Monday, February 9, 2015

YALIYONIKUTA TANGA SEHEMU YA (14)



HADITHI

YALIYONIKUTA TANGA (14)

ILIPOISHIA TOLEO LILILOPITA

Baada ya kumaliza maelezo yake ambayo yaliwashangaza maafisa hao, kamanda wa polisi akataka na mimi nieleze kilichotokea.

“Kwanza ulifikaje katika eneo hilo na ulikuwa na Sajenti Erick au ulikuwa peke yako?” akaniuliza.

“Nilikwenda peke yangu” nilimjibu.

“Kufuata nini?”

Niliona kama nitauma uma maneno nitajikuta nikiwekwa ndani, jambo la msingi ni kueleza ukweli wote.

“Kuna msichana niliwasiliana naye kwenye simu akataka nimfuate katika eneo hilo”

“Ni nani?”

“Wakati tunawasiliana nilikuwa simjui lakini baadaye niligundua alikuwa ni yule msichana ambaye mama yake tulimshitaki kwa kukutwa na kete za madawa ya kulevya na mama mwenyewe akafia mahabusi”

“Umesema wakati mnawasiliana ulikuwa humjui,?”

“Nilikuwa simjui”

“Uliwasiliana vipi na mtu ambaye ulikuwa humjui?”

SASA ENDELEA.

Swali hilo lilinifanya nieleze ukweli wa tukio zima la kuwasiliana na Maimuna. Nilianzia pale alipokosea namba akanitumia meseji. Kamanda baada ya kunisikiliza aliniuliza.

“Kwa hiyo ulipokuwa unakwenda kuonana naye ulikuwa na madhumuni gani?”

“Nilikuwa nataka tuwe marafiki, si unajua afande mimi sina mke”

Nilipojibu hivyo Kamanda wa polisi akamtazama Afisa upelelezi kisha akaendelea kunihoji.

“Enhe, ulipofika hapo mahali alipokwambia mkutane nini kilitokea”

“Nilipofika pale sikumkuta, nikampigia simu kumuuliza yuko wapi”

“Ndiyo”

“Akanijibu kwamba yuko nyumbani kwao hivyo nimfuate na akanielekeza njia ya kufika nyumbani kwao”

“Ukaenda?”

“Nikaenda. Njia yenyewe ni ya kwenye mapori. Mahali kwenyewe kuna nyumba moja moja na kuko giza”

“Ulipofika?”

“Nilikutana naye njiani. Akanipeleka kwenye hiyo nyumba. Tuliingia ndani akanikaribisha ukumbini halafu yeye aliondoka akaniambia nimsubiri. Lakini kuna kitu kimoja nataka kueleza”

“Eleza”

“Yule msichana nilimgundua kuwa ni yule ambaye mama yake alishitakiwa kwa kukutwa na madawa ya kulevya hivi karibuni akafia mahabusi. Nadhani unakumbuka afande”

“Nakumbuka na niliambiwa alikuwa na binti yake ambaye aliwatoroka” Kamanda alimwambia.

“Basi huyo binti ndiye huyo msichana mwenyewe”

“Kwa hiyo hakushituka kukuona”

“Hakushituka”

“Na wewe hukumuuliza kitu?”

“Wakati kumbukumbu zinanijia kujua ni yeye alikuwa ameshaondoka na kuniacha peke yangu pale ukumbini ambako aliniambia nimsubiri”

“Alikwambia anakwenda wapi?”

“Hakuniambia. Basi pale pale nilipitiwa na usingizi wa ghafla. Nilipozinduka ilikuwa saa tisa usiku. Yule msichana sikumuona…” nikaendelea kueleza kilichotokea baada ya hapo.

Kile kisa kiliwafanya maafisa hao wa polisi watazamane kwa mshangao.

“Una maana yule mwanamke aliyekufa ulimkuta akiwa mzima akichimba kaburi?” Afisa upelelezi ndiye aliyeniuliza.

“Ndiyo. Mimi nilishangaa sana kumuona” nikamjibu.

“Umetuambia kwamba watu hao ni majini?” Kamanda akauliza.

“Ni majini. Hata wenzangu waliokuja wameona kuwa ni majini”

“Hivi majini ni imani tu au ni viumbe kweli?”

“Kwa tukio hili mimi nimethibitisha kwamba majini si imani, wapo!”

“Kwa hiyo majini ndio wamemchinja Erick?’


“Ndio. Nafikiri ni kwa kisasi cha ile kesi kwa sababu yeye na mimi ndio tuliomkamata yule mwanamke”

“Kwa hiyo walikuwa wanataka kukuchinja na wewe?”

“Ndiyo”

“Kwa vile kuna tukio la mauaji ya polisi na kiserikali hatuamini kuwepo majini, tutawachukulia kuwa hao ni watu na inabidi tukio zima lithibitishwe” Kamanda wa polisi akaniambia kisha akamtazama Afisa upelelezi.

“Itabidi tufike katika eneo hilo la tukio, tupige picha pamoja na kuchukua maelezo kwa watu wa karibu na eneo hilo” Afisa upelelezi akamwambia kamanda.

“Sawa, itabidi tufike”

“Kuna mtu mmoja tumekuja naye kwa ajili ya kuandikisha maelezo” Yule inspekta niliyekuwa naye akasema.

“Ni nani?” Kamanda akamuuliza.

“Ni mwananchi tu mkazi wa jirani na mahali palipotokea hilo tukio na ndiye aliyetupigia simu kutujulisha kuwa kuna polisi waliolala juu ya makaburi”

“Hebu mlete hapa”

Inspekta alitoka na baada ya muda kidogo alirudi akiwa na mtu huyo.

Aliwasalimia wale maafande kwa uoga.

“Karibu sana” Kamanda alimwambia ili kumtoa hofu.

“Asante” Mtu huyo alijibu.

“Hebu tueleze ulichokiona huko Magomeni hadi ukapiga simu polisi” Kamanda alimwambia.

“Niliona polisi wamelala juu ya makaburi saa kumi na mbili asubuhi wakati nakwenda shamba, ndio nikapiga simu”

“Hao polisi walikuwa wamelalaje?” Kamanda alimuuliza.

“Walikuwa wamelala usingizi kabisa na walikuwa na bunduki”

“Hapo mahali ulipowaona palikuwa na nyumba?”

“Hapana, lile ni eneo la makaburi tu”

Kamanda wa polisi akanitazama kabla ya kuuliza tena.

“Tumepata maelezo kwamba wale askari waliingia kwenye nyumba, wakazirai na walipozinduka wakajiona wako juu ya makaburi na ile nyumba hawakuiona tena”

“Inawezekana. Pale mahali panatokea miujiza mara kwa mara. Inasemekana pana majini”

“Wewe uliwahi kuwaona?”

“Mimi sijawahi kuwaona lakini kuna mtu aliwahi kuona mwanamke mrefu kama mnazi amesimama pale usiku”

“Alipomuona nini kilitokea?”

“Yule mtu alikimbia na aliuporudi tena akiwa na wenzake, huyo mwanamke hawakumuona tena”

Je nini kitafuatia? Usikose kuendelea na hadithi hii kesho.
Nakuhakikishia kukufikishia kila kinachonifikia mtu wangu kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com
                                

No comments:

Post a Comment