Monday, January 16, 2017

HADITHI, ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU SEHEMU YA 17

HADITHI
 
ALIYEMUUA MCHUMBA WANGU 17
 
ILIPOISHIA
 
“Unadhani lini utakuwa na nafasi nzuri, siku ambayo si ya kazi?”
 
“Jumapili mchana nikitoka kanisani”
 
“Nitakupata wapi?”
 
“Hapa hapa”
 
“Naomba unipatie namba yako ya simu”
 
Maria hakuwa na uchoyo na namba yake, akampa. Kweka naye akampa namba yake. Baada ya kumaliza chakula Kweka alimpa Maria shilingi laki moja.
 
“Zitakusaidia kununulia vocha ya simu”
 
“Asante sana, nashukuru”
 
Wakaagana. Siku ya jumapili Maria alitimiza ahadi. Alipotoka kanisani alipanda teksi hadi mkahawa wa Afrique. Alipofika akakutana na Kweka.
 
Siku ile ndio Kweka alimtolea undani wake. Alimwambia wazi kuwa alikuwa akimuhitaji katika maisha yake. Kule kutoa kauli ya kukubali tu, Kweka alimpeleka ‘shopping’ siku ile ile. Alimfanyia shoping ya shilingi laki tano.
 
SASA ENDELEA
 
Kutoka hapo Kweka na Maria wakawa wapenzi. Siku zote walikuwa wakikutana kwenye mahoteli tu. Maria aliwahi kumfikisha nyumbani kwake mara kadhaa lakini Kweka hakumuonesha Maria alikuwa anaishi wapi zaidi ya kumwambia kuwa alikuwa akiishi Masaki.
 
Mapenzi yalipowakolea walifunga uchumba. Uchumba huo ulidumu kwa mwezi mmoja tu kabla ya Maria kupata balaa la kukamatwa na kuwekwa ndani.
 
Kweka alikuwa ameshitakiwa kwa kugushi nyaraka za wizara kwa ajili ya shughuli zake binafsi. Alipotolewa kwa dhamana alimtuma Maria kulitafuta faili la kesi yake hapo mahakamani na kuchomoa nyaraka muhimu za ushahidi ili kuharibu kesi.
 
Maria kwa sababu ya kutaka mpenzi wake asifungwe alifanya hivyo. Uchunguzi ulipofanyika ilibainika kuwa baadhi ya nyaraka za ushahidi hazikuwemo kwenye faili la Kweka. Shuku ikaenda kwa Maria. Maria akashukiwa kuzichomoa nyaraka hizo.
 
Polisi walimkamata akafunguliwa mashitaka. Wakati yeye akiendelea na kesi, Kweka alikuja kuachiwa kutokana na kukosekana kwa ushahidi. Uamuzi huo ulikuja baada ya kesi yake kuchukua muda mrefu.
 
Baada ya Kweka kuachiwa hakushughulika tena na Maria. Alibadili namba yake ya simu. Maria akawa hampati kwenye simu. Alikuwa akimtafuta ili amueleze kuwa kesi yake ilikuwa imekaa vibaya na kwamba alihitaji pesa za kuweka wakili.
 
Maria alipogundua kuwa Kweka alikuwa amemtosa, pengine akiamini kuwa angemtaja mahakamani aliamua kuachana naye.
 
Ulikuwa ni wakati ule anakutana na James ambaye alimwambia kuwa alikuwa na mchumba wake lakini mwisho akamwambia hakuwa na mchumba bila kumfafanulia.
 
Mungu si Athumani, hakimu aliyekuwa akisikiliza kesi ya Maria alimuachia huru kwa kukosekana kwa ushahidi wa kutosha kwamba ni yeye aliyechomoa nyaraka hizo.
 
Siku chache baada ya Maria kuachiwa huru Kweka alianza kumpigia Maria. Maria alipokea simu yake na kumuuliza alikuwa akihitaji nini.
 
“Maria nilikuwa London, nimerudi jana” Kweka alimwambia Maria kwenye simu.
 
“Kwenda zako, wewe ni tapeli mkubwa. Sina hamu ya kukuona wala usinipigie simu”
 
“Maria unanijibu hivyo, kumbuka tunatoka wapi?”
 
“Kwanini hukukumbuka wewe wakati ule nakabiliwa na kesi. Leo unaona nimeachiwa ndio unanipigia simu. Wewe mwanaume mbaya sana. Ulinituma nikuchomolee nyaraka nikafanya hivyo ili kukusaidia wewe, halafu ukaamua kunitosa!”
 
