Thursday, March 30, 2017

HADITHI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 1

SIMULIZI
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU, SEHEMU YA (1)
 
Jina langu ni Kassim Fumbwe. Nina umri wa miaka ishirini na minane. Mkazi wa jiji la Dar es Salaam.
 
Wazazi wangu walifariki dunia wakati nikiwa mdogo. Nakumbuka tulikuwa tunasafiri kutoka Dodoma kuja Dar, basi tulilokuwamo likagongana na lori uso kwa uso.
 
Baba yangu na mama yangu pamoja na abiria wengine kadhaa walifariki hapo hapo. Mimi nikanusurika.
 
Nakumbuka nilipata jeraha dogo tu kwenye mkono wangu wa kushoto baada ya kukatwa na vioo vya dirisha vilivyokuwa vimevunjika.
 
Babu yangu mzaa baba, Mzee Fumbwe Limbunga alipopata habari ya ajali ile alitoka Dar kwa gari lake akaja Morogoro. Majeruhi wa ajali ile tulikuwa tumelazwa katika hospitali ya Morogoro.
 
Mimi sikuwa nimeumia sana lakini kwa vile wazazi wangu walikuwa wamefariki ilibidi nibaki hapo hospitali ili niweze kutambuliwa na kuchukuliwa na ndugu zangu.
 
Babu alipokuja akanichukua. Aliichukua pia miili ya marehemu baba yangu na mama yangu.
 
Siku ya pili yake habari za ile ajali zilichapwa kwenye magazeti. Kila gazeti lilikuwa limechapa picha yangu ikielezea jinsi nilivyonusurika kimiujiza.
 
Baada ya msiba huo, nikawa ninaishi na babu. Babu yangu alikuwa tajiri lakini alikuwa hana mke. Aliachana na mke wake tangu alipokuwa kijana na hakutaka kuoa tena.
 
Kwa hiyo alinitafutia mtumishi wa kunihudumia kwa kila kitu ikiwa ni pamoja na kunipeleka shule. Nilipoanza masomo ya sekondari babu akanihamisha katika nyumba yake nyingine. Zote zilikuwa Tegeta lakini zilikuwa mitaa tofauti.
 
Ile nyumba aliyonihamishia upande mmoja ilikuwa na mpangaji, upande mwingine ndio niliokaa mimi.
 
Kila jumatatu babu alikuwa akinipa pesa za kutumia kwa wiki nzima. Baadhi ya siku nilikuwa ninapika mwenyewe nyumbani na siku nyingine nilikuwa ninakula kwenye mikahawa..
 
Baada ya kumaliza masomo yangu nilipata kazi Morogoro. Lakini babu alinishauri niache kazi nifanye biashara. Aliponipa mtaji nikaacha kazi. Nilifungua maduka matatu ya vifaa vya ujenzi pale Morogoro.
 
Yalikuwa maduka makubwa. Niliajiri karibu wafanyakazi kumi na watano. Kila duka lilikuwa na wafanyakazi watano. Biashara ilianza vizuri. Baada ya miezi sita tu nikaja Dar kununua gari la kutembelea.
 
Sasa nikawa nafikiria kutafuta mke nioe. Sikumaliza hata mwaka mmoja ile kasi ya biashara ikaanza kupungua. Maduka yangu yaliyokuwa yamejaa vitu yakaanza kuwa matupu. Haukupita muda mrefu nikaanza kupunguza wafanya kazi. Mwisho kila duka likabaki na mfanyakai mmoja.
 
Nilifikia mahali nikahisi kuwa pengine sikuwa na nyota ya kujiajiri. Nikajuta kuacha kazi niliyokuwa nayo mwanzo. Ikabidi yale maduka mawili niyafunge nikabaki na duka moja ambalo nililisimamia mwenyewe. Duka hilo nalo likafilisika nikalifunga. Nikawa sina kazi.
 
