Thursday, January 12, 2017

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 16

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 16
 
ILIPOISHIA
 
Akaendelea “ Nimeupitia ushahidi uliotolewa na mashahidi wawili wa upande wa mashitaka. Shahidi wa kwanza amejitoa kuwa shahidi wa upande wa utetezi kutokana na maelezo yake kumnufaisha mshitakiwa. Yeye ndiye aliyekuwa shahidi muhimu wa upande wa mashitaka na amekuwa shahidi muhimu wa upande wa utetezi.
 
“Kwa vile shahidi muhimu aliyetegemewa na upande wa mashitaka kueleza mahakama jinsi mshitakiwa alivyofanya mauaji amedai kuwa mshitakiwa aliyeletwa mahakamani siye aliyeua na hakukuwa na shahidi mwingine aliyesema kuwa mshitakiwa ndiye aliyeua, tayari ushahidi huo umeshakuwa ni faida kwa mshitakiwa”
 
Jaji aliinua uso wake akamtazama Mwendesha Mashitaka kisha akaendelea.
 
“Shahidi wa pili ambaye ni mpelelezaji wa kesi hii ameshindwa kuielezea mahakama kinaganaga uhusiano wa alama za vidole za mshitakiwa zilizokuwa kwenye simu ya marehemu na kwenye kitasa cha mlango wa marehemu zinahusiana vipi na mauaji yaliyotokea.
 
“Kwa hivyo mahakama hii inamuona mshitakiwa hana kosa la kujibu kutokana na kukosekana kwa ushahidi wa kutosha amabao ungeweza kumtia hatiani mshitakiwa. Mshitakiwa hutiwa hatiani kwa kukiri kosa yeye mwenyewe au kwa ushahidi unaodhihirisha kosa bila kuacha shaka”
 
SASA ENDELEA
 
Jaji aliinua tena uso wake akamtazama Mwendesha Mashitaka ambaye uso wake ulikuwa umepatwa na fadhaa. Akaendelea kusoma muhutasari huo.
 
“Katika kesi ya mauaji kama hii ambayo hukumu yake inaweza kuwa kifo ni lazima kuwepo ushahidi mzito na usio na shaka. Kwa hiyo narudia kusema kuwa mshitakiwa hana kosa la kujibu na namuachia huru”
 
Alipofika hapo alimtazama mshitakiwa  na kumwambia.
 
“Uko huru, nenda zako”
 
Simon Puto alikuwa amepatwa na kiwewe cha kuachiwa. Alikuwa amemkodolea macho jaji kabla ya kuzinduka na kushuka kizimbani haraka. Alipongezana na wakili wake ambaye alikuwa akimsubiri mbele ya kizimba mara tu jaji alipomwambia, nimukuachia huru”
 
Mwendesha Mashitaka na Inspekta Amour walikuwa wakiwatazama huku wakitikisa vichwa kwa uchungu.
 
Baada ya kupongezana na wakili wake, Simon alitoka nje ya mahakama na kukutana na James aliyekuwa akimsubiri mbele ya lango la mahakama.
 
James alimpa mkono na kumpongeza kutokana na kuachiwa huru. Akampigapiga kwenye bega na kumwambia.
 
“Kupotea njia ndiyo kujua njia, usijali”
 
“Asante sana” Simon alimjibu uso wake ukiwa umejaa aibu.
 
“Okey gari ile pale, twendezetu”
 
James alimuonesha gari lake alilokuwa ameliegesha mbele ya viwanja vya mahakama.
 
James na Simon walifuatana kuelekea kwenye gari hilo. Wakajipakia. James akaliwasha na kuondoka na Simon.
 
Miaka miwili iliyopita mtu mmoja ambaye aliwahi kufanya kazi wizara ya afya akiwa na taaluma ya udaktari aliwahi kusuhubiana na Maria kabla ya kifo chake.
 
Dokta Kweka alifahamiana na Maria kwa sababu ya kufika mahakamani mara kwa mara akiwa na shughuli zake binafsi zilizohitaji vibali vya mahakama.
 
Wakati huo Maria akiwa karani wa mahakama ndiye aliyekuwa akimhudumia Dokta Kweka, kupokea nyaraka zake na kuzifikisha kwa hakimu na kisha kuzichukua tena kwa hakimu na kumpa Dokta Kweka.
 
