Tuesday, February 21, 2017

MBUNGE JIMBO LA TANGA MJINI, MUSSA MBAROUK AUNGA MKONO MAPAMBANO MADAWA ILA-----



Tanga, MBUNGE wa jimbo la Tanga mjini, Mussa Mbarouk (CUF) amesema anaunga mkono   vita ya kupambana na madawa ya kulevya ila ukamataji na utajaji wa majina unatakiwa kufuata sheria.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana akizungumzia ukamatwaji wa Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Mussa alisema ionekanavyo ni kuuwa upinzani nchini.
Alisema kitendo cha jeshi la polisi kuzingira nyumbani kwake amekitaja kuwa ni vitisho lengo lake ni kuwabadilisha Watanzania kifikra ili CCM iendelee kutawala.
“Naunga mkono mapambano ya madawa ya kulevya kwa waingizaji wauzaji na hata watumiaji, ila mifumo yake inakinzana na haki za binadamu” alisema Mussa na kuongeza
“Katika jimbo langu nimeanza harakati za kuhakikisha biashara ya madawa ya kulevya inatokomezwa na kuvunja vijiwe vyote vya watumiaji wa mirungi na unga” alisema
Akizungumzia vijana kufanya kazi na kuacha kukaa vijiweni  Mbunge huyo alisema kuna fursa nyingi za kufanya ikiwemo kuunda vikundi na kupata mikopo.
Alisema kuna baadhi ya vijana wamekuwa wakishinda vijiweni na kushindia kahawa wakati fursa nyingi za kujipatia kipato zikiwepo na kuwakumbusha kuwa wanaweza kuja wageni na kuzichukua.
Alisema ujio wa bomba la mafuta ni fursa nzuri kwa vijana kuchangamka kwa kubuni miradi na kuunda vikundi kuweza kunufaika na mikopo katika taasisi za fedha.
“Ujio wa bomba la mafuta ni fursa nzuri kwa vijana kubuni aina ya miradi na kuunda vikundi, watakuja wageni na kuhodhi maeneo muhimu na mwisho kujutia” alisema
Aliwataka vijana wa Tanga kutambua kuwa miaka mitano mbeleni Tanga itakuwa Mkoa wa kibiashara jambo ambalo litawavutia watu wengi wa ndani na nje ya nchi baada ya bomba la mafuta kukamilika.
                                            Mwisho


 Mbunge wa Tanga mjini, Mussa Mbarouk (CUF) akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuzungumzia vita ya madawa ya kulevya na ukamataji wake.




No comments:

Post a Comment