Tuesday, January 24, 2017

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 19

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU19
 
ILIPOISHIA
 
Simon aliichukua ile bastola akaikagua.
 
“Lakini unaziwekea mafuta hizi bastola, usitukodishie vimeo vinavyokwama wakati wa hatari”
 
“Simon umekuja kufanya mzaha au unataka bastola. Hicho ni kimeo? Si unaona bastola mpya, unasema kibeo!”
 
Simon aliipindisha akaikagua kwa ndani.
 
“Hii mpya wapi, acha ujanja wako Samson! Tena hukuweka risasi!”
 
“Risasi utaweka mwenyewe”
 
“Sasa ziko wapi?”
 
“Umesema unataka risasi ngapi?”
 
“Nimekwambia risasi kumi”
 
SASA ENDELEA
 
“Nipatie hizo pesa kwanza nikupe risasi”
 
“Nitakupa laki mbili, nikikurudishia kesho kutwa nitakumalizia laki yako” Simon alimwambia huku akijipekua mifukoni.
 
Alitoa shilingi laki mbili akampa.
 
Mtu huyo alizihesabu pesa hizo kisha akazitia kwenye mfuko wa bukta aliyokuwa amevaa.
 
“Risasi hizi hapa” alimwambvia huku akimpa risasi hizo alizozitoa mfukoni.
 
“Hii inakaa risasi ngapi?’ Simon akamuuliza wakati akizipokea risasi hizo.
 
“Inakaa risasi kumi na mbili, hiyo ni mashine kubwa”
 
Simon alizitia zile risasi kisha akaiunga ile bastola. Alinyanyuka kutoka kwenye sofa akaipachika bastola ndani ya koti alilokuwa amevaa kisha akamuaga mwenyeji wake.
 
“Mimi nakwenda, makutano ni kesho kutwa” alimwambia na kuelekea kwenye mlango.
 
Mtu huyo hakumjibu kitu, alimtazama tu. Simon alifungua mlango akatoka na kujipakia kwenye gari, akaliwasha na kuondoka. Alirudi jijini.
 
Alikuwa ameshapanga mahali pa kwanza pa kumtega Dokta Kweka ni kwenye mkahawa wa Afrique ambapo Dokta Kweka huenda kupata chai kila asubuhi.
 
Wakati anafika alimuona Kweka akiondoka na gari lake baada kumaliza kunywa chai. Simon akaamua kumfuata nyuma. Alimfuata hadi kwenye kituo cha mafuta ambapo Dokta Kweka alilitia mafuta gari lake.
 
Wakati Kweka analitia mafuta gari hilo, Simon aliliegesha gari pembeni mwa barabara kumsubiri. Dokta Kweka alipoondoka na gari, Simon aliendelea kumfuata nyuma.
 
Kweka alikwenda kusimamisha gari mbele ya hoteli moja maarufu jijini Dar akashuka na kuingia ndani ya hoteli hiyo. Simon naye alilisimamisha gari kwa pembeni.
 
Alisubiri kwa karibu nusu saa. Alipoona Kweka hatokei alishuka na kumfuata ndani ya hoteli. Alimtafuta sehemu mbalimbali bila kumuona, akahisi pengine alikuwa amechukua chumba.
Akaenda mapokezi kumuulizia.
 
“Unasema nani?” msichana aliyekuwa mapokezi alimuuliza.
 
“Dokta Kweka”
 
Msichana alitazama kwenye kitabu cha wageni na kumwambia.
 
“Hapa tuna Alphonce Kweka aliyetoka Mwanza, si Dokta Kweka”
 
Simon kwa kujua huenda Dokta Kweka alikuwa akitumia majina ya bandia na kujifanya anatoka Mwanza alimkubalia.
 
“Ndiye yeye, yuko chumba namba ngapi?”
 
“Nenda chumba namba 45”
 
Chumba namba 45 kilikuwa ghorofa ya kwanza. Simon alipanda ngazi hadi ghorofa ya kwanza akakitafuta chumba namba 45. Alipokiona alifungua mlango akaingia ndani bila kubisha akiwa na hakika kwamba atakutana Dokta Kweka.
 
Lakini alipoingia alikutana na kitu cha kushangaza sana. Alimkuta Dokta Kweka amelala chini huku damu ikimvuja kwenye kifua. Simon alishuhudia tundu mbili za risasi zilizokuwa zikivuja damu kwenye kifua cha Kweka.
 
