Wednesday, April 27, 2016

HADITHI , SITOSAHAU NILIVYOGEUZWA PAKA SEHEMU 3

HADITHI na Faki A Faki, 0713 340572, 0655 340572

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI

SITASAHAU NILIVYOGEUZWA PAKA

ILIPOISHIA 
Tulipowapa taarifa polisi, polisi watatu wakatupakia kwenye gari na kwenda nao katika eneo la tukio.Hapo nilihojiwa maswali na nikajibu kila nilichoulizwa.Baada ya hapo polisi hao waliichukua ile maiti na ile bunduki ya majambazi pamoja na kile kiganja. Wakaniambia nirudi nyumbani lakini saa tatu nifike kituo cha polisi kuandika maelezo.

Polisi hao wakaondoka na ile maiti.Afisa wetu akaniruhusu niende nyumbani kubadili nguo kwani zilikuwa zimetota na kujaa tope.Nikarudi nyumbani.Nilimueleza mjomba kilichotokea.Akanipa moyo kwa kuniambia.

“Hayo ni matukio ya kawaida katika kazi zetu lakini umefanya kitendo cha kijasiri”

Ilipofika saa tatu nikawa kituo cha polisi.Nilikuwa nimeshaoga na kubadili nguo isipokuwa si kunywa chai kwa sababu ya wasiwasi.

Nikiwa kituo cha polisi niliingizwa katika ofisi ya afisa upelelezi ambaye alichukua maelezo yangu.Baada ya kumaliza kuchukua maelezo yangu alinipongeza kutokana na ujasiri wangu.

Tukio hilo la ujambazi lilisababisha nipande cheo kazini kwangu.Nikavalishwa v mbili begani. Pia ukawa ndiyo mwanzo kwa walinzi wa usiku wanaolinda sehemu nyeti kupewa bunduki. Kwa vile mimi nilikuwa sijapata mafunzo ya kutumia bunduki nilipewa lindo jingine la mchana kwa wiki nzima huku nikipewa mafunzo ya jinsi ya kutumia bunduki na kulenga shabaha.

SASA ENDELEA

Baada ya wiki moja nikawa tayari ninajua kutumia bunduki.Nikarudishwa kwenye lindo langu lilelile la usiku. 
Nimekieleza kisa hicho kwa sababu kilikuwa chanzo cha mimi kufahamiana na msichana mmoja anayeitwa Msekwa. Nilikutana na msichana huyo sokoni. Sote tulikuwa tunachagua nazi. Msichana huyo wa Kiruvu akanisalimia kwa kutabasamu kisha akaniambia. 

“Ninakufahamu”

“Tulikutana wapi vile….?” Nikamuuliza huku nikijaribu kuvuta kumbukumbu.

“Ninakufahamu tu”akaniambia

Nikawa sikumuelewa. Alipoona ameniacha njia panda akaniambia. 

“Wewe si ndiye uliyemkata jambazi mmoja kiganja cha mkono ukachukua bunduki yake.....?” hakumaliza sentensi yake akacheka kisha akaondoka. Nikabaki nimesimama nikimuangalia.

Kitu ambacho sikukijua ni kwamba habari zangu zilizungumzwa sana pale Handeni jinsi nilivyowasambaratisha wale majambazi.Wakati nikipita kwenye mitaa watu walikuwa akinisema na kuninyooshea kidole.Yule msichana alikisikia kisa changu na kuniona nilikuwa kijana shujaa. Kwa kweli alinipenda.

Siku nyingine nilikuja kukutana naye wakati ninaenda kazini. Akanisalimia na ndipo nilipogeuka na kumuona.Tukaulizana hali. Akanieleza anapoishi kisha tukaachana. Kutoka siku ile tukawa tunakutana mara kwa mara na kuzungumza. Bila kutegemea tukaja kuwa marafiki na mwisho akawa mchumba wangu.Nikaja kuoana naye.

Tayari nilikuwa nimepangisha chumba changu kwenye nyumba ya mzee mmoja iliyokuwa jirani na mahakama ya mwanzo.Nikaendelea na maisha nikiwa na mke wangu ambaye tulipendana sana. Miaka mitatu ikapita.

Siku moja wakati naenda kazini mchana,nilisikia sauti ya msichana akiniita nyuma yangu. “Rajabu….Rajabu….” nikageuka nyuma na kumuona Chausiku yule mchumba wangu wa kwanza ambaye tulipanga kuoana nikipata kazi lakini nilipopata kazi nikamsahau na kuoana na msichana mwingine.

“Oh! Chausiku ni wewe? Sikukujua, samahani”

“Najua hukunijua.Habari za siku?”

“Nzuri, za Songe au hukai Songe siku hizi?”

“Niko Songe nakusubiri wewe uje unioe, naona kimya tu”

Nikajidai kucheka.

“Mbona mimi nilishaoa”

“Kumbe ulishaoa?” akaniuliza kwa sauti ya fadhaa.

“Nilishaoa mwenzako”

“Sasa kwanini hukuja kuniambia kama umebadili mawazo?”

“Kwa hilo nakuomba unisamehe.Najua nilikosea”

“Basi nimeshakusamehe.Ndoa ni riziki, kama haikupangwa haiwezi kuwa. Sasa unafanya kazi wapi?”

“Ninafanya kazi ya ulinzi. Si unaniona nilivyovaa?”

“Unafanya wapi?”

