Tuesday, May 5, 2015

SOMA MAKUBWA YALIYOJIRI MAGAZETINI LEO MAY 05 TZ

Uchambuzi huu unaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha Elimu Cha Candle Education Centre Tanga. Kituo kipo Tanga mkabala na Bank ya CRDB simu 0715 772746

red
MWANANCHI
Nchi imesimama. Hii ndiyo sentensi inayofaa kuelezea tukio la jana la mgomo wa madereva nchini kote ambao kwa mara ya kwanza ulisababisha mabasi yote kutoka Dar es Salaam kwenda mikoani na nchi jirani kushindwa kuondoka.
Hii ni mara ya kwanza katika historia ya Kituo Kikuu cha Mabasi Ubungo (UBT), kushindwa kutoa huduma kwa sababu yoyote ile.
Tangu asubuhi hadi jioni, hakuna basi hata moja lililotoka wala kuingia katika kituo hicho hadi abiria walipoanza kukata tamaa na baadhi yao kuondoka na wengine kuanza kushinikiza kurejeshewa nauli.
Mgomo huo ambao ni mwendelezo wa ule uliofanyika Aprili 9, mwaka huu ulipewa uzito na madereva hao baada ya ahadi walizopewa na Serikali kutofanyiwa kazi kama ilivyoahidiwa na Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka.
Tofauti na wa awali, safari hii mpaka inatimu saa 11.00 jioni hakuna kiongozi yeyote aliyejitokeza katika kituo hicho kusikiliza kilio cha madereva hao.
Hata hivyo, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ameunda kamati ya iliyotangazwa na Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta ya kusimamia usafiri barabarani itakayowakutanisha wadau wote ili kutatua matatizo katika sekta hiyo kila yanapotokea.
Tangu saa 2.30 asubuhi, polisi walijaribu kuyasindikiza mabasi waliyodhani madereva wake wako tayari kuondoka Ubungo lakini walishindwa baada ya kutoungwa mkono.
Mkuu wa Trafiki Ubungo, Inspekta Yussuf Kamotta akiwa na Inspekta Solomon Nkindwa ambaye pia ni mkaguzi wa magari, waliingia katika basi la Kampuni ya Master City na kuliondoa kituoni hapo wakiwa na mmiliki wa kampuni hiyo, Abdallah Mohammed huku wakimtafuta dereva bila mafanikio na kulazimika kulitafutia sehemu salama ya kuliegesha baada ya madereva kulizingira.
Kutokana na vurugu zilizotokea nje ya kituo hicho, polisi walilazimika kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya watu waliokuwa katika makundi.
Nje ya UBT, magari sita ya polisi yaliegeshwa katika makutano ya barabara za Sam Nujoma, Nelson Mandela na Morogoro wakati mengine yakielekea Mwenge na Buguruni kwenda kukabiliana na tishio lolote ambalo lingeweza kutokea.
MWANANCHI
Raia watatu wa Ugiriki na Mtanzania mmoja wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na shtaka la kughushi  muhuri wa Mkuu wa Jeshi Polisi Nchini (IGP).
Akisoma hati ya mashtaka  jana, Wakili wa Serikali, Mununila Munisi  alidai mbele ya Hakimu Mkazi,  Emilius Mchaulu  kuwa washtakiwa walitenda kosa hilo katika tarehe na muda usiofahamika wilayani Ilala.
Alidai kwamba katika shtaka la kwanza washtakiwa hao kwa pamoja kwa nia ovu, walighushi muhuri huo wa IGP wakionyesha ni halali na umetolewa na Jeshi la Polisi la Tanzania wakati wakijua si kweli.
Shtaka la pili wanadaiwa kuwa katika tarehe zisizofahamika jijini Dar es Salaam, walighushi taarifa ya upotevu wa mali inayotolewa na jeshi  hilo la polisi wakionyesha ni halali  na imetolewa na polisi wakati wakijua siyo kweli.
Washtakiwa wote walikana mashtaka hayo na upande wa mashtaka ulidai upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na kuomba ipangwe tarehe nyingine.
Hakimu aliwataka washtakiwa hao wawe na wadhamini wawili wa kuaminika na kila mmoja atasaini bondi ya Sh5 milioni .
Pia, washtakiwa hao hawaruhusiwi kutoka nje ya Mkoa wa Dar es Salaam bila kibali cha mahakama na wametakiwa kuwasilisha hati zao za kusafiria.
Washtakiwa wote walishindwa kutimiza masharti hayo na hivyo wamerudishwa rumande.
NIPASHE
Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge, amefungua kesi ya kikatiba dhidi ya Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma na maazimio ya Bunge kuhusiana na malalamiko ya ukiukaji wa maadili ya uongozi.
