Saturday, January 10, 2015

HHADITHI HARISHI (30)

HADITHI HII INALETWA KWENU KWA HISANI YA MKOMBOZI SANITARIUM CLINIC, MABINGWA WA TIBA ASILIA, WAPO CHUDA TANGA, 0654361333
 
KISIWA CHA HARISHI (30)
 
ILIPOISHIA TOLEO LILILOPITA
 
Rais wa Zanzibar akawasiliana na Rais mwenzake wa Comoro na kuzungumza naye.
 
“Binti yako Yasmin ninaye hapa” Rais wa Zanzibar alimwambia Rais wa Comoro.
 
“Nimepata habari zake na nimeshukuru sana kusikia kwamba mwanangu bado yuko hai. Sisi tulidhani ameshakufa” Rais wa Comoro alisema kwenye simu.
 
“Ni kweli kwamba alipotea siku ya harusi yake mwaka mmoja uliopita?”
 
“Nikweli. Lilikuwa tukio la kushangaza sana!”
 
“Ameniambia alikuwa akiishi katika kisiwa kimoja kisicho na watu na hajui alifikaje katika kisiwa hicho”
 
“Binti yangu alipata masahibu makubwa lakini nashukuru kuwa amenusurika”
 
“Huyu hapa, ongea naye”
 
Rais alimpa Yasmin mkono wa simu ili azungumze na baba yake.
 
“Asalam alaykum baba!” Yasmin alimwamkia baba yake.
 
“Wa alaykum salam warahmatulahi wabarakat. Hujambo mwanangu?”
 
SASA ENDELEA
 
“Sijambo baba. Matatizo yaliyonitokea ni kama ulivyoyasikia”
 
“Nimeyasikia na nimemtuma kaka yako Umar na maofisa wangu kuja kukuona. Nimeambiwa kuwa mmeshakutana”
 
“Tumekutana na kaka ninaye hapa”
 
“Nimefurahi kwamba uko naye kwa rais mwenzangu. Je wewe afya yako ikoje?”
 
“Afya yangu si nzuri lakini pia si mbaya sana. Nikija huko mtaniona”
 
“Ulikuwa unaishi vipi huko kisiwani ulikokuwa?”
 
“Nimeishi kwa taabu tu baba. Nikija nitawaeleza vizuri”
 
“Ningependa uzungumze na mama yako ili umtoe wasiwasi lakini hatapatikana kwa sasa kwa sababu mimi bado niko ikulu”
 
“Hakuna wasiwasi baba. Mwambie mama mimi ni mzima. Ni masahibu tu yamenikuta na ishallah nitakutana naye”
 
”Si mtakuja hii leo?”
 
“”Kama tutaruhisiwa kuondoka tutakuja leo”
 
“Sawa. Sasa mpe simu mheshimiwa rais”
 
Yasmin akampa samu rais wa Zanzibar.
 
“Umeshazungumza na mwanao?” Rais wa Zanzibara akamuuliza rais wa Comoro kimzaha.
 
“Tumezungumza kidogo. Unatarajia wataweza kuondoka leo hii kurudi Comoro”
 
“Kwa vile ndege iko tayari sioni cha kuwazuia kuondoka leo”
 
“Basi ningependa uwaruhusu kuondoka na mtupatie taarifa muda ambao wanaondoka”
 
Baada ya maraisi hao kumaliza kuzungumza, rais wa Zanzibar alizungumza na maofisa wake.
 
“Nataka mhakikishe kuwa ugeni huu unaondoka leo kurudi Comoro. Na kwa upande wa huyu binti apatiwe mahitaji yote ya kibinaadamu kwa gharama ya serikali wakati akiwa hapa nchini kwetu bila kumsahau kijana Zahrani aliyekuwa naye kule kisiwani”
 
Baada ya rais kutoa agizo hilo aliagana na sisi na kuwatakia safari njema akina Yasmin.
 
Yasmin alimuahidi rais wa Zanzibar kuwa hataisahau Zanzibar na atarudi kuitembelea tena atakapojaliwa.
 
Tulipotoka ikulu tulipelekwa katika hoteli ya Bwawani ambako tulipatiwa huduma mbalimbali kama vile chakula, nguo na mahali pa kupumzika. Hapo tulikutana na watu mbali mbali waliopata habari zetu na kututembelea. Walikuja maofisa wa serikali na pia mawaziri.
 
Kusema kweli nilipata umaarufu mkubwa kutokana na Yasmin. Kwa vile mwenzangu alikuwa binti wa rais na alikuwa akieleza mara kwa mara kuwa kama si mimi na yeye angeangamia, watu waliotutembelea walikuwa wakitupa pole pamoja na kunipongeza.
 
