Saturday, February 4, 2017

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 25

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 25
 
ILIPOISHIA
 
“Tulikuwa tumetengana kidogo…”
 
“Kwa vipi?”
 
“Niliwahi kupata matatizo kidogo ya kipolisi nikashitakiwa kwa kuhisiwa kuwa nilifanya mauaji ya msichana mmoja lakini mahakama ikaona sikuwa na hatia ikaniachia huru. Sasa niliporudi uraiani Vicky akaniambia kuwa alidhani ningenyongwa hivyo ndoa yetu alishaivunja kwa Padre”
 
“Unamfahamu mtu anayeitwa Kweka?”
 
Simon alishituka alipoulizwa swali hilo. Mshituko wake ulionekana waziwazi.
 
Akajiambia akijibu kuwa hamfahamu atajiingiza katika matatizo kwani hakujua Vicky aliwaeleza nini polisi.
 
“Namfahamu” akajibu baada ya kusita kidogo.
 
“Tueleze unavyomfahamu?”
 
“Ni rafiki yangu”
 
“Ni kweli kwamba alimuoa mke wako baada ya wewe kuwekwa ndani kutokana na kesi iliyokuwa inakukabili?’
 
Simon aligundua kuwa hilo swali lilikuwa la mtego.
 
“Vicky aliwahi kunieleza kuwa aliolewa na mtu mwingine lakini nilimwambia kuwa hakupaswa kuolewa”
 
“Alikwambia aliolewa na nani?”
 
SASA ENDELEA
 
“Hakuniambia. Labda leo baada ya kukutana naye ndio angeniambia”
 
“Baada ya kukwambia kuwa ameolewa na mtu mwingine ulikasirika sana?”
 
“Sikukasirika”
 
“Bila shaka ulitaka kumjua mtu ambaye alimuoa mke wako?”
 
“Sikutaka kumjua”
 
“Na bila shaka ulikuwa na kisasi naye?”
 
Simon akatikisa kichwa.
 
“Kisasi cha nini. Wanawake si wamejaa tele”
 
“Jana majira ya saa sita mchana ulikuwa wapi?”
 
“Nilikuwa katika shughuli zangu”
 
“Utakataa kwamba ulionekana katika hoteli ya Suzy saa sita mchana”
 
Hapo Simon hakutaka kukubali. Aliona akikubali tu atahusishwa na mauaji ya Dokta Kweka.
 
“Sikuwahi kufika katika hoteli hiyo”
 
“Vicky alikuona ukitoka katika mlango wa hoteli, ulikwenda kufanya nini?”
 
“Labda amenifananisha, sikuwa mimi”
 
“Tulikuwa tunamtafuta mtu aliyemuua Kweka. Bila shaka utakuwa ni wewe. Umemuua kwa kisasi cha kuchukuliwa mke wako”
 
“Si kweli na pia sijui kama Kweka ameuawa”
 
“Sasa nakwambia kwamba Kweka ameuawa na wewe utakuwa mtuhumiwa wetu namba mbili kwa sababu ulionekana katika eneo la tukio”
 
Simon akawekwa ndani baada ya alama zake za vidole kuchukuliwa.
 
Kwa upande mmoja alikuwa na wasiwasi wa kukabiliwa na kesi nyingine ya mauaji na kwa upande mwingine alijiambia hakukuwa na ushahidi kuwa yeye ndiye aliyemuua Kweka. Kuonekana katika eneo la tukio la mauaji hakumaanishi kwamba umeua, alijiambia.
 
Akakumbuka kwamba alipofika pale hoteli alizifuta alama za vidole vyake kwenye kitasa cha mlango wa chumba alichokuwemo Kweka na hivyo kuondoa ushahidi mwingine kuwa alifika mahali hapo.
 
Hata hivyo alimlaani Vicky kwa kujua kuwa ndiye aliyemtaja baada ya yeye kukamatwa na kusuka mipango ya kumpigia simu ili na yeye akamatwe.
 
Temba baada ya kumuweka ndani Simon alichukua gari na kuelekea hospitali ya Muhimbili ilikokuwa maiti ya Kweka ili achukue alama za vidole za marehemu.
 
Alikuwa na shaka sana na Simon. Alijiambia upo uwezekano mkubwa kuwa Simon ndiye aliyemuua Kweka kwa sabubu ya kumchukulia mke wake.
 
Alipofika hospitali ya Muhimbili Temba alitaka apelekwe mochwari ili achukue alama za vidole za Kweka kwa ajili ya uchunguzi wao. Alipelekwa mochwari na kufunguliwa sehemu iliyokuwa imewekwa mwili wa Kweka.
 
Kwa mastaajabu makubwa, mwili wa Kweka haukuonekana! Mhudumu wa mochwari alidhani mwili huo ulikuwa umewekwa sehemu nyingine, akaanza kutafuta. Nusu saa baadaye ikagunduliwa kuwa mwili wa Kweka haukuwemo mochari.
 
Ulikuwa umetoweka!
 
Kulikuwa na maiti tatu ambazo zilichukuliwa na jamaa zao asubuhi ile. Kwa kushuku kwamba mwili wa Kweka ulitolewa kwa makosa. Temba azunguka na gari katika sehemu zote zilikopelekwa maiti hizo na kugundua kuwa maiti ya kweka haikuwa miongoni mwa maiti zilizotolewa.
 