Chenge, anatuhumiwa kupokea fedha kutoka kwa Kampuni ya VIP Engineering and Marketing Ltd Sh. bilioni 1.6.
Chenge aliitwa katika Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma kuhojiwa kuhusiana na tuhuma hizo ambazo ni kinyume cha maadili.
Hata hivyo, alipinga akisema kuwa baraza hilo halina mamlaka ya kumhoji kwa kuwa liko katika Mahakama ambayo ina mamlaka kuliko baraza, na kueleza kuwa atafungua kesi ya kupinga mahakamani.
Katika maombi yake, lililowasilishwa masjala kuu ya Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Chenge ameorodhesha sababu 13 za kupinga mwenendo wa  baraza na mapendekezo yaliyowasilishwa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Kamati ya Bunge na Hesabu za Serikali (PAC) kuhusiana na shauri hilo.
NIPASHE
Wakati kukiwa kumebaki miezi mitano kufanyika uchaguzi mkuu, Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, ametamka kuwa safari hii hatakubali kunyang’anywa urais wa Zanzibar kama ilivyozoeleka katika chaguzi zilizopita.
Maalim Seif alitoa kauli hiyo juzi jioni baada ya wafuasi wa CUF kufika nyumbani kwake Mbweni, Zanzibar kwa ajili ya kumkabidhi Sh. 1, 500,000 za kuchukulia fomu ya kugombea urais.
“Safari hii, wakitaka wasitake, nakuwa Rais wa Zanzibar kwa ridhaa ya wananchi,” Maalim Seif.
Alidai kuwa CUF kimekuwa kikishiriki uchaguzi mkuu tangu mfumo wa vyama vingi vya siasa na kushinda chaguzi hizo zilizopita, lakini hakipewi ushindi.
CUF kilimsimamisha Maalim Seif kugombea urais mwaka 1995, 2005 na 2010 .
Maalim Seif alisema uchaguzi wa mwaka huu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, hakuna atakayemzuia kuchukua dola kwani CUF kina kila sababu ya kushinda.
NIPASHE
Idadi ya watu wanaoingia nchini kutoka Burundi kukimbia machafuko ya kisiasa kupitia mkoani Kigoma, imezidi kuongezeka kutoka 1,645 hadi kufikia  1,852.
Kati ya hao,  1,252 tayari wameshasajiliwa kama wakimbizi rasmi na kupelekwa katika kambi ya Nyarugusu, wilayani Kasulu.
Hayo yalibainishwa na msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Isaac Nantanga, wakati wa mahojiano na
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na wizara ya mambo ya ndani juzi, hadi  kufikia Aprili 30, mwaka huu, mkoa huo  ulikuwa umeshapokea idadi ya watu 500 walioingia kupitia vijiji sita vya Kibuye, Kagunga, Kosovo, Kakonko, Sekeeye na Kigaye.
Kwa mujibu wa msemaji huyo, hali ya usalama katika maeneo ya mipakani, imeimarishwa na kutoa wito kwa wakazi wa maeneo hayo kutoa taarifa kwa uongozi wa vijiji iwapo kuna mgeni asiyefahamika kufika maeneo hayo.
Kwa upande wake, Afisa wa Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Kigoma, Maurice David, alisema hadi juzi jioni idadi ya wakimbizi walioingia mkoani humo ilifikia 1,645.
Hata hivyo, aliongeza kuwa idadi ya wakimbizi waliofika kabla ya kuzuka upya kwa vurugu hizo nchini humo ilikuwa 46, lakini hadi jana mkoa mzima ulikuwa umepokea jumla ya wakimbizi takribani I, 852.
Burundi imekumbwa na vurugu kutokana na maandamano yanayofanyika kwenye mji mkuu wa nchi hiyo Bujumbura, kwa wananchi kupinga hatua ya Rais Pierre Nkurunziza kutaka kugombea tena urais kwa muhula wa tatu kinyume cha katiba ya nchi hiyo.
MTANZANIA
Mkazi wa kijiji cha Ndelete, Kiteto Saria Kidali amefariki dunia baada ya kunyongwa na shuka alilokua amejifunika wakati anaendesha pikipiki.
Tukio hilo la aina yake lilitokea jana asubuhi wakati Kidali alipokuwa akitok,ea shambani kwake ambapo shuka ya mwendesha pikipiki huyo ilinasa kwenye tairi ya nyuma na kisha kumbana shingo hadi alipopoteza maisha na kudondoka chini.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara Christopher Fuime alithibitisha kutokea kwa kifo hicho.
Mashuhuda walisema walipata taarifa kutoka kwa abiria mmoja wa basi aliyekuwa akitokea Kiteto kwenda Arusha ambaye aliuona mwili wa mtu huyo ukiwa chini.
