Thursday, April 21, 2016

HADITHI MWANAMKE ALIENICHUNUKU SEHEMU YA 20

HADITHI na Faki  A Faki 0655 340572

MWANAMKE Alienichunuka inaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha Elimu Cha Candle Education Centre Tanga, Candle ni mabingwa wa kufaulisha wanafunzi kidato cha pili hadi cha sita na wanaojiendeleza kielimu, Candle wapo Tanga mkabala na Bank ya CRDB simu 0715 772746

ILIPISHIA

Nikamfuata yule msichana aliyekuja kuniita, nikaingia naye ndani. Nilikuta watu mbalimbali waliovalia maridadi wameketi wakinywa vinywaji na kushereheka.

Msichana huyo alinichukua hadi kwenye chumba kimoja ambacho alinionesha bafu na kuniambia.

“Unatakiwa uoge, ukimaliza unakuja hapa kwenye kabati”

Alinifungulia kabati lililokuwa mle ndani ya kile chumba na kunionesha nguo zilizokuwemo ndani.

“Utachagua suti utakayoipenda, utavaa na shati jeupe na viatu vyeupe. Halafu utagonga mlango, mimi nitaingia ili nikupeleke kwa dada”

Kwanza nilisita, nikataka kumuuliza kulikoni lakini nikaona nitekeleze vile nilivyoagizwa.

Nikaoga. Nilipomaliza nilichagua suti ya kijivu niliyoipenda. Nikaivaa pamoja na shati jeupe na viatu vyeupe.

Nilipomaliza niligonga mlango. Hapo hapo yule mtumishi akaingia.

SASA ENDELEA

“Umependeza. Sasa twende” akaniambia.

Nikaenda naye katika chumba kingine ambacho kilikuwa kimepambwa. Nilimkuta yule msichana mwajiri wangu naye amepambwa. Alikuwa amekaa kwenye kitanda huku wasichana wanne wakiwa wamesimama karibu yake kama walinzi.

Niliogopa hata kuingia mle chumbani lakini yule msichana mwajiri wangu aliponiona aliniambia.

“Ingia”

Nikaingia. Akanitazama kwa makini kisha akaniambia.

“Alfred umependeza leo!”

“Asante, hata na wewe umependeza”

“Sogea karibu yangu’

Nikamsogelea. Alikuwa ananukia uturi (manukato).

“Inama nikuambie”

Nikainama.                                                                                               

Akaniambia kwenye sikio langu “ Samahani sikuwahi kukwambia, shughuli hii ni yako wewe. Nilitaka kukushitukizia”

“Mh!. Unasema shughuili hii ni yangu mimi?” nikamuuliza baada ya kutomuelewa.

“Ndiyo, ni yako wewe. Leo tutafunga ndoa usiku huu na hutakuwa mlinzi wangu tena bali utakuwa bwana wa nyumba hii”

“Umesema utafunga ndoa na mimi usiku huu?” nilimuuliza kwa mshituko uliochanganyika na kiwewe.

“Ndiyo, ni kwa sababu nilikupenda tangu nilipokuona ukilinda pale dukani. Nikapanga uwe mume wangu”

Wakati akiniambia hivyo alikuwa anatabasamu huku akiniangalia kwa jicho la huba.

Nilishindwa kujizuia na mimi nikamwambia.

“Kama ni kweli unayoniambia nitafufurahi kama utakuwa mke wangu”

“Sasa ninamuita sheikh nimpe idhini atuozeshe”

Msichana akamtuma yule mtumishi amuite sheikh. Sheikh alipofika msichana huyo akamwambia.

“Nimekuita kukupa idhini uniozeshe na Alfred na tangu sasa atakuwa anaitwa Abubakar, jina ambalo nimemchagulia mimi”

“Nataka na idhini ya mzazi wako wa kiume” Sheikh akamwambia.

“Atakupa idhini huko huko”

“Twende bwana!” Yule sheikh akaniambia.

Nikatoka na yule sheikh nikiwa siamini yale yaliyokuwa yanatokea.

Tulikwenda sebuleni ambako watu mbalimbali walikuwa wamekaa. Katikati ya sebule palitandikwa zulia dogo na palikuwa na watu wanne waliokuwa wamekaa hapo. Wote wanne walikuwa wamevaa kanzu nyeupe na vilemba kama waarabu.

Sheikh niliyekuwa nimefuatana naye alinishika mkono na kuniambia.

“Kaa hapa”

Alinionesha pale walipokuwa wamekaa watu wanne. Nikakaa na yeye akakaa mbele yangu. Mtu aliyekuwa ameketi upande wake wa kulia alikuwa mzee aliyekuwa na ndevu nyingi nyeupe.

Nikasikia akimwambia.

“Wewe ndiye walii (baba) wa bi harusi. Nataka idhini yako ili nimuozeshe binti yako kwa Abubakar”

Ninakupa idhini” Yule mzee akamwambia kwa sauti ndogo.

Sheikh huyo akanishika mkono na kunifungisha ndoa ambayo sikuitarajia.

Baada ya kufungishwa ndoa nilipelekwa katika chumba alichokuwemo yule msichana. Nikaambiwa nimpe mkono, nikampa mkono.

“Karibu kwenye nyumba yako mume wangu” Msichana huyo akaniambia kwa furaha na kwa sauti ya unyenyekevu iliyotoka kwenye moyo wake. Hapo vigelegele na chereko vilisikika nyumba nzima.

Mke wangu huyo akaniambia nikae kwenye kitanda karibu yake. Nikakaa. Baadaye kidogo tuliletewa vyakula na vinywaji. Mke wangu akanikaribisha, tukala pamoja. Hata hivyo mimi sikula sana kutokana na kihoro kilichonipata ingawa chakula kilikuwa kitamu.

Baada ya kumaliza kula tuliachwa peke yetu. Msichana huyo akaniambia.

 “Sasa tulale mume wangu. Hapa ni kwako”

Tukalala hadi asubuhi.

 Wakati huo wa asubuhi nyumba ilikuwa kimya. Sikuona mtu yeyote humo ndani zaidi ya mke wangu na watumishi wake wawili.

Wakati tunakunywa chai nilimuuliza.

“Wale watu wa jana usiku wamekwenda wapi?”

“Walienda zao usiku ule ule. Walikuja kwa ajili ya harusi yetu”

Tuliporudi chumbani msichana huyo akaniambia.

“Mimi napenda sana kusimulia hadithi. Ngoja nikusimulie hadithi moja”

Nikamwamia “Nisimulie”

“Zamani kulikuwa na msichana mmoja mrembo ambaye alimpenda sana kijana mmoja ambaye naye alikuwa mzuri. Msichana huyo alitamani sana kijana huyo awe mume wake lakini ikawa vigumu kwa wawili hao kuoana”

“Kwanini ilikuwa vigumu, huyo kijana hakumpenda huyo msichana?” nikamuuliza.

“Lahasha mume wangu. Ilikuwa vigumu kuoana kwao kwa sababu yule kijana alikuwa binaadamu lakini yule msichana alitoka katika kizazi cha kijini”

“Enhe!. Halafu ikawaje?” nikamuuliza baada ya kuona hadithi yake inafanana na kile kisa kilichonotokea mimi.

“Yule kijana alipogundua yule msichana ni jini alianza kumkimbia lakini msichana huyo hakukata tamaa, aliendelelea kumfuatilia kijana huyo na kumrai na kumueleza jinsi alivyokuwa anampenda”

Hadithi ile ilianza kunishangaza. Nikawa makini kuisikiliza ili nijue mwisho wake.

ITAENDELEA KESHO hapahapa Tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment