Friday, April 29, 2016

HADITHI, SITASAHAU NILIVYOGEUZWA PAKA SEHEMU YA 5

HADITHI

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0655 340572, 0713 340572

SITASAHAU NILIVYOGEUZWA PAKA 5

ILIPOISHIA JANA 

Wanawake waliokuwa uani pamoja na mama mwenye nyumba wakatushangaa.

"Jamani kuna nini, mbona mnatushitua?" mama mwenye nyumba aliuliza kwa hofu.

"Msekwa ameuliwa,amepigwa kisu kifuani na shemeji.Nendeni chumbani mwao mumuone!" Mkiwa akasema huku akilia

"Sikumpiga kisu shemeji, hebu nielewe.Mimi nilikuja na kumkuta ameshapigwa kisu. Mbona unataka kunitia katika hatia?" nikamwaambia kwa ukali kidogo.

"Ni wewe shemeji, ndiye uliyekuwa naye huko chumbani.Ni chuki za jana hizo"

Wanawake wote waliokuwa uwani wakaenda ukumbini, wakaingia chumbani mwangu.Mimi nilikuwa nikiendelea kueleza kile nilichokishuhudia.Kila aliyeingia mle chumbani alitoka mbio huku akipiga kelele.

Wanawake wengine walikimbilia uani wengine walikimbilia nje.Mama mwenye nyumba alinifuata na kunishika mkono na kuniuliza "Kwanini umefanya kitendo kama kile mwanangu?"

"Sikumpiga kisu mimi mama"

"Ni wewe, shemeji yako amekuona.Unakataa nini" mama mwenye nyumba akanikata kauli.

SASA ENDELE

"Siye mimi.....mbona hamnielewi jamani.....?" kila nilipotaka kueleza nilizingirwa na vilio vya wanawake hao.Wengine wakinilaani na wengine wakiniapiza.

"Baba unaweza kufanya kitendo kama kile kwa mke wako?" mwanamke mmoja aliniuliza akiwa amenitolea macho.

"Ha! ni ukatili wa hali ya juu!. Unamchoma kisu mwenzako kwa jambo la kipuuzi tu?" mwanamke mwingine akajisemea peke yake.

Huo ulikuwa ni ushahidi wa kutosha kunitia kwenye hatia hata kama sikuwa mimi niliyeua.Nikaona usalama wangu ulikuwa hatarini.

Nilihofia pia kuwa kelele za wanawake hao zingeweza kuwavuta majirani na nyumba ikajaa watu. Penye wengi huzaa mengi, ningeweza kushikwa na watu wenye hasira nikapigwa na kuuawa wakati sikutenda kosa lolote na sijamjua aliyetenda kosa hilo.

Nikaona niondoke. Kuondoka kwenyewe pia nilitumia udanganyifu wa kujifanya ninakwenda polisi kutoa taarifa. Hapo ndipo nilipofanikiwa kutoka salama. Lakini sikwenda polisi. Nilikwenda katika kituo cha mabasi cha Handeni,nikapanda basi la kijijini kwetu Songe

Lakini ni kwanini sikwenda polisi?.Sikwenda polisi kwa sababu nilijua kuwa wangenikamata mimi na huo ndio ungekuwa mwisho wa maisha yangu.

Ningefunguliwa kesi ya kuua kwa kukusudia.Wale wanawake wote wangeitwa wakatoa ushahidi wakati mimi sikuwa na shahidi hata mmoja. Uongo wa wengi si ukweli wa mtu mmoja. Ningenyongwa tu.

Baada ya kujipakia kwenye basi hilo haukupita muda mrefu basi likaondoka. Nikaenda kijijini kwetu Songe. Mji wa Handeni nikaukimbia. Sikujua tena kilichotokea nyuma yangu.

Nilipofika Songe nilijificha kwenye mashamba hadi usiku, ndipo nikatoka na kutembea kwa miguu hadi kijiji kingine ambako Chausiku alikuwa anaishi kwenye chumba chake mwenyewe.

Mpaka nilipokuja kuigundua nyumba aliyokuwa anaishi ilipita kazi.Lakini kwa kifupi nilipoipata nyumba yake ilikuwa saa tatu usiku.

Ilikuwa ni nyumba kubwa iliyojengwa kwa tofali.Yeye alikuwa amepangisha chumba.

Chausiku aliponiona alifurahi sana akanikaribisha chumbani kwake kwa bashasha.Tukazungumza.Nikamdanganya kuwa nimeamua kuacha kazi na kurudi kijijini kwetu kujishughulisha na kilimo.

Nilidhani angeniuliza kwanini nimeacha kazi. Lakini swali lake lilikuwa.  "Na mke wako umemuachia nani?"

"Nimeachana naye ili nije nikuoe wewe mchumba wangu wa zamani"

Chausiku akafurahi sana.  "Kumbe bado ulikuwa unanipenda?"

