Saturday, January 28, 2017

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 21

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 21
 
ILIPOISHIA
 
James lipopokea simu alimuuliza.
 
“James uko kazini au uko nyumbani?”
 
“Niko kazini” James alimjibu kwenye simu.
 
“Ukitoka mchana kwenda kula tukutane”
 
“Si unapafahamu pale ninapokula?”
 
“Ndiyo”
 
“Nikukute hapo”
 
“Sawa”
 
Wakati Simon anakata simu alipata wazo jingine. Upande mmoja wa akili yake ulimwambia arudi pale hoteli ili aone nini kitatokea. Akageuza gari na kurudi. Alipofika hapo hoteli aliliegesha gari pembeni.
 
Tayari alishaona gari la polisi na gari la hospitali yaliyokuwa yamesimama mbele ya mlango wa hoteli. Wakati anasimamisha gari aliona polisi waliobeba machela iliyokuwa na mwili wa Dokta Kweka wakitoka kwenye mlango wa hoteli.
 
Mwili huo ulipakiwa kwenye gari la hospitali. Simon alimuona msichana wa Kweka aliyekuwa mke wake akitolewa na polisi akiwa analia huku mikono yake imefungwa pingu.
 
Alipakiwa kwenye gari la polisi. Gari hilo likaondoka pamoja na gari la hospitali.
 
Ndipo Simon alipoondoka. Hakujua ni kwanini mke wake wa zamani alikamatwa, wakati alipofika hapo hoteli Kweka alikuwa ameshauawa.
 
SASA ENDELEA
 
Simon  akafikiria kwamba aende Kimara. Kwa vile kile alichokuwa anakitaka kimetimia aliona aende akajipongeze kwa kinywaji kwenye baa ya ABC.
 
Alipofika alilisimamisha gari kwenye eneo la kuegesha la ABC akashuka na kuingia ndani. Akiwa kwenye ukumbi wa baa, Simon alizungusha macho kumtafuta kimanzi wake, lakini hakumuona.
 
Alikwenda kaunta akaketi kwenye kigoda na kumuuliza msichana aliyemkuta.
 
“Kimanzi wangu yuko wapi?”
 
“Anaingia usiku” msichana huyo alimjibu.
 
“Oh! Sikufurahi kutomkuta, nipatie kinywaji”
 
“Unaweza kumfuata nyumbani kwake kama unamuhitaji”
 
“Muda huo wa kufuatana majumbani ndio sina”
 
“Basi njoo usiku”
 
“Nipatie kinywaji”
 
“Kinywaji gani?”
 
“Ndiyo tatizo la kutomkuta Kimanzi, yeye ndiye anayejua kila kitu. Nipatie toti mbili za kunyagi na kibonge cha barafu”
 
“Ukija tena kesho nitakuwa ninajua sasa”
 
Msichana alimpatia kinywaji hicho. Simon aliinua bilauli akaipiga funda konyagi iliyopozwa kwa barafu kisha akaimeza huku akikunja uso.
 
Aliondoka hapo baa majira ya saa sita. Ingawa alikunywa konyagi ya kutosha, hakuonesha dalili yoyote ya kulewa. Alikwenda katika hoteli aliyopanga kukutana na James.
 
Alipofika alimkuta James ameshafika.
 
“Nina habari njema, nataka kukwambia” Simon aliwambia James huku akiketi.
 
“Niambie”
 
“Nimeshamuua Dokta Kweka”
 
“Sipendi utani Simonai!
 
“Si utani, tayari nimemuua”
 
“Umempata wapi?”
 
“Nilimuandama na gari hadi Suzy Hotel, alikwenda kupangisha chumba pale sijui ni kwa ajili gani. Nikamuingilia chumbani na kumpiga risasi mbili”
 
James alikuwa akimsikiliza kwa makini.
 
“Ilikuwa saa ngapi?”
 
“Wakati ule ninakupigia simu ndiyo ninatoka kumuua”
 
“Simon una hakika kuwa umemuua?”
 
“Amini usiamini. Maiti yake imechukuliwa na polisi na yule mke wangu alijitokeza pale naye alikamwatwa”
 
“Alikamatwa kwa sababu gani?”
 
“Sijajua bado lakini nadhani ni kwa sababu alikutwa katika eneo la tukio akashukiwa yeye”
 
“Wakati huo wewe ulikuwa wapi?”
 