Akarudi kituoni kutafakari suala la kupotea kwa maiti ya Kweka. Mara tu alipoketi, polisi mmoja aliingia ofisini mwake na kumwambia.
 
“Afande kuna jambo la kutatanisa”
 
“Jambo gani?”
 
“Yule mtu aliyeuawa jana amekuja akiwa mzima, anataka mke wake atolewe!”
 
“Eti nini? Unamaanisha Kweka?’
 
“Kweka ndiyo”
 
“Haiwezekani! Kweka amekufa na nimeishuhudia maiti yake!”
 
“Yuko nje afande!”
 
“Mlete”
 
Polisi huyo alitoka. Baada ya dakika chache aliingia akiwa amefuatana na Dokta Kweka.
 
Temba alimtolea macho ya mshangao. Kweka alimpa mkono Temba ili kumsalimia. Temba akaukwepa.
 
“Wewe nani?” akamuuliza.
 
“Mimi Dokta Kweka” 
 
“Natoka kuzimu!” Kweka alijibu.
 
Uso wa Temba ulinywea, akamtazama yule polisi aliyengia na daktari huyo.
 
“Nenda kamlete Vicky” akamwambia.
 
Polisi huyo alitoka. Baada ya muda kidogo aliingia akiwa na Vicky. Vicky alishituka alipomuona Kweka ndani ya ofisi hiyo.
 
“Huyu ndiye mke wako?” Temba akamuuliza Kweka.
 
“Ndiye yeye”
 
Vicky alikuwa bado akimshangaa Kweka.
 
“Mke wangu nimekufuata twende zetu” Kweka akamwambia Vicky.
 
“Wewe si uliuawa?” Vicky akamuuliza kwa mshangao.
 
Kweka alikenua midomo akacheka. Akamshika mkono Vicky huku akimtazama Temba.
 
“Kuna kesi yoyote inayomkabili?” akamuuliza.
 
“Kesi inahusu kuuawa kwako wewe” Temba alimjibu.
 
“Sasa mimi niko hapa. Mmeniona niko hai, bado kuna kesi tena?”
 
“Na maiti yako pia imetoweka kule hospitali!”
 
“Kwa hiyo sidhani kama kuna kesi tena”
 
Temba akanyamaza kimya.
 
“Namchukua”
 
Kweka alitoka na Vicky huku Temba na polisi mwenzake wakimkodolea macho.
 
Walipotoka, Temba alimtazama yule polisi mwingine.
 
“Anasema anatoka kuzimu!”
 
“Ni maajabu ya mwaka. Nimepata hofu sana”
 
Masaa mawili baadaye Simon naye aliachiwa na kesi ikafutwa kimyakimya.
 
                                     *************
 
Mara tu Simon alipoachiwa alikwenda New Africa kuliangalia gari alilokuwa ameliacha asubuhi alipokamatwa. Akalikuta mahali pale pale alipoliegesha. Alifungua mlango akaitazama ile bastola aliyokuwa ameificha chini ya siti, akaiona ipo. Akajipakia na kuondoka.
 
Alikwenda nyumbani kwa James. Wakati anafika James naye alikuwa anatoka na gari. Alipomuona Simon akashuka kwenye gari.
 
“Vipi mbona hukutokea asubuhi?” akamuuliza.
 
“Nilikamatwa na polisi, nimeachiwa sasaa hivi” Simon alimjibu huku akishuka kwenye gari.
 
“Ulikamatwa kwa kosa gani?”
 
“Kwa mauaji ya Kweka. Tuingie ndani tuzungumze”
 
James alifunga mlango wa gari yake akaingia nyumbani kwake huku Simon akimfuata nyuma. Wakati anapita mlangoni alimwambia Simon.
 
“Karibu ndani”
 
Walikwenda kuketi sebuleni.
 
“Niambie imekuwaje?” James akamuuliza kwa wasiwasi.
 
“Jana wakati natoka pale hoteli baada ya kumuua Kweka nilimuona yule mke wangu Vicky akishuka kwenye teksi, kumbe na yeye aliniona. Nafikiri baada ya yeye kukamatwa na polisi alinitaja mimi”
 
“Kwanini akutaje wewe?”
 
“Alinitaja kwa kudhani nilikuwa na kisasi na Kweka na hivyo polisi walihisi kwamba mimi ndiye niliyemuua”
 
“Sasa walikupata wapi?”
 
“Walitumia mbinu. Walimwambia Vicky anipigie simu kutaka nikutane naye New Africa Hotel. Nilipofika New Africa nikakamatwa”
 
“Na huyo Vicky ulikutana naye hapo?”
 
“Ndiyo nilikutana naye. Wakati tunazungumza ndio polisi wakatokea na kunikamata”
 
“Mlipofika kituo cha polisi ikawaje?”
 
“Mimi nilikanusha kumuua Kweka na pia nilikanusha kufika katika hoteli ya Suzy. Niliwekwa ndani tangu asubuhi. Hii saa tisa ndio wakaniachia”
 
ITAENDELEA kesho, Usikose

No comments:

Post a Comment