Thursday, January 29, 2015

YALIYONIKUTA TANGA (7)

HADITHI HII INALETWEA KWENU KWA HISANI YA MKOMBOZI SANITARIUM CLINIC MABINGWA WA TIBA ASILI, WAPO CHUDA TANGA, 0654 361333
 
YALIYONIKUTA TANGA (7)
 
ILIPOISHIA JUMATATU ILIYOPITA
 
Nikakata simu na kumfuta yule kijana wa bodaboda.
 
“Shilingi ngapi?” nikamuuliza.
 
“Ni elfu mbili tu”
 
Nikatoa noti za shilingi elfu mbili na kumpa.
 
“Baadaye nitakupigia uje unichukue, sawa?”
 
“Itakuwa saa ngapi?”
 
“Sijajua lakini haitakuwa saa nyingi sana”
 
“Sawa”
 
Kijana akaondoka na pikipiki na kuniacha pale pale. Nilisimama kwa dakika kadhaa huku nikitazama kila upande kwa tamaa ya kumuona yule msichana. Nilipoona muda unazidi kwenda nikampigia.
 
“Nimekuchelewesha?” akaniuliza.
 
“Naona muda unazidi kwenda sioni mtu”
 
“Sasa sikiliza nikwambie, fuata hiyo njia ya miguu iliyoko nyuma ya huo mbuyu uje moja kwa moja. Mbele yako utakuta mwembe, utakata kushoto…”
 
SASA ENDELEA
 
“Si uliniambia utanifuata hapa?” nikamuuliza.
 
“Ndiyo lakini kuja huko nimeshindwa, mwenzko naogopa. Lakini wewe mwanume unaweza kuja tu”
 
“Kwani wewe uko wapi?”
 
“Niko huku nilikokuonesha”
 
Nikatupa macho katika eneo hilo lilioko nyuma ya ule mbuyu. Niliona pori tupu.
 
“Kwani kuna nyumba huko?”
 
“Ziko nyingi tu”
 
“Ngoja nije”
 
“Njoo, nikikuona nitakufuata”
 
Nikakata simu na kwenda nyuma ya ule mbuyu. Nikaona njia ya miguu iliyoelekea kwenye pori. Halikuwa pori la kutisha bali lilikuwa la miti ya mikoroshi na nyasi. Nikaifuata ile njia. Nilikwenda taratibu huku nikiangaza macho mbele ya lile pori.
 
Kitu kilichonipa matumaini ya kuwepo na nyumba ni kwamba nilipishana na watu wawili waliokuwa wakitoka katika eneo hilo. Nilikwenda hadi nikauona ule muwembe. Kulikuwa na njia upande wa kulia na upande wa kushoto wa muwembe huo.
 
Nikakumbuka msichana aliniambia nishike njia ya upande wa kushoto. Nikashika njia hiyo. Baada ya kupiga hatua kadhaa nilianza kuona nyumba moja moja. Nyingine zilikuwa zimekamilika, nyingine zilikuwa bado.
 
Msichana akanipigia simu, nikaipokea.
 
“Nimeona mtu anakuja, sijui ni wewe?” akaniuliza.
 
“Labda ni mimi kwa sababu niko peke yangu”
 
“Umevaa tisheti nyekundu?”
 
“Ndiyo”
 
“Basi ni wewe, ngoja nikufuate”
 
“Kwa hiyo nikusubiri hapa nilipo au niendelee?”
 
“Njoo tu na mimi ninakuja. Tutakutana”
 
Msichana akakata simu. Nikaendelea kwenda. Mara nikaona msichana anakuja mbele yangu. Alikuwa amevaa dera la mauaua. Nikahisi alikuwa ndiye yeye.
 
Alipofika karibu yangu nikasimama, akaja akasimama mbele yangu.
 
“Nafikiri wewe ni mgeni wangu” akaniambia huku akitabasamu.
 