Nikamuelekeza zilipokuwa ofisi zetu.

“Sasa wewe utakuja lini Songe?”

“Nikipata likizo mwaka huu nitakuja kuwatembelea”

“Sawa, basi mimi huwa ninakuja mara kwa mara kuuza
vyungu. Nikimaliza kuuza ninapanda gari ninarudi”

“Basi ukija nitembelee ofisini kwetu. Si umesha pajua?”

“Nimeshapajua”

Baada ya hapo tukaagana. Akaenda zake na mimi nikaenda kazini kwangu.

Kumbe kile kitendo cha kumwambia nitembelee ofisini kwetu kilikuwa kosa.Baada ya wiki mbili wakati nimerudi nyumbani jioni kutoka kazini,nikasikia mtu anabisha mlango wa chumba changu.Mke wangu alikuwa uani.Nilipofungua mlango nikamuona mfanyakazi mwenzangu amefuatana na Chausiku.Nikashituka.

"Karibuni" nikawaambia huku nikitoa tabasamu la uongo kuficha mshangao wangu.

"Ahsante" mfanyakazi mwenzangu ndiye aliyejibu na kuongeza  "Huyu msichana alikuja ofisini kukuulizia.Anasema anatoka Songe,alikuja kuuza bidhaa zake hapa mjini lakini amechelewa gari.Ametuambia wewe ni kaka yake"

"Ndiyo, tunatoka kijiji kimoja" nikasema na kumtazama Chausiku. 

"Kumbe leo ulikuja na umechelewa gari?" nikamuuliza.

"Gari limewahi kuondoka na sina pa kulala ndiyo nikaja kukuulizia kazini kwako ili unipe msaada wa mahali pa kulala hadi kesho asubuhi nirudi kijijini" Chausiku akasema kwa ufasaha na kujiamini kama vile alijua mimi nina chumba cha wageni wakati chumba changu kilikuwa kimoja tu.

Kadhalika sikuufurahia ugeni wake nyumbani kwangu kwa sababu ya vile nilivyomuacha kwenye mataa na kuoa mke mwingine.Sikutaka kabisa wakutane na mke wangu lakini ndiyo alikuwa ameshaletwa nyumbani. Sikuwa na la kufanya zaidi ya kumkaribisha.

"Basi mimi ninarudi kazini" mfanyakazi mwenzangu aliniambia.

Nikaagana naye akaenda zake.

Mke wangu aliposikia sauti za watu akaja haraka kwenye mlango, akamuangalia yule msichana.

Nikamtambulisha kuwa ni binti wa shangazi yangu anayeishi Songe kisha nikamueleza tatizo lililomleta kwangu jioni ile.

Mke wangu Msekwa kwa kudhani ni wifi yake alimkaribisha chumbani.Wakazungumza sna kwa furaha na vicheko.Jua likawa limekuchwa. Nikamfuata mama mwenye nyumba na kumuomba amruhusu mgeni wangu alale chumbani kwa binti yake kwa siku moja.

Mama mwenye nyumba akanikubalia.Jioni ile tulipika wali kwa sababu ya mgeni.Wenyewe tulikuwa tupike ugali.Baada ya kula tulikaa nje tukazungumza mpaka saa nne usiku tulipoingia ndani kulala.

Asubuhi kulipokucha Chausiku aliondoka mapema sana ili kuwahi gari la saa moja.Nilishukuru kwamba katika kukaa kwake pale nyumbani mke wangu hakumgundua kwamba alikuwa mchumba wangu wa kwanza.

Baada ya wiki mbili ulitokea ugomvi kati yangu na mke wangu. Kisa cha ugomvi huo ni mke wangu kuchelewa kupika. Siku hiyo nilirudi kutoka kazini saa kumi na moja jioni. Kwa kawaida ninakuwa sili mchana siku nikiwa kazini. Ni mpaka jioni ninaporudi mke wangu anakuwa ameniwekea chakula cha mchana.

Siku hiyo sikukuta chakula na njaa ilikuwa inaniuma. Nilimkuta mke wangu amelala. Nikamuuliza   "Vipi?"

Akanijibu kuwa alikuwa amechoka baada ya kurudi kutoka katika harusi ya jirani yetu.

Kawaida yetu ni kuwa ninaporudi kutoka kazini huniuliza kuwa aniwekee chakula au maji ya kuoga. Lakini siku ile hakuniuliza chochote. Ikabidi nimwaambie mwenyewe. 

"Nimwekee chakula"

"Sikupika" akanijibu haraka.

"Hukupika kwa nini?"

"Si nilikwenda harusini?"

"Ukenda harusini ndiyo hupiki?"

"Ah! nimechoka bwana, nimerudi sasa hivi!"

"Sasa kama wewe umekula harusini mimi nikale wapi?"

"Lakini si umeniruhusu mwenyewe niende?"

"Hilo sio swali langu. Nimekuuliza kama hukupika mimi nikale wapi?"

"Lakini uliniruhusu mwenyewe!"

"Kwamba usipike?"

"Niende harusini"
"Lakini sikukuambia nenda harusini lakini usipike. Kama umesharudi huko harusini kwanini hukupika?"

Nilipomuuliza hivyo alikunja uso akaguna. Jambo hilo liliniudhi nikakasirika.

Je nini kilifuatia baada ya hapo? Hebu endelea kufuatilia hadithi hii katika blog yako maarufu ya Tangakumekuchablog.

No comments:

Post a Comment