Maelezo yetu yalionekana kama kioja kikubwa kwa vile yalimuhusisha jini anayeitwa Harishi ambaye alimteka Yasmin nchini Comoro na kumpeleka katika kile kisiwa cha mauti.
 
Taarifa zilipowafikia waandishi nao walianza kumiminika katika hoteli ya Bwawani kutuhoji na kutupiga picha.
 
Baadhi ya waandishi hao baada ya kupata maelezo kutoka kwangu na kwa Yasmin, walimuhoji Yasmin kutaka kujua jinsi tulivyoishi katika kisiwa hicho tukiwa peke yetu.
 
Mwandishi: “Mliishije na Zaharani mkiwa watu wawili wa jinsia tofauti katika kisiwa hicho?”
 
Yasmin: “Tuliishi kama marafiki”
 
Mwandishi: “Mlitarajia kuwa mngeokoka?”
 
Yasmin: “Kusema kweli hatukutarajia ingawa tulikuwa tunaomba sana”
 
Mwandishi: “Mlikuwa mnalalaje usiku?”
 
Yasmin: “Usiku wa jana ndio tulilala pamoja lakini pia hatukulala usingizi kwa sababu tulijua kuwa tungeuawa”
 
Mwandishi: “Sasa umeshaokoka. Unadhani utaendelea kuwa karibu na Zahrani?”
 
Yasmin: “Bila shaka. Tulipokuwa kule kisiwani nilimpa ahadi Zahrani kuwa kama tutasalimika atanioa”
 
Mwandishi: “Una maana kwamba umempenda Zahrani?”
 
Yasmin akacheka kabla ya kujibu. “Nimempenda sana”
 
Mwandishi: Je sasa unadhani utatimiza ahadi uliyomuahidi?”
 
Yasmin: “Ndiyo nitaitimiza”
 
Mwandishi: “Kwa hiyo una mpango wa kuoana na Zahrani?”
 
Yasmin: “Mpango bado, ni mawazo tu ambayo naamini hayatabadilika”
 
Mwandishi: “Umetuambia kuwa kabla ya kupotelea katika kisiwa mlichokua mnaishi ulikuwa unaolewa na mwana wa mkuu wa jeshi la ulinzi la Comoro, je kijana huyo akitaka muoane tena itakuwaje wakati umeshamuahidi Zahrani kuwa mtaoana?”
 
Yasmin: “Nadhani atakuwa ameshaoa”
 
Kaka wa Yasmin Umar Sharif Abdulatif ambaye alikuwepo wakati Yasmin anahojiwa alithibitisha kuwa aliyekuwa anamuoa Yasmin kabla ya Yasmin kupotea Comoro alishaoa mke mwingine na walikuwa wanaishi Ufaransa. Visiwa vya Comoro vilikuwa koloni la Ufaransa.
 
Mwandishi: “Kwa hiyo unatarajia kwenda Comoro na Zaharani?”
 
Yasmin: “Natarajia hivyo”
 
Mwandishi: “Ndoa yenu itafanyika lini?’
 
Yasmin: “Siku yoyote wazazi wetu watakaponiidhinisha kuolewa na Zaharani”
 
Mwandishi aliyekuwa akimuhoji Yasmin alinigeukia mimi.
 
Mwandishi: “Je umeyachukuliaje maelezo ya Yasmin?”
 
Zahrani: “Yamenifurahisha sana”
 
Mwandishi: “Uko tayari kuoana na msichana ambaye baba yake ni rais wa nchi?”
 
“Zahrani: “Kama wazazi wake watakubali niko tayari”
 
Mwandishi: “Mtakuwa mnaishi wapi  mtakapooana, Zanzibar au Comoro?’
 
Zahrani : “Popote tu tutakapokubaliana”
 
Mara tu baada ya waandishi wa habari kuondoka maofisa usalama kutoka ikulu ya Zanzibar walinitambulisha kwamba umefika wakati ambapo nitaachana na Yasmin kwa vile muda wa safari yao ya kurudi Comoro ulikuwa umefika.
 
Kauli ile ilinivunja moyo hasa kwa vile nilitegemea kuondoka na Yasmin. Yasmin akawaomba maofisa hao waniache niende naye Comoro.
 
“Hatumzuii mtu yeyote kwenda mahali popote anapotaka ila Zahrani hana hati ya kusafiria” Afisa mmoja alimwambia Yasmin.
 
ITAENDELEA KESHO, USIKOSE UHONDO HUU HAPO KESHO SAFARI YA ZAHRAN ITAKUWEPO AU KUTATOKEA MIZENGWE?

No comments:

Post a Comment