HABARILEO
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maliasili na Utalii jana ilikataa kujadili bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii huku ikiwataka Waziri na watendaji wake kuondoka ukumbi wa mikutano wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Dar es Salaam ambako walikuwa wakutane kwa majadiliano.
Sababu kubwa imetajwa ni wizara hiyo kushindwa kutekeleza maagizo yaliyotolewa na kamati hiyo, ikiwemo kukaidi amri ya Mahakama Kuu ya kutaka kuanza mara moja utekelezaji wa tozo mpya kwenye Hifadhi za Taifa.
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu, ya Maliasili na Utalii, James Lembeli alitoa uamuzi huo jana jijini Dar es Salaam wakati kamati hiyo ilipokutana na wizara hiyo chini ya Waziri wake Lazaro Nyalandu ambaye alikiri kuwapo kwa tatizo katika ripoti huku akiahidi kufanyia kazi.
“Hatuwezi kupitia bajeti hii, kwa sababu maagizo tuliyotoa awali hayajatekelezwa, sasa tuna uhakika gani kama tukipitia hii bajeti yao ya mwaka 2015/16, watakwenda kutekeleza tutakachoagiza?”  Lembeli.
Alisema kimsingi, wizara hiyo imekwenda kinyume na makubaliano yao na kwamba ni vyema wizara hiyo ikaenda kujipanga na kufanya marekebisho ya maagizo yaliyotolewa kisha kurejea kujadili bajeti hiyo.
Lembeli aliyataja maagizo yaliyotolewa na kamati hiyo kuwa ni pamoja na utaratibu wa kiingilio kwenye hifadhi, ambapo tozo iliyotakiwa ni kila mtalii anapoingia anachajiwa kiingilio na akitoka na kutaka kuingia tena ni lazima alipe.
Waziri Nyalandu alikiri kuwepo na matatizo kwenye maagizo ya ripoti hiyo na kuahidi kuyafanyia kazi hiyo jana na wataalamu wa wizara hiyo ili wahakikishe wanatatua changamoto hizo, na leo wanaweza kutoa ripoti hiyo ili kamati ijadili bajeti yao.
HABARILEO
Mtu mmoja aliyetambulika kwa jina la Annuary Ally, raia wa nchi jirani ya Kenya ametiwa mbaroni na polisi baada ya kukutwa akivunja mashine ya kutolea fedha (ATM) ya Benki ya Barclays, Tawi la Stendi Kuu ya mabasi jijini hapa.
Kwa mujibu wa Ofisa Mikopo wa benki hiyo, Regina Kitali mtuhumiwa huyo alifika katika benki hiyo saa 5:15 asubuhi jana na kuingia katika mashine ya ATM kwa lengo la kutoa fedha.
Lakini baada ya dakika chache walisikia mtikisiko usiokuwa wa kawaida katika mashine hiyo na kumlazimu mmoja wa wafanyakazi wenzake kutoka nje kwenda kuangilia ni kitu gani.
Alisema baada ya mfanyakazi huyo kuingia ndani ya chumba hicho alimkuta Ally akiwa anajaribu kung’oa mashine hiyo ili apachike mashine maalumu aliyokuwa nayo kwa lengo la kuchukua fedha zilizokuwa ndani ya ATM hiyo.
Alisema baada ya kuona hali hiyo alimuuliza Ally kuna tatizo gani na kutaka kujua kama anahitaji msaada, lakini mtuhumiwa huyo alimjibu kuwa anataka kutoa fedha na alipotakiwa kupewa msaada alijifanya mbabe kwa kutaka kumtoa nje mfanyakazi huyo wa benki.
“Kufuatia hali hiyo mwenzetu alitoka nje mara moja na kubonyeza kengele ya tahadhari kuomba msaada kutoka kampuni ya ulinzi inayolinda katika tawi hili huku wengine tukipiga simu kuomba msaada wa polisi,” .
Kwa mujibu wa Regina wakati mtuhumiwa akiendelea kung’oa mashine hiyo polisi wa kikosi cha FFU walifika eneo hilo na ndipo mtuhumiwa alipotoka nje na kuwaponyoka polisi na kuanza kukimbia kwa lengo la kutoroka.
Alisema walianza kupiga kelele za kuomba msaada ambapo raia wema walijitokeza na kuanza kumkimbiza mtuhumiwa huyo kwa kushirikana na polisi na kufanikiwa kumkamata katika eneo la benki ya NBC tawi la Meru huku akiwa na vitambulisho vingi vya aina mbalimbali pamoja na mashine hiyo maalumu.
Baada ya mtuhumiwa huyo kutiwa mbaroni alipelekwa Kituo Kikuu cha Polisi kwa mahojiano zaidi ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.
Yote haya unayapata kupitia hapa hapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment