Saturday, April 30, 2016

HADITHI, SITASAHAU NILIVYOGEUZWA PAKA SEHEMU 6

HADITHI, SITASAHAU NILIVYOGEUZWA PAKA

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI, 0655 340572

SITASAHAU NILIVYOGEUZWA PAKA

Asubuhi nilipomuuliza, Chausiku alikasirika akaja juu na kuniambia kuwa alikuwa ametoka barazani kupunga upepo kwa sababu ya joto lililokuwemo ndani.

Nikamwaambia haikuwa jambo zuri kutoka nje peke yake wakati wa usiku kwani anaweza kushambuliwa na fisi wanaozunguka ovyo usiku kucha.

Chausiku akanyamaza kimya.

Siku nyingine aliniaga kuwa anakwenda kwa bibi yake mzaa mama yake aliyekuwa akikaa kijiji cha jirani. Akaniambia atalala hukohuko na atarudi kesho yake.

Lakini akanionya kuwa nisifungue chumba chake ambacho alikuwa akikitumia kama stoo yake. Baada ya kile chumba tulichokuwa tunalala alikuwa na chumba kingine ambacho sikupata kukiingia hata siku moja. Alikuwa akiingia yeye mwenyewe tu kuweka vitu vyake pamoja na vyungu alivyokuwa anatengeza.

Siku ile alipoondoka kwenda kumsalimia bibi yake, usiku wake nikaamua kuingia katika kile chumba alichonikataza nisiingie.

Nilivizia watu wote walikuwa wameshalala. Nikafungua mlango na kuingia huku nimeshika taa ya kandili (Chemli) ili niweze kuona.

Hayo niliyoyakuta humo chumbani sikuyatarajia kabisa. Yalikuwa ni maajabu yaliyonishitua sana!

SASA ENDELEA

Nilipoingia mle chumbani nilishituka nilipomuona Chausiku ameketi kwenye kigoda kilichokuwa katikati ya chumba hicho, ameelekea upande ule uliokuwa na mlango.

Alikuwa ametulia kimya na amefumba macho kama aliyekuwa amelala.

"We Chausiku!" nilimuita kwa kugutuka.

"Kelele!" akaniambia kwa sauti tulivu bila kufumbua macho.   "Si nilikuonya usiingie katika chumba hiki?" akaniuliza.

"Nilikuwa natafuta .....nilikuwa natafuta.....!"

"Toka!" akaniambia kwa ukali akiwa bado amefumba macho yake vilevile.

Nikatoka huku nikitetemeka kwa hofu. Nguvu ziliniishia kabisa mwilini.

Huyu mwanamke aliniaga anakwenda kwa bibi yake tangu asubuhi. Kumbe amejifungia humu chumbani kwenye giza na mbu, anafanya nini? nikawa najiuliza.

Nilirudi chumbani mwetu nikaweka ile taa na kuketi kwenye kiti kutafakari. Baadaye nilimuona akiingia mle chumbani huku akicheka.

"Nimekugundua sasa, kwanza wewe si muaminifu na pili muoga" akaniambia huku akiketi kitandani.

"Kwanini unaniambia hivyo?" nikamuuliza.

"Nilikuonya usiingie katika kile chumba. Ulipoona nimeondoka ukaingia. Je ni uaminifu huo?"

Nikanyamaza kimya. Sikuwa na cha kumjibu.Ni kweli kuwa alinionya lakini nilivyoona ameondoka nikaingia. kumbe na mwenyewe alikuwamo humo ndani.

"Halafu wewe ni muoga sana" akaendelea kuniambia.

"Kumbe ulikuwa unafanya nini mle chumbani?" nikamuuliza

"Nilitaka kukupima wewe nione uaminifu wako kwangu na nione ujasiri wako. Sasa nimeshakugundua"

Nikabaki kuguna tu.

Tukalala. Asubuhi kulipokucha nikaenda zangu shambani kwangu. Ilipofika saa saba mchana mke wangu akaja shamba kuniletea chakula.Ilikuwa ni kawaida yetu siku nikienda shamba mke wangu kuniletea chakula.

Wakati ninakula akaniambia kuwa mtoto wa jirani yetu mzee Juma amagongwa na nyoka na hali yake si nzuri. Habari ile ikanishitua kwa sababu huyo mtoto alizoea kucheza barazani mwa nyumba yetu na alikuwa mtoto mcheshi aliyependwa na kila mtu.

"Amegongwa na nyoka?" nikamuuliza mke wangu huku nikishangaa.

"Amegongwa kama saa tano hivi"

"Wapi?"

"Huko nyumbani kwao.Alikuwa akicheza na wenzake kwenye mti,kumbe palikuwa na nyoka akamgonga"

"Nyoka wa rangi gani?"

"Wenzake wanasema ni nyoka wa rangi ya kijani"

"Nyoka wa kijani wana sumu kali sana. Sasa wamempa dawa gani?"

"Babu yake anajua dawa za nyoka, amemchanja akampaka dawa"

"Lakini umesema hali yake si nzuri?"