Alikuwa akimrahisishia sana kazi. Badala ya Kweka kusota kwenye mabenchi ya mahakama kumsubiri hakimu au kuelekezwa kwenda huku na huko, alikuwa akizikabidhi kazi zake kwa Maria ambaye huzishughulikia na kisha huja kuzichukua tena kwa Maria.
 
Maria alikuwa akimtumikia Kweka kwa sababu Kweka alikuwa akimpa bahashishi nono. Kuna siku Kweka alikwenda mahakamani hapo asubuhi akampa nyaraka zake Maria. Maria akamwambia azipitie mchana.
 
Saa sita mchana Kweka alifika mahakamani. Maria alikuwa ameshazishughulikia. Akampa.
 
“Naomba tuonane saa saba kwa ajili ya chakula cha mchana” Kweka akamwambia Maria.
 
“Unataka kunipa ofa?” Maria akamuuliza.
 
“Au hupendi?”
 
“Kwanini…tukutane hoteli gani?’
 
“Nitakuwa pale Afrique”
 
“Nitahitaji usafifiri”
 
“Usijali”
 
Dokta Kweka alitia mkono kwenye mfuko wa ndani wa koti lake akatoa noti mbili za shilingi elfu kumi kumi akampa.
 
“Usafiri wako ndio huo”
 
“Asante”
 
“Usikose”
 
“Sitakosa”
 
Kweka akaondoka.
 
Saa saba mchana Maria akafika Afrique. Ulikuwa mkahawa uliokuwa juu ya ghorofa. Watu waliokuwa wakiingia katika mkahawa huo walikuwa watu wanaojiweza kwani bei yake ya vyakula ilikuwa kubwa.
 
Maria alimkuta Kweka akimsubiri. Alipomuona alimfuata kwenye meza aliyokuwa ameketi na yeye akaketi. Mhudumu alipowaendea, Kweka alimwambia Maria.
 
“Agiza chakula unachotaka”
 
Kweka mwenyewe aliagiza ugali na kuku. Maria akaagiza chips kuku. Wote wawili walitaka waletewe pia juisi ya nanasi.
 
Mhudumu alipoondoka. Kweka aliendelea kusoma gazti alilokuwa amelishika mkononi.
 
Vyakula walivyoagiza vilipoletwa, Kweka alilikunaja gazeti wakaanza kula.
 
“Kuna kitu nilikuwa nataka kukwambia Maria, umekuwa ukinisaidia sana. Nashukuru kwa hilo. Nilikuwa nikijiuliza ni kwanini tusisuhubiane mimi na wewe?” Kweka alimwambia Maria.
 
Maria alinyamaza kimya.
 
“Nadhani nitatafuta muda mwingine mzuri zaidi ili tuliongelee hilo kwa kirefu au unasemaje?”
 
Maria akabetua mabega.
 
“Ni sawa tu”
 
“Unadhani lini utakuwa na nafasi nzuri, siku ambayo si ya kazi?”
 
“Jumapili mchana nikitoka kanisani”
 
“Nitakupata wapi?”
 
“Hapa hapa”
 
“Naomba unipatie namba yako ya simu”
 
Maria hakuwa na uchoyo na namba yake, akampa. Kweka naye akampa namba yake. Baada ya kumaliza chakula Kweka alimpa Maria shilingi laki moja.
 
“Zitakusaidia kununulia vocha ya simu”
 
“Asante sana, nashukuru”
 
Wakaagana. Siku ya jumapili Maria alitimiza ahadi. Alipotoka kanisani alipanda teksi hadi mkahawa wa Afrique. Alipofika akakutana na Kweka.
 
Siku ile ndio Kweka alimtolea undani wake. Alimwambia wazi kuwa alikuwa akimuhitaji katika maisha yake. Kule kutoa kauli ya kukubali tu, Kweka alimpeleka ‘shopping’ siku ile ile. Alimfanyia shoping ya shilingi laki tano.
 
ITAENDELEA kesho hapahapa tangakumekuchablog, usikose uhondo huu

No comments:

Post a Comment