Ingawa macho ya Kweka yalikuwa wazi yakilitazama dari jeupe la chumba cha hoteli lakini hayakuwa na uhai wowote. Simon hakuhitaji mtaalamu wa kumuuliza kama mtu huyo alikuwa hai au alikuwa amekufa. Alithibitisha yeye mwenyewe kuwa Kweka hakuwa hai.
 
Kutokana na uthibitisho wa tundu mbili za risasi zilizokuwa zikivuja damu kifuani mwa Kweka ilitosha kumuonesha Simon kuwa Kweka alipigwa risasi mbili sekunde chache tu zilizopita.
 
Simon aliyazungusha macho yake ndani ya chumba hicho na kujiuliza ni nani aliyempiga risasi Kweka katika muda mfupi ule. Alikosa jibu akaona ageuke na kutoka ndani ya kile chumba. Alifunga mlango akatoa kitambaa cha mkononi na kukisafisha kitasa kufuta alama zake za vidole kisha akaondoka.
 
Alipotoka nje ya hoteli hakuliona lile gari la Kweka. Wakati anaelekea lilipokuwa gari lake alimuona mke ake aliyekuwa amechukuliwa na Dokta Kweka akishuka kwenye teksi. Akajifanya hakumuona, alikwenda alipoliacha gari akafungua mlango na kujipakia.
 
Kabla ya kuliwasha gari hilo alimuona mke wake akiingia ndani ya hoteli. Aliwaza kwamba huenda Kweka alikuwa amepangana na msichana huyo wakutane hapo. Lakini atakachokwenda kukiona mle chumbani kitamshangaza, Simon alijiambia.
 
Aliliwasha gari na kuondoka mahali hapo. Akili yake ilikuwa ikijaribu kutafuta ni nani aliyemuua Dokta Kweka. Alijiambia kama alivyokuwa akimuinda yeye kulikuwa na mtyu mwingine aliyekuwa akimuinda ili amuue.
 
Atakuwa ni mtu mwepesi na wa ajabu sana, Simon alijiambia akiamini kuwa muuaji huyo alikuwa pale hoteli wakati Kweka anafika.
 
Simon aliamini kuwa baada ya mtu huyo kumuua Kweka, ndiye aliyeondoka na gari lake sekunde chache tu zilizopita. Simon alijiambia kama angewahi kutoka tu angemfuma akiondoka na gari hilo na angemtambua.
 
Simon aliendelea kujiambia kuwa japokuwa Kweka ameuawa na mtu mwingine aende akamwambie James kuwa amemuua yeye ili aweze kumpa pesa aliyomuahidi.
 
Asante sana muuaji, umenirahisishia kazi. Sasa nitaona ujanja wa yule mwanamke aliyenitoroka mimi, Simon alijiambia kwa faraja.
 
Alitoa simu akampigia James.
 
James lipopokea simu alimuuliza.
 
“James uko kazini au uko nyumbani?”
 
“Niko kazini” James alimjibu kwenye simu.
 
“Ukitoka mchana kwenda kula tukutane”
 
“Si unapafahamu pale ninapokula?”
 
“Ndiyo”
 
“Nikukute hapo”
 
“Sawa”
 
Wakati Simon anakata simu alipata wazo jingine. Upande mmoja wa akili yake ulimwambia arudi pale hoteli ili aone nini kitatokea. Akageuza gari na kurudi. Alipofika hapo hoteli aliliegesha gari pembeni.
 
Tayari alishaona gari la polisi na gari la hospitali yaliyokuwa yamesimama mbele ya mlango wa hoteli. Wakati anasimamisha gari aliona polisi waliobeba machela iliyokuwa na mwili wa Dokta Kweka wakitoka kwenye mlango wa hoteli.
 
Mwili huo ulipakiwa kwenye gari la hospitali. Simon alimuona msichana wa Kweka aliyekuwa mke wake akitolewa na polisi akiwa analia huku mikono yake imefungwa pingu.
 
Alipakiwa kwenye gari la polisi. Gari hilo likaondoka pamoja na gari la hospitali.
 
Ndipo Simon alipoondoka. Hakujua ni kwanini mke wake wa zamani alikamatwa, wakati alipofika hapo hoteli Kweka alikuwa ameshauawa.
 
ITAENDELEA kesho usikose hapahapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment