Saturday, April 30, 2016

WAPENZI WA SOKA TANGA WAINGIWA NA KIWEWE



Tangakumekuchablog
Tanga, WAPENZI na washabiki wa soka  Tanga wameingiwa na kiwewe cha kuzipoteza timu zao tatu kushiriki ligi kuu Tanzania Bara msimu ujao na kuwataka viongozi wa Mkoa kuungana kutoa msukumo kwa makocha na viongozi ili kushinda michezo iliyoko mbele yao.
Wakizungumza na Mwanaspoti kwa nyakati tofauti leo, Kamishna wa Chama Cha NCCR Magezi Tanga, Ramadhani Manyeko, alisema tatizo liko kwa viongozi kwani wachezaji wamekuwa wakionyesha kandanda safi uwanjani.
Alisema wachezaji wamekuwa wakionyesha mchezo mzuri uwanjani na wamekuwa wakijituma lakini wamekuwa wakikatishwa tama baada ya kukosa ushirikiano hivyo kutaka kipindi hiki cha lala salama kushikamana na kuwa kitu kimoja.
“Ni jambo ambalo huwezi kuamini timu tatu kutoka mkoa mmoja zinachungulia tanuri, hapa kwetu kuna namna na sisi wapenzi wa soka tunawashushia viongozi wetu” alisema Manyeko na kuongeza
“Timu kama Coastal imeifunga Simba  na kutoa upinzani mkubwa kwa Yanga, hapa utasema timu ni mbovu, hebu tuutafute muarubaini kabla kipenga cha kuisha msimu wa ligi” alisema
Alisema endapo timu zote tatu zitateremka daraja soka la Tanga litakufa na ni ndoto kurudi ligi kuu kwa miaka ya karibuni na wachezaji wengi wataibukia timu za nje ya Mkoa huo.
Kwa upande wake shabiki wa mpira mkazi wa Mikanjuni Tanga, Habib Swaleh, aliwataka viongozi wa Serikali na Mkoa kuzipa ushirikiano timu zote tatu, Coastal Union, African Sports na Mgambo ili ziweze kunusurika na janga la kushuka daraja.
Alisema itakuwa aibu uwanja wa Mkwakwani kuchukuliwa na timu za nje na kuufanya uwanja wa nyumbani ilhali zipo timu tatu ambazo zimekuwa zikionyesha upinzani kwa timu shiriki za ligi kuu Tanzania Bara.
Alisema ili kuweza kuzinusuru timu na soka la Tanga ni wajibu wa viongozi wa mpira na viongozi wa Serikali kukaa chini na kutafakari namna ya kuzinusuru timu hizo kutumbukia janga la kushuka daraja.
“Tuko na uwanja mzuri ambao ni wa pili nchini kwa uzuri na ubora lakini tunashuhudia tukiuwacha uote nyasi ili kupata majani ya kulisha ng’ombe na mbuzi” alisema Swaleh
Alisema kama viongozi wako na dhamira ya kweli timu za Tanga timu mbili zinaweza kubaki ligi kuu msimu ujao hivyo wakazi wa Tanga macho yao yako kwa viongozi wa soka na Serikali.
                                                 Mwisho

No comments:

Post a Comment