Nilifikiria kwenda kumueleza babu ili anipe mtaji mwingine lakini nilishindwa kwani nilijua asingekubali tena kunipa pesa zake. Nikauza lile gari. Siku ile nauza gari babu akanipigia simu na kunijulisha kuwa alikuwa anaumwa na alikuwa amelazwa katika hospitali ya Aga Khan.
 
Nikapanda basi kuja Dar. Nilipofika Dar nilikwenda moja kwa moja katika hospitali katika hospitali ya Aga Khan..
 
Vile nafika tu na babu yangu anakata roho. Hata sikuwahi kuzungumza naye lolote.
 
Kifo chake babu hakikunishitua sana kwa sababu alikuwa na mali na mimi ndiye ambaye ningemrithi.
 
Dereva wake nilimkuta hapo hapo hospitali, alinieleza kuwa Mzee Fumbwe alianza kuumwa siku tatu zilizopita lakini usiku uliopita ndio alizidiwa. Presha ilikuwa juu na sukari ilipanda. Hali ikawa mbaya.
 
Kwa kushirikiana na dereva huyo tuliuchukua mwili wa Mzee Fumbwe siku ya pili yake kwa ajili ya maziko. Baada ya maziko nikaanza mchakato wa kukagua mali za marehemu.
 
Nilichokuwa nikikifahamu awali ni kuwa babu yangu alikuwa na maduka kadhaa Dar es Salaam. Alikuwa na vituo vitatu vya mafuta na malori sita.
 
Pia alikuwa na nyumba alizokuwa amezipangisha ambazo sikujua zilikuwa ngapi.Nilikuwa nikijua nyumba mbili tu, ile aliyokuwa akiishi yeye na ile niliyokuwa nikikaa mimi kabla ya kuhamia Morogoro.
 
Mali zake nyingine alikuwa akizijua yeye mwenyewe. Niliingia chumbani mwake nikafungua makabati na kuanza kupekuwa nyaraka zake alizozihifadhi kwa lengo la kutambua mali hizo.
 
Jambo ambalo lilinishangaza, nilikuta hati ya nyumba yake aliyokuwa akiishi na hati za gari alilokuwa akilitumia. Sikukuta hati wala nyaraka nyingine zinazohusu mali zake.
 
Wakili wake nilikuwa namfahamu. Nikaenda ofisini kwake barabara ya Samora na kumjulisha kuhusu kifo cha mteja wake.
 
“Oh mzee amefariki?” akaniuliza kwa mshituko.
 
“Amefariki juzi, tumemzika jana”
 
“Alikuwa mgonjwa?”
 
“Wakati anaumwa mimi nilikuwa Morogoro. Juzi akanipigia simu yeye mwenyewe akaniambia kuwa anaumwa na amelazwa hospitali. Muda ule ule nikapanda gari kuja kumuona. Mpaka nafika Dar nikakuta ameshafariki”
 
“Oh pole sana. Aliwahi kuniambia kuwa mwanawe alifariki dunia”
 
“Mwanawe ni baba yangu. Alifariki mimi nikiwa mdogo”
 
“Kwa hiyo mrithi wake utakuwa wewe. Kwa maana hakuwahi kuandika wasia wowote ila alinieleza kuwa hakuwa na ndugu wala mtoto mwingine isipokuwa mjukuu”
 
Wakili alipoleta suala la urithi akawa amenirahisishia tatizo lililokuwa limenipeleka kwake.
 
“Hilo ndilo lililonileta kwako”
 
“Umefanya vizuri kuja kunifahamisha. Sasa unatakiwa ufungue mirathi mahakamani ili uweze kumrithi babu yako”
 
“Kabla ya kufungua mirathi kuna suala moja ambalo limenishitua sana”
 
“Suala gani?”
 
ITAENDELEA kesho hapahapa tangakumekuchablog, Usikose uhondo huu nini kitaendelea
 

No comments:

Post a Comment