“Mimi baada ya kumpiga risasi, nilitoka haraka mle chumbani nikashuka chini na kuingia garini. Nilikaa kwenye gari kwa muda mrefu, nikamuona yule mwanamke. Alifika pale kwa teksi, sijui alifuata nini. Akaingia ndani ya hoteli. Baadaye nikaona polisi wamefika”
 
“Nitakwenda hapo hoteli kuhakikisha”
 
“Itakuwa vyema sana, nenda sasa hivi”
 
“Chakula pia nitasamehe, acha niende kwanza. Nitakupigia simu nikueleze tukutane wapi. Sawa?”
 
James alikuwa ameshanyanyuka kwenye kiti.
 
“Sawa”
 
James akatoka na kumuacha Simon akimtazama.
 
Dakika chache baadaye alilisimamisha gari mbele ya hoteli ya Suzy. Mandhari aliyoiona hapo nje ya hoteli, peke yake ilimuashiria kuwa palikuwa na tukio ambalo halikuwa la kawaida.
 
Mbali ya polisi kuendelea kuonekana katika eneo hilo kulikuwa na watu waliokuwa wamezagaa mbele ya hoteli.
 
James alishuka kwenye gari akaelekea kwenye mlango wa hoteli. Aliwasikia watu wakizungumza kuhusu mtu aliyeuawa kwa kupigwa risasi ndani ya chumba cha hoteli hiyo.
 
Aliingia ndani ya hoteli akaelekea upande wa mkahawa. Kulikuwa na watu wawili watatu wakila chakula lakini wafanyakazi wa hotelini hapo walionekakana kuwa kwenye taharuki.
 
James aliketi kwenye meza iliyokuwa na mtu mmoja.
 
“Kaka habari ya saa hizi?” akamsalimia.
 
“Nzuri. Karibu”
 
“Asante”
 
Mhudumu alipomfuata alimuagiza chakula alichohitaji. Mhudumu alipoondoka alimuuliza yule mtu aliyemkuta akila chakula.
 
“Pametokea nini hapa hoteli, naona watu wengi na polisi?’
 
“Nilisikia kuna mtu ameuawa humu ndani” Mtu huyo alimjibu.
 
James akajifanya anashangaa.
 
“Kuna mtu ameuawa humu ndani ya hoteli?”
 
“Nimesikia aliuawa chumbani, alipigwa risasi na mtu asiyefahamika”
 
“Huyo mtu amekamatwa?”
 
“Hakufahamika”
 
“Loh! Dar es Salaam imeharibika sana siku hizi. Watu wanauana kama nzige!”
 
“Kwa kweli inatisha sana”
 
“Na sidhani kama atapatikana”
 
“Nimesikia kuna mwanaamke aliyekamatwa aliyehusishwa na hayo mauaji”
 
“Mwanamke? Alikamatwa wapi?”
 
“Hapa hapa hoteli”
 
Pakapita kimya hadi chakula alichoagiza James kilipoletwa.
 
“Eti huyo mtu aliyeuawa hapa hoteli ni nani?” James akamuuliza mhudumu huyo.
 
“Alikuwa ni mteja wetu. Alichukua chumba tangu jana. Leo mchana ndio amekutwa amepigwa risasi chumbani” Mhudumu huyo akamueleza.
 
“Alichukua chumba tangu jana?”
 
“Ndiyo alikuja jana, hatujui ni nani aliyemuua na kwa sababu gani”
 
“Eti kuna mwanamke aliyekamatwa?”
 
“Huyo mwanamke ndiye aliyesababisha tujue kuwa huyo mtu ameuawa. Aliingia mle chumbani kisha akatoka na kupiga kelele”
 
“Kwa hiyo siye aliyemuua?’
 
“Hatujui. Yeye anadai yule mtu ni mume wake lakini yule bwana alikuja peke yake hapa hoteli”
 
“Polisi wamemkamata kwa kumtilia mashaka?” Yule mtu mwingine alisema.
 
Baada ya hapo mhudumu aliondoka. James alipomaliza kula alilipa pesa naye akaondoka. Sasa aliamini kuwa Dokta Kweka alikuwa ameuawa.
 
“Nitapata mengi kwenye taarifa ya habari ya usiku” James alijiambia wakati akiendesha gari kurudi kazini kwake.
 
                            **************
 
Alikuwa mfanyakazi mmoja wa hoteli ya Suzy aliyeitwa Mage ambaye alimpigia simu Vicky na kumjulisha kuwa mwanaume wake alikuwa amepangisha chumba hapo hoteli.
 
Vicky ambaye alikuwa mke wa Simon kabla ya kuchukuliwa na Dokta Kweka alikuwa akifahamiana na Mage na ulikuwa umbea tu wa kike uliomfanya Mage ampigie simu.
 
ITAENDELEA kesho usikose uhondo huu

No comments:

Post a Comment