"Nakupenda sana.Yule msichana nilikuwa nimemuoa kwa bahati mbaya tu lakini chaguo langu lilikuwa ni wewe"

"Sasa ngoja basi nikuwekee maji ukaoge halafu nikupikie chakula"

"Nitakushukuru sana"

Huo ndio uzuri niliouona kwa wanawake wa vijijini.Hawakuulizi umekuja na nini au una kiasi gani cha pesa.Wao wanafurahia mume tu.

Baada ya muda kidogo Chausiku alirudi chumbani na kuniambia "Maji tayari"

Chausiku akanipa khanga yake ili nivue nguo.Kule kijijini kwetu taulo hazikuwa zikitumika sana.Pengine ni kwasababu ya ukata. Chausiku akanisindikiza hadi uani ambako alinitambulisha kwa wapangaji wenzake kuwa ni mchumba wake ninayetokea Handeni. Akatoa maelezo marefu ya tangu tulivyoanzana tukiwa shule.Wenyeji wangu wakanifurahia na kunikaribisha.

Niliporudi kutoka kuoga sikukaa sana Chausiku akaniletea ugali kwa perege. Nikala hadi nikashiba.

Huo ukawa mwanzo wa maisha yangu katika kijiji hicho. Siku za kwanza kwanza nilikuwa najifichaficha.Baada ya juma moja Chausiku alipata habari kuwa kuna polisi waliokwenda Songe kuniulizia lakini wakaambiwa niliondoka kijijini hapo miaka mitatu iliyopita na sijaonekana tena.

Mke wangu akaja kuniambia. Mimi nikamwaambia kwamba polisi walikuja kuniulizia kutokana na kesi ya ujambazi.Nikamhadithia kile kisa cha jambazi niliyemkata mkono na mwingine kumpiga risasi. Chausiku akaamini kuwa hao polisi walikuwa wananitafuta kwa sababu hiyo.

Ilipofika wiki ya pili nikaandaa mipango ya harusi. Harusi za vijijini hazina gharama kubwa,hivyo mipango yangu ilikwenda vizuri japokuwa sikuwa na fedha za kutosha.Wiki ya tatu yake nikaoana na Chausiku na kuendelea kuishi katika nyumba ileile.

Nilikuwa nikijishughulisha na kilimo na mke wangu alikuwa akiendelea na kazi yake ya ufinyanzi wa vyungu ambavyo alikuwa akivipeleka Handeni kuviuza kila wiki. Hivyo maisha yalikuwa yanatuendea vizuri. Chakula tulikuwa nacho cha kutosha na pesa za kutumia hazikuwa zikitupiga chenga.

Baada ya kupita mwaka mmoja angalau nikajiona niko huru. Ule wasiwasi wa kukamatwa ukaanza kunitoka. Nikahisi lile tukio la kuawa kwa mke wangu wa kwanza limeanza kusahauliwa na polisi.

Katika maisha yetu na Chausiku kulijitokeza kitu ambacho kilinitia wasiwasi. Mara nyingi ninapoamka usingizini wakati wa usiku Chausiku alikuwa hayupo kitandani. Lakini ninapolala tena baadaye ninakuja kuta nimelala naye.

Niliwahi kumuuliza anakwenda wapi.Siku za kwanza alinijibu kuwa labda ninaota. Lakini siku zingine aliniambia anakwenda maliwatoni kujisaidia.

Kuna siku moja ambayo nimeamka na kukuta nimelala peke yangu. Nikatoka hadi uani kumfuatilia lakini sikumuona,nikarudi chumbani.

Asubuhi nilipomuuliza, Chausiku alikasirika akaja juu na kuniambia kuwa alikuwa ametoka barazani kupunga upepo kwa sababu ya joto lililokuwemo ndani.

Nikamwaambia haikuwa jambo zuri kutoka nje peke yake wakati wa usiku kwani anaweza kushambuliwa na fisi wanaozunguka ovyo usiku kucha.

Chausiku akanyamaza kimya.

Siku nyingine aliniaga kuwa anakwenda kwa bibi yake mzaa mama yake aliyekuwa akikaa kijiji cha jirani. Akaniambia atalala hukohuko na atarudi kesho yake.

Lakini akanionya kuwa nisifungue chumba chake ambacho alikuwa akikitumia kama stoo yake. Baada ya kile chumba tulichokuwa tunalala alikuwa na chumba kingine ambacho sikupata kukiingia hata siku moja. Alikuwa akiingia yeye mwenyewe tu kuweka vitu vyake pamoja na vyungu alivyokuwa anatengeza.

Siku ile alipoondoka kwenda kumsalimia bibi yake, usiku wake nikaamua kuingia katika kile chumba alichonikataza nisiingie.

Nilivizia watu wote walikuwa wameshalala. Nikafungua mlango na kuingia huku nimeshika taa ya kandili (Chemli) ili niweze kuona.

Hayo niliyoyakuta humo chumbani sikuyatarajia kabisa. Yalikuwa ni maajabu yaliyonishitua sana!

Je kijana huyo ameona nini? Hakikisha hupitwi na uhondo. Usikose kufungua blog hii hapo kesho ili ujue kilichotokea.

No comments:

Post a Comment