"Walichelewa kumpa dawa. Babu yake alikuwa shambani, mpaka anakwenda kuitwa, mtoto alikuwa ameshalegea na mguu umevimba"

"Wangempeleka hospitali Songe"

"Mh! watu wa hapa wanaamini zaidi dawa zao za kiasili kuliko za hospitali"

''Lakini kama mtoto amelegea kiasi hicho wangempeleka hospitali tu"

"Nitakwenda kuwashauri wampeleke hospitali"

"Nikirudi nitakwenda kumuangalia"

Nilipomaliza kula mke wangu alichukua vyombo akarudi nyumbani.

Nilirudi kutoka shamba majira ya saa kumi jioni. Sikuona dalili nzuri nyumbani kwa mzee Juma.Nilikuta watu wamejazana barazani na huko ndani kulikuwa na sauti za watu wanaolia. Hapo hapo nikajua nini kimetokea. Niliingia nyumbani mwetu nikaweka jembe. Mama mmoja mkazi wa mle ndani akaniambia  "Nyumba ya pili kumefiwa"

"Nani aliyekufa?" nikamuuliza lakini tayari nilikwisha jua

"Ni Hamisi, mtoto wa mzee Juma.Amegongwa na nyoka asubuhi, wamemchelewesha kumpeleka hospitali hivi jioni amekufa"

"Na mke wangu yuko hukohuko?"

"Tulikuwa naye hukohuko kwenye msiba. Mimi nimerudi mara moja tu kumpikia mume wangu.Je unataka nikuitie?"

"Hapana.Mimi pia nitakwenda hukohuko.Mke wangu alikuja shambani kuniambia kuwa Hamisi amegongwa na nyoka. Nikamwaambia kwanini baba yake hakumpeleka hospitali. Kumbe wamemuacha mpaka amekufa"

"Babu yake alikuja kumpa dawa lakini haikusaidia"

"Nyoka wa kijani wana sumu kali sana"

Baada ya kuzungumza na yule mama nikatoka kwenda kumpa pole mzee Juma na kumuuliza juu ya mipango ya maziko.Akaniambia wamepanga kumzika mtoto wao kesho yake asubuhi.

Asubuhi mimi na mke wangu tukaenda kwa jirani yetu kuhudhulia maziko.Muda ulipowadia jeneza lilibebwa kuelekea eneo la makaburi ambalo halikuwa mbali sana.Tukamzika yule mtoto kisha tukarudi

Siku ile tulishinda nyumbani kwa mzee Juma kumfariji mwenzetu.Mke wangu alikuwa miongoni mwa akina mama waliokuwa wakishughulika kupikia wageni kama ilivyo kawaida ya mahali panapotokea msiba. Ilipofika usiku mimi na mke wangu tukarudi nyumbani kulala.

Nilikuja kushituka usiku wa manane. Nikamuona mke wangu anashuka kitandani. Nikanyamaza kimya na kujifanya kama nimelala.Akajifunga upande wa kaniki kisha akaniita mara tatu.

lakini sikumjibu kitu. Akatoka mle chumbani.Alipotoka na mimi nikashuka kitandani, nikanyata hadi mlangoni kumchungulia. Nikamuona ameingia katika kile chumba cha pili. Baadaye kidogo akatoka, mimi nikarudi kitandani. Akaingia tena mle chumbani na kunichungulia.Mkononi alikuwa ameshika kitu ambacho sikuweza kukiona vizuri kwa sababu nilikuwa namwaangalia kwa kumuibaiba.

Nilitulia kimya pale kitandani, nikasikia akifungua mlango wa nje.Nikainuka na kwenda kumchungulia.Nikamuona anatoka na kuufunga mlango.Nilisubiri kwa dakika chache kisha nikaenda kwenye mlango huo. Nikaufungua taratibu na kumchungulia.Nikamuona anapotea kwenye kiza upande wa kushoto mwa nyumba yetu ambako palikuwa na pori.

Yule msichana anakwenda wapi usiku huu? nikajiuliza kwa mshangao bila kupata jibu. Nikatoka nje na kuufunga mlango.Niliamua kumfuatilia ili nijue anakwenda wapi.

Kulikuwa na baridi l;akini sikuisikia kwa sababu ya kutaharuki. Nilipoingia kwenye lile pori nilimuona Chausiku ametokea upande wa pili wa pori hilo na kuendelea kwenda.Nami niliendelea kumfuatilia taratibu huku nikijifichaficha kwenye miti ili asinione.

Nikaendelea kumfuatilia hadi kwenye eneo la makaburi mahali ambako kwa usiku ule palikuwa panatisha kweli kweli na isingekuwa rahisi kwa mtu yeyote mwenye akili zake timamu kufika mahali hapo wakati ule usiku akiwa peke yake tena bila taa na akionekana hana wasiwasi.

Mh! Makubwa! Haya huyo msichana anakwenda wapi usiku huo? Hebu endelea kufuatilia  hadithi hii ya kusisimua  katika blogy hii hapo kesho.

No comments:

Post a Comment