“Bahati mbaya hatukuwa tumeulizana majina. Lakini natumaini ni mgeni wako”
 
“Sawa. Mimi naitwa Maimuna. Wewe unaitwa nani?”
 
“Mimi naitwa Martin”
 
“Nimefurahi kukufahamu, karibu nyumbani”
 
Nikafuatana na yule msichana kuelekea kule alikotoka.
 
Ingawa kulikuwa na giza, sura ya yule msichana haikuwa ngeni machoni kwangu. Nilikumbuka kwamba niliwahi kumuona mahali fulani pale pale Tanga lakini sikuweza kukumbuka vizuri nilimuona mahali gani na sikutaka kumuuliza.
 
“Maimuna unaishi na nani?”
 
“Naishi na mama yangu”
 
“Ndiyo mmejenga huku?”
 
“Ndiyo tulikopata kiwanja”
 
“Lakini baada ya muda si mrefu kutakuwa ni mji”
 
“Karibuni eneo lote limeshapimwa isipokuwa watu wenyewe hawajaanza kujenga. Wengine wameanza lakini wanakwenda taratibu”
 
“Nyinyi mmeshakamilisha nyumba yenu?”
 
“Bado kidogo. Lakini tumeamua kuhamia hivyo hivyo. Si unajua adha ya nyumba za kupanga?”
 
“Ninaijua. Mmefanya uamuzi mzuri. Mtakamilisha kidogo kidogo wenyewe mkiwemo ndani”
 
“Bora tumepiga bati na tunaweza kukaa, mambo mengine yatafuata. Hatunaharaka”
 
Tukatokea mbele ya nyumba moja kama boma lakini lilikuwa limepigwa bati. Ilikuwa imezungukwa na miti ya mikoroshi.
 
“Hapa ndio nyumbani” Msichana akaniambia na kuongeza.
 
“Karibu ndani”
 
Alikuwa ametangulia kwenye mlango akausukuma na kuingia ndani.
 
“Karibu” akaniambia.
 
Nikamfuata. Tulitokea kwenye chumba kama sebule. Hakikuwa kimesakafiwa na hata kuta za chumba hicho hazikuwa zimepigwa lipu. Juu kulikuwa wazi. Hakukuwa na dari.
 
Sebule yenyewe ilikuwa shaghalabaghala. Kulikuwa na makochi mawili yaliyokuwa yamechakaa na meza moja. Taa ya fanusi ilikuwa imening’inizwa katikati ya chumba hicho.
 
“Karibu ukae” msichana akaniambia.
 
Nilikaa kwenye kochi mojawapo. Nikimlinganisha msichana huyo na ile nyumba vilikuwa ni vitu viwili tofauti. Msichana alikuwa mzuri na mrembo kuliko maelezo lakini nyumba aliyokuwa akiishi ilikuwa inatisha.
 
Lakini sikujali. Nilikuwa nimevutika na yule msichana. Nilijiambia anafaa hata kumuoa.
 
Msichana aliongeza mwanga wa ile taa ya fanusi kisha akaniambia.
 
“Nisubiri kidogo”
 
Alielekea uani.
 
Nikamsubiri. Hapo hapo simu yangu ikaanza kuita. Nikaitoa mfukoni na kuona namba ya kachero mwenzangu ambaye nyumba zetu zilikuwa jirani.
 
“Vipi John…?” nikamuuliza mara tu nilipopokea ile simu.
 
“Umepata taarifa yoyote kumhusu Sajenti Erick?” Sauti ya John ikaniuliza.
 
“Sijapata taarifa yoyote”
 
“Nimesikia Sajenti hakuripoti leo kazini na mke wake amekwenda kulalamika kituoni usiku huu kuwa mume wake hajamuona tangu asubuhi na hajulikani aliko”
 
“Niko mbali kidogo. Nikirudi nyumbani tutazungumza”
 
“Sawa.
 
 
Endelea kufuatilia hadithi hii kesho
Kwa maoni na ushauri piga namba 0655 9029292 au kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com
 

No comments:

Post a Comment