdi lakini hakuonesha dalili yoyote ya kutaka kunieleza chochote. Na mimi nikashindwa kumuuliza.
 
Niliona uso wake ulikuwa umefadhaika na alikosa raha. Hakuwa hata akinitazama.
 
Tulirudi kwenye gari lake tukajipakia na  kuondoka.
 
Wakati Abdi akiendesha gari kurudi mjini aliniambia.
 
“Nina hoteli mbili. Ile unayokaa wewe na nyingine mpya. Nataka uwe mneneja wa ile hoteli yangu mpya”
 
“Nitawezaje kuwa meneja wa hoteli yako wakati nataka kuondoka?” nikamuuliza.
 
“Huwezi kuondoka bila paspoti. Subiri nikutengezee paspoti”
 
“Utanitengezea lini?” nikamuuliza.
 
“Usiwe na haraka Amour. Ninakuhakikishia kuwa nitakutengezea isipokuwa katika kipindi hiki cha kusubiri paspoti yako iwe tayari nataka uwe meneja wa hoteli yangu. Nitakupa nyumba na gari na kama utahitaji mke wa kisomali nitakutafutia msichana mrembo”
 
Abdi alianza kunitia tamaa ya maisha na kunipa ushawishi wa kubaki Somalia.
 
Hata hivyo moyo wangu ulikuwa mzito kukubaliana naye. Nilikuwa simuelewi japokuwa mipango aliyonieleza ilikuwa ya maana kwa upande wangu.
 
“Unataka kurudi Tanga, kuna nini? Kama utakaa hapa kwa muda mfupi tu Amour unaweza kupata maendeleo makubwa na ukarudi kwenu ukiwa tajiri” Abdi aliendelea kunishawishi.
 
Muda wote nilikuwa nimebaki kimya nikiyatafakari maneno yake. Alipoona nipo kimya na yeye akanyamaza. Sikuweza kujua ni kwanini aliileta ile mada ya hoteli wakati kulikuwa na tukio jingine la kuibuka kwa Zena ambalo ndilo alilopaswa kunieleza.
 
Kwanza kile kisomo alichokuwa anasoma yule mzee hadi nazi zikapasuka na Zena akatokea, nilijiuliza, kilikuwa kiosomo cha nini. Hapo pia sikupata jibu.
 
Dakika chache baadaye Abdi alilisimamisha gari mbele ya nyumba moja iliyokuwa katika mtaa mtulivu.
 
Aliniambia tushuke, tukashuka.
 
“Nifuate” akaniambia.
 
Tuliingia katika geti la ile nyumba tukakuta mafundi wakipaka rangi kwenye kuta. Alizungumza nao kwa kiomali kisha tukaingia ndani ya ile nyumba.
 
Ilikuwa nyumba nzuri na ya kupendeza. Abdi alitazama sehemu zilizokuwa zimeshapigwa rangi, akaniambia.
 
“Hii ni nyumba yangu. Ninaifanyia ukarabati kwa ajili yako. Wewe utakuja kuishi hapa”
 
“Wewe mwenyewe  unaishi wapi?”
 
“Nitakupeleka ukapaone nyumbani kwangu”
 
“Ni lini hii nyumba itakuwa tayari?”
 
“Leo watamaliza kupiga rangi. Labda keshokutwa unaweza kuhamia. Kesho nitakuwekea fanicha mpya”
 
Alifungua milango ya vyumba na kunionesha ndani.
 
“Patakufaa sana hapa” akaniambia.
 
Sikumjibu kitu. Nilikuwa bado ninajadiliana na moyo wangu kuhusu suala la kubaki pale Somalia.
 
“Amour unafikiria nini. Unataka kuiacha bahati kama hii?” Abdi aliniambia kisha akacheka peke yake.
 
“Twenzetu” akaniambia.
 
Tukatoka tena. Tulijipakia kwenye gari tukaondoka.
 
Breki ya kwanza ilikuwa mbele ya hoteli moja iliyokuwa katika mtaa mwingine. Ilikuwa hoteli ndogo ya ghorofa moja, Ilikuwa imeandikwa kwa herufi kubwa. AL ASAD.
 
“Hii ndio hoteli ambayo nitakuachia wewe, itakuwa kama mali yako kwani tutakuwa tunagawana faida kila mwezi na kila mwaka kama utapenda kuendelea kubaki Somalia” Abdi aliniambia tukiwa bado tupo kwenye gari.
 
Alipoona nilikuwa nikiiangalia angalia ile hoteli, aliniambia.
 
“Tushuke uione vizuri”
 
Tukashuka.
 
Tuliingia ndani ya ile hoteli. Kwa kweli ilikuwa imechangamka.
 
“Sasa nani anaiendesha kwa hivi sasa?” nikamuuliza.
 
“Yuko mtu lakini nitamuondoa”
 
“Sasa ni kwanini umuondoe?”
 
“Lengo langu ni kukunufaisha wewe rafiki yangu au nimefanya kosa?’
 
“Hapana. Ni vizuri”
 
Abdi alinitembeza hoteli nzima kisha tukaingia katika ofisi ya meneja.
 
Meneja mwenyewe alikuwa mtu mzima. Kichwa chake kilishaanza kutoka mvi.
 
JE WEWE MSOMAJI UMESHAPATA WAZO GANI KUHUSU HUYU ABDI? MIMI BADO SIMUELEWI! LAKINI HEBU ACHA TUENDELEE TUTAMGUNDUA TU. KWA LEO NAKOMEA HAPA. Kesho ni kama kawa kama dawa!
 

No comments:

Post a Comment