Wednesday, January 18, 2017

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 17

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 17
 
ILIPOISHIA
 
Mhudumu aliondoka. Simon akamtazama Kweka.
 
“Ndiyo Dokta, umepata habari gani?”
 
Dokta Kweka akatabasamu.
 
“Umefanya kazi nzuri, nimeshapata taarifa zote. Asante sana”
 
Simon akacheka.
 
“Jana nilipokwambia ulidhani ni mzaha”
 
“Nilijua haikuwa mzaha, nitakupatia pesa yako iliyobaki”
 
Supu ilipoletwa Simon alianza kula huku akiendelea kuzungumza na Kweka. Walipomaliza kula Dokta Kweka alifungua mkoba wake akampa Simon shilingi milioni mbili na nusu.
 
Simon alizitia mifukoni kisha akamuaga Kweka na kunyanyuka.
 
“Subiri” Kweka alimwambia.
 
Simon akainamia meza ili kumsikiliza Kweka.
 
“Ndiyo”
 
SASA ENDELEA
 
“Usifurahie pesa tu, kumbuka kwamba Inspekta Amour wa jeshi la polisi ameshingia kazini kumtafuta muuaji. Kwa hiyo jihadhari”
 
“Ninafahamu”
 
“Kama una fahamu, sawa”
 
Simon akaondoka.
 
Kwa kawaida kila ifikapo saa mbili usiku Simon alikuwa na tabia ya kufika katika klabu ya usiku ya ABC iliyopo Kimara. Pale ABC alikuwa na msichana wake ambaye alikwishaachana naye baada ya kuoana na Vicky.
 
Siku chache baada ya mauaji ya Maria, Inspekta Amour aliipata namba ya msichana huyo kutoka kampuni ya simu na kumpigia. Baada ya kumpigia alimfuatilia hapo klabu na kukutana naye uso kwa uso.
 
Simon alipofika klabuni hapo saa mbili usiku, msichana huyo alikwenda kumuita lakini Simon alipomuona aliyemuita aliamua kukimbia. Alikuwa akimjua Inspekta Amour na alijua kuwa alikwenda pale kumkamata yeye kufuatia mauaji ya Maria.
 
Baada ya Simon kukimbia Amour alimuandama. Ndipo yalipotokea yaliyotokea ambapo Simon alikamatwa na hatimaye kufikishwa mahakamani kabla ya kuachiwa huru na mahakama baada ya James kutoa ushahidi ulioonesha kuwa Simon hakumuua Maria na kwamba alikuwa hamtambui.
 
Tangu Simon alipokamatwa hadi kuachiwa huru ilikuwa imeshapita miezi sita.
 
                                ***************
 
James alipoondoka na Simon nje ya mahakama, alikwenda naye nyumbani kwake Msasani. Alishuka kwenye gari akamkaribisha ndani.
 
“Karibuni ndani Mr Simon” alimwambia.
 
Waliingia ndani na kutokea kwenye sebule pana iliyopangwa vizuri.
 
“Karibu ukae tafadhali”
 
Simon alikaa kwenye kochi mojawapo.
 
“Umepata kifungua kinywa?”
 
“Uji tu”
 
“Subiri nikutayarishie kikombe cha chai ya maziwa”
 
James alimwambia na kwenda jikoni alichukua chupa ya chai, bisikuti na vikombe viwili. Alirudi sebuleni akamimina chai kwenye vikombe viwili. Kimoja alimpa Simon akamsogezea sahani ya bisikuti.
 
“Karibu” alimwambia mgeni wake huku akichukua biskuti moja na kuipeleka midomoni. Alitafuna na kuisukumia na kikombe cha chai.
 
Simon naye aliinua kikombe akapiga funda la chai ya maziwa kisha akaokota bisikuti na kuitia midomoni.
 
“Umekaa ndani miezi mingapi?” James alimuuliza huku akiuweka mguu mmoja juu ya mwingine.
 
“Huu ni mwezi wa sita” Simon alimjibu.
 
“Pole sana, yote ni maisha” James alimwambia baada ya kumeza funda la chai.
 
Pakapita kimya cha sekunde kadhaa kabla ya james kumtazama Simon.
 
“Najua umeshangaa sana kutokana na ushahidi wangu dhidi yako. Nadhani hukuutegemea kabisa”
 
“Ni kweli”
 
“Katika kipindi ambacho wewe uko mikononi mwa polisi niligundua mambo mengi ambayo sikuyatarajia” James aliendelea kumueleza.
 
Alimeza funda la chai kisha akaongeza.
 
