Thursday, February 23, 2017

HADITHI ALIYEMUUA MCHUMBWA WANGU SEHEMU YA 36

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU
 
ILIPOISHIA
 
Walipofika nyumbani kwa Mwana Alphonce alioneshwa chumba atakachokuwa akikaa mpaka hapo atakapoondoka kurudi Dar es Salaam. Kilikuwa chumba kipana kilichokuwa na kila kitu.
 
“Utakaa kwenye chumba hiki. Nafikiri kila kitu kimo. Kama kutakuwa na kitu zaidi unahitaji utaniambia” Mwana limwambia Alphonce.
 
Alphonce alikuwa amefungua sanduku lake akitoa vitu vilivyokuwemo. Mwana akamfungulia kabati.
 
“Kabati lina nafasi ya kutosha kuweka vitu vyako. Hakuna kitu zaidi ya shuka na taulo”
 
Alphonce alianza kupanga vitu vyake kwenye kabati.
 
“Endelea kupanga, mimi niko sebuleni” Mwana akamwambia Alphonce na kutoka.
 
Alphonce aliendelea kupanga nguo zake na vitu vyake vingine. Alipomaliza alilifunga kabati na kutoka. Alikwenda sebuleni akaketi na Mwana.
 
“Naomba unipatie lile gazeti”
 
“Liko kwenye mkoba wangu” Mwana limwambia na kuuchukua mkoba wake uliokuwa kando yake akaufungua na kulitoa gazeti hilo.
 
“Hili hapa”
 
Alimpa Alphonce ambaye alifungua ukurasa wa nne uliokuwa na zile habari zilizomuhusu. Akazisoma tena.
 
SASA ENDELEA
 
“Zimekutia wasiwasi?”
 
“Hapana, ninashangaa huu upotoshaji wa habari zinyewe”
 
“Upotoshaji upi?”
 
“Hapa wanasema kwamba huyu kijana ameuawa kwa kisasi na si kwa wizi”
 
“Ni kwa sababu polisi hawakupata ukweli”
 
“Wameegemea kwenye maelezo ya yule kijana aliyewambia kuwa walikuwa wanatembea wakavamiwa na mtu wakati ukweli ni kwamba wote walikuwa ni wezi. Walikuwa vijana watatu”
 
“Lakini ninaamini hakutakuwa na tatizo kwa upande wako, hawatakupata”
 
“Mimi bado nitakuwa hapa Lagos kwa wiki nzima”
 
“Hata ingekuwa ni kwa mwezi mzima. Watu wanauawa kila siku katika jiji hili. Hakuna anayekamatwa”
 
“Yaani jiji hili liko hivyo?”
 
“Ni majiji yote makubwa. Pale Johannasburg kila saa moja kunakuwa na tukio la mauaji, haijambo hapa Lagos. Unataka uniambie Dar es Salaam hakuna mauaji?”
 
“Mauaji yapo”
 
“Sasa…usidhani ni hapa tu. Miji inapokuwa mikubwa ina mengi. Mdogo wangu aliuawa mbele yangu mwaka juzi kwa risasi. Waliomuua hawajapatikana hadi leo!”
 
“Aliuawa kwa sababu gani?”
 
“Haikujulikana. Waliomuua walikimbia na gari lakini ilidaiwa kwamba alikuwa akichukua mke wa mtu”
 
“Huyo mtu mwenye huyo mtu alifahamika?”
 
“Sasa la ajabu ni kwamba wakati polisi wanamfuatilia mtu huyo, naye akauawa na watu wasiojulikana!”
 
“Kwa hiyo mauaji yanaonekana ni kitu cha kawaida hapa Lagos?”
 
“Kama nilivyokwambia ni katika majiji yote makubwa si Lagos peke yake. Polisi wanadanganya tu kueleza kuwa wanamtauta muuaji, watu wakisahau na habari inaisha”
 
Alphonce alitingishatingisha kichwa chake kumkubalia Mwana kabla ya kumwambia.
 
“Ndiyo unataka nije niishi hapa?”
 
“Ndiyo. Unakuja kufanya kazi”
 
“Katika jiji hili la mauaji!”
 
“Umeanza kupata hofu. Ni wazi kuwa hutaweza kuishi mahali popote katika dunia hii ya leo kwa sababu mauaji yapo kila mahali mpaka Marekani na Ulaya. Lakini wanaouana wana visasi vyao ambavyo wewe havikuhusu”
 
“Nakumbuka siku moja Dar es Salaam wakati nikiwa mwanaunzi wa chuo kikuu, mwanaunzi mwenzetu alipigwa risasi tatu na watu wawili waliokuwa wamepanda pikipiki na hawakupatikana hadi leo”
 
“Hiyo ndiyo hali ya ulimwengu wa leo”
 
Wakati wanazungumza mtumishi wa ndani wa Mwana alipita akielekea uani. Mwana alimuita.
 
“Nataka nikutambulishe kwa mgeni wetu” Mwana alimwambia na kumuionesha Alphonce.
 
“Huyu mtu unayemuona ni mgeni wetu atakuwa hapa nyumbani kwa siku kadhaa”
 
“Sawa. Nimemuona” Eda alijibu huku akimtazama Alphonce.
 
“Karibu sana” akamwambia.
 
“Asante” Alphonce alimjibu.
ITAENDELA

No comments:

Post a Comment