Saturday, January 28, 2017

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 22

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 22
 
ILIPOISHIA
 
Alimuita kwa kumpigia simu ya mkononi.
 
“Rose unaitwa hapa kaunta”
 
“Naitwa na nani?” Sauti ya Rose ikauliza kwenye simu.
 
“Kuna askari anakuulizia”
 
“Anataka nini?”
 
“Sijui, we njoo umsikilize. Si unajua kuna tukio limetokea hapa hoteli”
“Mimi bado nina kazi”
 
“Njoo mara moja”
 
Fatuma akakata simu. Dakika chache baadaye Rose akafika hapo mapokezi. Alimsalimia Inspekta Temba kisha akamuuliza Fatuma.
 
“Nani ananiita?”
 
“Nimekuita mimi” Inspekta Temba alimwambia na kuongeza. 
 
“Naitwa Inpekta Temba, natokea makao ya polisi. Wewe ndiye Rose?”
 
“Ndiye mimi”
 
“Unamfahamu Vicky?”
 
“Namfahamu?”
 
“Ni kweli kwama mtu aliyeuawa hapa hoteli ni mume wake?”
 
“Ndio, ni mume wake”
 
“Wewe ndio ulimpigia simu kumjulisha kuwa mume wake amekodi chumba hapa hoteli”
 
Rose akagwaya.
 
“Nataka jibu”
 
SASA ENDELEA
 
“Nilimpigia lakini tulikuwa na maongezi mengine, hilo nililiingiza tu baada ya kumuona mume wake yuko hapa”
 
“Sawa. Hebu nieleze ukweli, huyo mume wake alikuwa na msichana?”
 
“Sikumwambia kama mume wake alikuwa na msichana…”
 
“Najua hukumwambia isipokuwa nakuuliza mimi, je mume wake alikuwa na msichana”
 
“Sikumuona na msichana”
 
“Nina maana kwamba kama alikuwa na msichana ndiye atakuwa muuaji”
 
“Kusema kweli hakuwa na msichana”
 
“Au alikuwa naye lakini hamkumuona, pengine alikuja baadaye”
 
“Inawezekana”
 
“Sawa, asanteni sana. Nitakuja kuwaona wakati mwingine”
 
Dakika chache baadaye wakati Temba akiwa kwenye gari alipigiwa simu na kamanda wa polisi.
 
Ingawa hakupenda kuzungumza kwenye simu wakati anaendesha lakini alipoona namba ya kamanda wake aliipokea simu haraka.
 
“Afande, nakusikiliza”
 
“Uchunguzi wako juu ya mauaji yaliyotokea katika hoteli ya Suzy umefikia wapi?” Sauti nzito ya kamanda wa polisi ikamuuliza kutoka simu ya upande wa pili.
 
“Bado ninaendelea na uchunguzi huo”
 
“Waandishi wa habari wameanza kufika ofisini kwangu kutaka kujua nini kilitokea hadi mtu huyo akauawa. Lakini mpaka sasa sijakuwa na taarifa kamili”
 
“Yule mtu alikutwa akiwa ameshakufa katika chumba alichokuwa amepangisha tangu jana. Aliyegundua maiti yake ni msichana mmoja aliyedai ni mke wa marehemu, alifika pale hoteli na kugundua kuwa mume wake alikuwa ameuawa”
 
“Huyo msichana aliyedai ni mke wa marehemu alitokea wapi?”
 
“Alifika pale hoteli baada ya kupigiwa simu na mfanyakazi mmoja wa hapo hoteli ambaye ni rafiki yake, alimwambia kwamba mume wake alikuwa amechukua chumba hapo hoteli. Nadhali alikuwa amekuja kumfumania akidhani mume wake alikuwa na msichana”
 
“Sasa uchunguzi wenu wa awali umeonesha kwamba marehemu aliuawa kwa sababu gani na labda aliuawa na nani?”
 
“Ndio tunaendelea na uchunguzi afande”
 
“Kuna mtu yeyote ambaye mnamshikilia kufuatia tukio hilo”
 
“Tunamshikilia yule msichana ambaye alidai ni mke wa marehemu”
 
“Ningependa hadi kesho mchana nipate taarifa iliyo kamili”
 
“Sawa afande nitajitahidi”
 
Simu ikakatwa.
 
                                ********
 
Saa mbili usiku James akiwa mbele ya televisheni yake aliisikia taarifa ya kuuawa kwa Stiphano Kweka na mwili wake ulioneshwa ukipakiwa kwenye gari la polisi.
 
Taarifa ya polisi ikaeleza kuwa mtu huyo aliuawa kwenye chumba cha hoteli ya Suzy ambacho alikuwa amepangisha.
 
Taarifa hiyo iliendelea kueleza kuwa Kweka aliuawa kwa kupigwa risasi mbili za bastola kifuani akiwa katika chumba hicho na kwamba polisi walikuwa wanamshikilia msichana mmoja aliyedai kuwa ni mke wa marehemu kwa uchunguzi wa tukio hilo.
 
