Friday, March 31, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 2

SIMULIZI
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 2
 
ILIPOISHIA
 
“Kuhusu mali za marehemu. Babu yangu alikuwa tajiri lakini katika kumbukumbu zake nimekuta hati ya nyumba moja aliyokuwa anaishi pamoja na hati ya gari alilokuwa akitumia”
 
“Sasa kama hakuna hati wala nyaraka zozote utazijuaje mali zake nyingine?”
 
“Kwanza hizo nyaraka zitakuwa zimekwenda wapi?”
 
“Nenda kapekue vizuri. Inaweekana aliuza baadhi ya mali zake”
 
Kutokana na ushirikiano alionipa wakili huyo kutafiti mali alizokuwa akimiliki marehemu babu yangu, tuligundua kuwa mpaka marehemu anafariki duniani hakuwa na mali yoyote aliyoacha zaidi ya nyumba aliyokuwa akiishi pamoja na gari lake.
 
Hata baada  ya kufungua mirathi mahakamani na  kuthibitishwa kuwa mimi ndiye mrithi wa marehemu, sikukuta pesa ya maana katika akaunti yake ya benki. Akaunti yake ilikuwa na shilingi elfu kumi tu.
 
SASA ENDELEA
 
Kwa Kweli mimi na wakili wa marehemu tulishangaa sana. Kila mtu alikuwa akifahamu kuwa  Mzee Fumbwe alikuwa ni miongoni mwa matajiri wazawa wa jiji la Dar es Salaam. Jinsi alivyokufa akiwa masikini ni jambo ambalo halikueleweka.
 
Katika utafiti nilioufanya baadaye niligundua kuwa Mzee Fumbwe alikuwa ameuza baadhi ya mali zake zikiwemo nyumba na  vituo vya mafuta siku chache kabla ya kufariki dunia.
 
Lakini uchunguzi wangu ulishindwa kubaini marehemu alipeleka wapi pesa zake kwani benki hakukuwa na kitu.
 
Kwa kipindi cha karibu wiki mbili nilikuwa nikiendelea kufanya utafiti kwenye nyaraka za marehemu ili kupata uhakika kwamba kweli babu hakuwa na kitu.
 
Nikaja kugundua kitabu cha kumbukumbu cha marehemu ambacho alikuwa akiandika mambo yake. Nilipopekua karasa na kitabu hicho niliona kulikuwa na watu ambao walikuwa wakifanya biashara na babu na kwamba babu alikuwa akiwadai wafanyabiahara hao pesa nyingi.
 
Nilikuta majina ya wafanya biashara wanne. Katika watu hao ni mmoja tu aliyekuwa akiishi hapo Dar, wengine walikuwa wakiishi nchi za nje. Mwenyewe aliandika kama ifuatavyo
 
Abdul Baraka wa Mbezi Dar es Salaam. Namdai dola milioni moja.
 
(Aliandika na namba ya simu yake)
 
Isaac Chusama wa Harare Zimbambwe. Namdai dola milioni mbili na laki tano.
 
(Aliandika namba ya simu yake na mtaa aliokuwa anaishi)
 
Benjamin Muhoza wa Gaborone Botswana. Namdai dola milioni moja na laki tano.
 
(Aliandika namba ya simu yake na mtaa aliokuwa akiishi)
 
Dumessan Dube wa Cape Town Afrika Kusini. Namdai dola milioni tatu.
 
(Aliandika namba ya simu yake na mtaa aliokuwa akiishi)
 
Hapo nikajua kuwa marehemu babu alikuwa akidai fedha nyingi kwa watu waliokuwa wakiishi nje ya nchi.
 
Kitabu hicho cha kumbukumbu kiliendelea kunjulisha siri ya babu ambayo nilikuwa siifahamu. Babu alikuwa akifanya biashara ya madini. Tena madini ya Tanzanite na kwamba alikuwa akiwauzia wafanya biashara hao.
 
Kumbukumbu za nyuma za kitabu hicho zilionesha ameshawahi kuwauzia madini wafanyabiashara hao kwa thamani ya dola ya Kimarekani. Na kwamba alikuwa akilipwa kwa awamu.
 
Nikajiuliza babu alikuwa akipata wapi madini mengi kiasi cha kumpatia mamilioni hayo ya dola?
 
Swali jingine nililojiuliza ni wapi babu yangu alikokuwa anaficha fedha hizo, isingewezekana afe akiwa hana kitu.
 
Niliitafuta paspoti yake na nikaipekua. Nikagundua kuwa mara kwa  mara alikuwa akitembelea Zimbabwe, Botwana na Afrika kusini.
 
Nilipopekua zaidi kwenye mafaili yake nikaipata mikataba yake na wafanya biashara hao. Alikuwa amelipwa pesa nusu na nusu alikuwa akiwadai.  Tarehe ya kuwafuata wafanya biashara hao wammalizie deni lake ilikuwa imeshapita.
 
Nikajiambia kama nitafanikiwa kupata fedha hizo nitakuwa tajiri mkubwa hapa Dar kwani kwa pesa za Kitanzania dola hizo zilikuwa ni mabilioni ya shilingi.
 
Kwa vile marehemu aliandika namba za simu zao, nikaanza kumpigia Abdul Baraka aliyekuwa hapo Dar. Nilimpigia kwa kutumia laini ya marehemu. Simu yake haikupatikana.
 
Nikampigia Isaac Chusama wa Harare. Simu  iliita kwa sekunde chache kisha ikapokelewa.
 
Nikashangaa kusikia sauti ikinisalimia kwa Kiswahili.
 
“Habari yako Bwana Fumbwe?”
 
“Nzuri lakini mimi siye Bwana Fumbwe. Bwana Fumbwe amefariki wiki tatu zilizopita, mimi ni mjukuu wake. Naitwa Kassim Fumbwe”
 
“Heh! Mzee Fumbwe amefariki?”
 
“Amefariki. Hivi sasa ni wiki tatu zimeshapita”
 
“Oh pole sana”
 
“Asante. Sasa kumbukubu za babu zinaonesha kwamba alikuwa akikudai dola milioni mbili na laki tano. Na mkataba wa makubaliano yenu ninao hapa”
 
“Ndio ni kweli ananidai”
 
“Kwa vile tarahe ya kumlipa imeshapita, ninataka nije Harare unipatie hizo fedha. Mimi ndio mrithi wake”
 
“Sasa nitakuaminije Bwana Fumbwe?”
 
“Nitakuja na hati zote zikiwemo hati za mahakama zinazoonesha kwamba mimi ndiye mrithi wa marehemu, cheti cha kifo chake na mikataba ya makubaliano yenu”
 
Pakapita kimya cha sekunde kadhaa kabla ya sauti ya mtu wa upande wa pili kusikika tena.
 
“Unatarajia kuja lini?”
 
“Baada ya siku mbili tatu. Hivi sasa ninajiandaa kwa safari”
 
“Utakapokuja utanijulisha”
 
“Sawa”
 
Isaac akatangulia kukata simu.
 
Hapo hapo nikampigia Benjamin Muhoza. Nilishukuru naye alipopokea simu.
 
ITAENDELEA kesho usikose nini kitajiri katika Uhondo huu
 
 

No comments:

Post a Comment