Saturday, February 21, 2015

YALIYONIKUTA TANGA SEHEMU YA (20)



HADITHI

YALIYONIKUTA TANGA (20)

ILIPOISHI TOLEO LILILOPITA

Meja akanichagua mimi na polisi mmoja mwenye bunduki tulinde ile nyumba hadi asubuhi ili mwizi asije akaingia na kuiba vitu kwani mlango wake wa mbele ulikuwa umesindikwa tu kama ambavyo tumeukuta.

Meja na polisi wengine wakaondoka na kutuacha sisi. Saa yangu iliniambia ilikuwa saa tisa na nusu usiku. Kulikuwa na baridi kali ambayo ilitupiga. Mimi ambaye nilivaa nguo nyepesi ndio niliisikia vizuri sana.

Tukakaa pale barazani kulinda ile nyumba kama tulivyoagizwa. Taa za ndani ya ile nyumba tulikuwa tumezizima. Mara tukaona zile taa zinawashwa. Tukasikia kama sauti za mapanga yakigongana pamoja na hatua za watu wanaopishana.

Wakati tumetega masikio tukisikiliza, tulisikia sauti ambayo mimi niitambua kuwa ni ya yule mwanamke ikisema.

“Chinja chinja tu sasa…kila mtu chinja….hapana kuacha…!”

Ghafla tulisikia kishindo kikubwa kwenye ule mlango wa mbele kama vile ulipogwa na kitu kizoto. Mlango huo ukafunguka na kuwa wazi huku sauti ya yule mwanamke ikiendelea kusikika.

“Chinja chinja tu sasa…kila mtu chinja….!”

SASA ENDELEA

Tulisikia kishindo cha watu waliokuwa wakikumbana kuwania kutoka katika mlango huo hku mlio wa mapanga yanyoyogongana ukisikika.

Askari mwenzangu niliyekuwa naye alikuwa wa kwanza kuinuka pale tulipokuwa tumeketi akatimua mbio. Laiti kama ule mkanda wa buduki yake usingekuwa begani angeiacha bunduki yake pale pale. Kwa vile alikuwa ameuvaa mkanda wa bunduki hiyo kwenye bega aliweza kukimbia nayo.

Nilipoona mwenzangu anatimua, na mimi nikainuka na kumuata mbio!

Tulichokikimbia hapo ilikuwa ni kuchinjwa na majini. Tulishatia imani kuwa wale walikuwa majini na ndio waliokuwa wamemchinja Sajenti Erick hivyo tilona kwamba na sisi tungechinjwa kutokana na ile sauti iliyokuwa ikiashiria kuchinja.

Tuliendelea kwenda mbio bila kutazama nyuma mpaka tukaikafika kituo cha polisi. Polisi wenzetu walitushangaa.

“Vipi?” Polisi mmoja akatuuliza.

Tukaeleza kilichokuwa kimetutoa mbio. Hapo hapo ikapigwa radio Call, gari lililokuwa kwenye doria likawasili. Mimi na mwenzangu tukapanda katika gari hilo kuelekea katika ile nyumba.

Tulipofika tulishuka na kwenda kwenye mlango. Tuliujaribu mlango na kukuta ulikuwa umeffungwa. Zile taa zilizokuwa zimewashwa tulikuta zimezimwa.

Hakukuwa na dalili yoyote iliyoonesha kuwa ndani ya nyumba hiyo mlikuwa na watu. Polisi mmoja kampigia mkuu wa zamu wa kituo kutaka apewe ruhusa ili tuvunje mlango tuingie ndani. Ile timu tuliyokwenda nayo ilikuwa haiamini mashetani.

Ruhusa ikatolewa kuwa tunaweza kuvunja mlango na kuwakamata waliokuwa ndani. Polisi mmoja aliupiga vikumbo vitatu mlango huo ukafunguka. Moyo wangu ulikuwa ukinienda mbio. Polisi wakaingia ndani, mimi nilikuwa wa mwisho kuingia.

Niliwasha taa ya ukumbini na na uani. Tukaanza kutafuta. Hatukukutamtu yeyote humo ndani. Nyumba ilikuwa tupu.

“Wako wapi?” Polisi mmoja aliyekuwa na kimbelembele akauliza kwa umori.

“Nadhani wameshaondoka” nikamjibu.

“Wameondoka wamekwenda wapi?”

“Hatuwezi kujua”

Nikapiga simu tena kituoni kuwajulisha kuwa tumevunja mlango na tumeikuta nyumba iko tupu.

Amri tuliyopewa ni kuwa tubakishe askari wawili walinde nyumba na wengine warudi kituoni. Polisi wawili wakabakishwa kulinda nyumba na waliagizwa kumkamata mtu yeyote atakayeingia mle ndani.

Tuliporudi kituoni, mimi niliruhusiwa kurudi nyumbani. Ile gari ya doria ikanipeleka nyumbani. Asubuhi kulipokucha nikaenda tena kituoni. Nikaambiwa ninaitwa kwa aisa upelelezi wa mkoa.

Nilipofika akaniambia ameshapata taarifa zote za matukio yaliyotokea usiku uliopita.

“Miujiza imekuwa mingi. Utaanza likizo yako kesho isipokuwa tufahamishe utakuwa wapi ili tutakapokuhitaji tuweze kukupata”

“Nitakuwa nyumbani Kagera”

“Sawa. Leo kamilisha taratibu za kuanza likizo, kesho utaondoka”

“Nashukuru aande”

Nikamuaga na kutoka.

Siku ya pili yake nikaanza likizo yangu. Na siku ya tatu nikaondoka kwenda Dar nikiwa nimekichukua kile kisanduku cha dhahabu. Nilikitia kwenye begi langu.

Nilipofika Dar siku iliyofuata nikatafuta usafiri wa kuelekea Kagera. Mpaka ninafika kijijini kwetu ilinichukua siku mbili. Japo nilikuwa nimekutwa na madhila huko Tanga, nilipata furaha kukutana tena na wazazi wangu pamoja na ndugu zangu ambao tuliachana kwa karibu miaka mitatu iliyopita.

ITAENDELEA

Kwa mengi mazuri na habari kemkem tembelea blog hii kila wakati kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com

No comments:

Post a Comment