Baada ya kuiona taarifa hiyo James alimpigia simu Simon.
 
“Kesho ni jumamosi siendi kazini, njoo nyumbani kwangu saa nne asubuhi nikupe chako” alimwambia.
 
“Lakini umeshathibitisha”
 
“Ndiyo nimethibitisha”
 
“Sawa. Basi ni hapo kesho asubuhi”
 
James akakata simu. Alifarijika sana kupata uhakika kuwa Kweka alikuwa ameuawa.
 
“Sasa nimetimiza kisasi changu, hata Maria huko aliko atafurahi” akajiambia kimoyo moyo.
 
Akiwa amelala katika chumba cha mahabusi usiku, Vicky alipata wazo ambalo hapo mapema hakuwa amelitia maanani. Pengine ilikuwa sakafu ya mahabusi iliyokuwa ikizizima ndiyo iliyomfanya amkumbuke Simon.
 
Alikumbuka kwamba wakati nafika katika hoteli ya Suzy alimuona Simion. Alimuona wakati anashuka kutoka kwenye teksi iliyokuwa imempeleka hotelini hapo. Alipomuona aliugeuza uso wake haraka akajifanya kama hakumuona.
 
Akajiuliza Simon alifuata nini pale hoteli? Na licha ya kuwa na hakika kuwa alionekana na Simon, alijiuliza ni kwanini Simon hakumuulia kitu wakati anajua kuwa alimtoroka na kuchukuliwa na mwanume mwingine?
 
Hapo ndipo shaka ilipoingia kwa Viky, kwamba huenda Simon ndiye aliyemuua Dokta Kweka kwa chuki ya kuchukuliwa mke wake.
 
“Wazo hilo halikunijia mapema lakini inawezekana kuwa Simon ndiye aliyemuua Dokta Kweka kwa sababu alishawahi kukamatwa kwa tuhuma za mauaji” Vick alijiambia huku akiinuka.
 
Aliketi kwenye sakafu na kuendelea kujiambia.
 
“Kama ningewambia polisi mapema, Simon angelikwishakamatwa na pengine wangeniachia mimi”
 
Asubuhi kulipokucha Vicky aliwambia polisi kuwa alitaka kuzungumza na Inspekta Temba. Polisi walidhani kuwa Vicky alikuwa ameamua kulikiri kosa la mauaji.
 
Inspekta Temba alipofika alijulishwa kuwa Vicky alikuwa anataka kuzungumza naye.
 
“Mleteni” akawambia.
 
Polisi mmoja mwanamke alikwenda kumtoa mahabusi na kumpeleka ofisini kwa Temba.
 
“Kaa kwenye kiti” Temba alimwambia. Ilikuwa nadra sana kwa polisi kumkaribisha mtuhumiwa kwenye kiti.
 
Vicky akaketi.
 
“Unasemaje?” akamuuliza.
 
“Kuna kitu ambacho jana nilisahau kukizungumza” Vicky akaanza.
 
“Kitu gani? Kizungumze hivi sasa”
 
“Mimi kabla ya kuolewa na marehemu nilikuwa na mume mwingine anayeitwa Simon. Tulitenganishwa na Padre baada ya mume wangu huyo kukabiliwa na kesi ya mauaji….”
 
“Ndiyo, endelea”
 
 “Mwanzo nilijua kuwa atanyongwa lakini baadaye mahakama ilimuachia huru kwa kumuona hakuwa na hatia”
 
“Ndiyo”
 
“Mimi sikutaka tena kurudi kwa yule mwanaume, ninahisi kuwa yeye ndiye amemuua Dokta Kweka”
 
“Unahisi tu au unayo maelezo zaidi ya kutuambia?”
 
“Ninahisi na pia nilimuona jana pale hoteli?”
 
Inspekta Temba akagutuka.
 
“Ulimuona wakati gani na alikuwa wapi?”
 
“Wakati nashuka kwenye teksi nilimuona”
 
“Ulimuona wapi?”
 
“Nilimuona akitoka kwenye mlango wa hoteli”
 
“Halafu akaenda wapi?”
 
“Sikumpatiliza tena, mimi nilijifanya kama sikumuona nikaingia hoteli. Na ndio nikaenda kumkuta Kweka ameuawa kule chumbani”
 
“Yeye alikuona?”
 
“Nina hakika kuwa aliniona”
 
“Alikusemesha chochote?”
 
“Hakunisemesha”
 
“Je aliwahi kukwambia au kumwambia marehemu kuwa atafanya kitu?’
 
“Hakuwahi kuniambia wala kumwambia marehemu kuwa atafanya kitu lakini nina shaka naye”
 
“Ungetuambia tangu jana tungelikwisha mkamata. Anaweza kuwa mtuhumiwa namba mbili. Anapatikana wapi?”
 
“Kwa sasa sijui anapatikana wapi?”
 
“Unadhani tutampataje”
 
“Hapo siwezi kujua”
 
“Una namba yake ya simu?”
 
ITAENDELEA kesho hapahapa tangakumekuchablog, Usikose uhondo huu

No comments:

Post a Comment