“Niligundua kwamba marehemu Maria alikuwa na mchumba mwingine kabla yangu. Kuna visa walifanyiana na Maria akaamua kuvunja uchumba. Kitendo kile cha Maria kuvunja uchumba kilimpa yule mtu chuki akaamua kukutuma wewe umuue…”
 
Muda wote Simon alikuwa kimya akinywa chai huku akimsikiliza James kwa makini.
 
“Baada ya wewe kukamatwa, mtu huyo alimfuata mke wako akamchukua. Alimwambia mume aliyemuoa ni jambazi na atanyongwa kutokana na kukabiliwa na kesi ya mauaji. Hivi sasa mke wako si wako tena amechukuliwa na mtu huyo na anaishi naye nyumbani kwake”
 
Maneno ya kuchukuliwa mke wake na Dokta Kweka yalipiga kwenye moyo wa Simon kama mkuki uliotiwa sumu. Akashituka na kumkazia macho James.
 
James alitoa simu yake akaingia katika eneo la kuhifadhi picha na kumuonesha Simon picha zinazomuonesha Dokta Kweka akiwa na Vicky. Kulikuwa na picha tatu, mojawapo iliyomchoma zaidi Simon ilimuonesha Vicky akipigana busu na Dokta Kweka huku Dokta Kweka amekishika kiuno cha Vicky.
 
“Nilitaka utoke ili nikuoneshe hizi picha. Hivi sasa mke wako anatembea na gari alilopewa na huyo mtu” James alizidi kumuumiza Simon aliyekuwa ameduwaa.
 
James alikuwa amemuachia simu Simon, akainuka na kuanza kuranda.
 
“Mimi ninajua kuwa wewe ulimuua mchumba wangu lakini usingemuua kama usingetumwa. Huyo aliyekutuma si tu amenifanyia ubaya mimi, amekufanyia ubaya na wewe kwa kukuchukulia mke wako. Pengine alikuwa akimtamani siku zote”
 
Simon aliweka simu kwenye kochi akamtazama James. Uso wake sasa ulikuwa umetaharuki.
 
James aliendelea kuranda.
 
“Sikutaka unyongwe na huyo mtu abaki akitanua” alisema na kuongeza.
 
“Nilikutoa kwa makusudi ili nikutume uende ukamuue kama alivyomuua Maria”
 
Jame alisita akamtazama Simon.
 
“Ukimuua mtu huyo nitakuwa nimekusamehe”
 
Simion alikuwa ameduwaa kwa sekunde kadhaa akiwaza. Sebule ikawa kimya. James alikwenda kuketi kando ya Simon.
 
“Unafikiri nini?” akamuuliza.
 
“Nanifikiri kwamba Dokta Kweka amenitoa muhanga” Simon alimjibu huku macho yake yakimkwepa James.
 
“Kwanini?”
 
“Ni kweli alinituma nimuue Maria. Sikujua ni kwanini alitaka Maria afe lakini mbali na hilo bila shaka alijua kuwa nitakamatwa na alishapanga kumchukua mke wangu. Mtu yule ni mshenzi sana”
 
“Nataka uende ukamuue!” James alirudia kumwambia kwa mkazo.
 
“Ameniweka katika wakati mgumu hivi sasa. Miezi sita niliyokaa ndani nimepoteza kila kitu, nyumba, mke na pesa…”
 
“Kwa tatizo la pesa nitakusaidia. Unahitaji kiasi gani cha kuanzia maisha?”
 
“Kama milioni moja hivi”
 
“Nitakupatia laki tano, ukimuua huyo mtu aliyekutuma umuue Maria, nitakumalizia laki tano hapo hapo”
 
“Utanipatia sasa hivi?”
 
“Kama tumekubaliana nitakupatia”
 
“Bado nitkuwa na tatizo la usafiri”
 
“Nitakukodia gari”
 
“Sawa. Nipatie hizo pesa na usafiri. Nitakwenda kumuua”
 
“Unadhani utaweza kumpata kwa leo?”
 
“Kwa leo si rahisi, nipe siku tatu”
 
“Sawa. Sasa twende kwenye ATM nikatoe pesa”
 
James akanyanyuka. Simon naye akainuka. Walitoka nje wakajipakia kwenye gari la James na kuondoka.
 
“Ulifahamianaje na Dokta Kweka?” James alimuuliza Simon wakati gari likiwa kwenye mwendo.
 
“Alinitafuta”
 
ITAENDELEA kesho hapahapa usikose uhondo huu

No comments:

Post a Comment