“Sijakutosa, nimekwambia nilikuwa safari na safari yenyewe ilikuwa muhimu kwa maisha yetu. Nikubalie mchumba wangu ili tuanze kupanga harusi yetu”
 
“Kwenda zako tapeli mkubwa. Ulikuwa hapa hapa nchini, sema ulibadili namba yako kwa kujua ningefungwa, hata utu huna. Ulishindwa kukumbuka kwamba wewe ndiye uliyeniponza!”
 
“Kwa hiyo umeamua kuvunja uchumba wetu?
 
“Uchumba umeshavunjika muda mrefu hivi sasa nina mchumba mwingine anaayenipenda na kunijali”
 
“Kumbuka kwamba nilikupa pesa zangu nyingi”
 
“Na wewe kumbuka kwamba ulinitumia sana mpaka ukasababisha nipate kesi”
 
“Maria fikiria tena uamuzi wako”
 
“Sifikirii na nimesha amua!”
 
Maria akakata simu.
 
Tangu siku ile Maria hakupokea tena simu za Kweka.
 
Ndipo Kweka alipomtafuta Simon Puto, muuaji wa kukodiwa. Simon alikuwa akiishi nchini Kenya ambako alifanya mauaji mengi. Baada ya msako wa kumtafuta kupamba moto alirudi nchini.
 
Akiwa jijini Dar alishirikiana na vikundi vingi vya ujambazi. Baada ya wenzake wengi kuishia mikononi mwa polisi aliamua kujitenga na vikundi na kufanya kazi peke yake.
 
Yeye na Kweka walipeana ahadi kwenye simu wakutane katika hoteli ya New Africa. Walipokutana ndipo Kweka alipompa kazi ya kumpeleleza Maria ili kujua kama kweli alikuwa na mchumba mwingine.
 
 Ili kufanya upelelezi wake kwa ufanisi Kweka alimpa Simon shilingi laki tano.
 
Simon akaanza kazi ya upelelezi, akaja kugundua kuwa Maria alikuwa akishirikiana na kijana mmoja aliyekuwa akiishi Msasani.
 
Kazi yake kubwa ilikuwa ni kumuandama James kutoka nyumbani kwake hadi kazini kwake kila asubuhi.
 
Alikuwa akimsubiri, anapotoka mchana aliendelea kumfuatilia hadi sehemu anayokwenda kula. Jioni alikuwa nyuma yake hadi anafika nyumbani kwa Maria.
 
Ndipo siku moja alipomuibukia James katika hoteli ambayo alikwenda kula chakula cha mchana, akamuuliza kama alikuwa na uchumba na Maria. (Rejea sehemu ya tatu ya riwaya hii) James akamjibu kuwa Maria alikuwa mchumba wake.
 
Akamuuliza pia walitarajia kuoana lini swali ambalo lilimshitua James na kutaka kujua mtu huyo alikuwa nani. Hatimaye Pascal aliondoka na kumuacha James akiwa na wasiwasi.
 
Jioni yake Pascal aliibukia nyumbani kwa Maria ambako alijirushia picha za Maria kutoka kwenye simu ya Maria. Picha hizo alimpelekea Dokta Kweka ili kumthibitishia kuwa Maria ana mchumba.
 
Dokta Kweka alipopata uhakika kwamba Maria alikuwa na mchumba na kwamba angeoana naye karibuni alimwambia Simon Puto.
 
“Nataka unifanyie kazi moja tu, nitakulipa kiasi chochote unachotaka”
“Kumbuka kwamba hii kazi ya awali uliyonipa nimeikamilisha”
 
“Ndiyo, hii imekamilika. Nataka kukupa kazi nyingine amabayo ni nzito kidogo”
 
“Kazi gani?”
 
“Nataka umuue Maria!”
 
“Kwanini?”
 
“Si juu yako kujua hilo kwa sasa na halina umuhimu na wewe. Kilicho muhimu kwako ni kuniambia unataka kiasi gani?”
 
Simon alipitisha muda kidogo kabla ya kumuuliza.
 
“Unataka nimuue kwa lini?”
 
“Ukiweza hata leo. Sitaki aishi. Si tu atanisononesha roho yangu bali pia amenitenda vibaya”
 
“Wewe unataka kunipa kiasi gani kwa kazi hiyo?”
 
“Sijui. Niambie wewe unataka kiasi gani?”
 
“Nipatie shilingi milioni tano”
 
“Nitakupa nusu yake, ukimuua Maria nakumalizia kiasi kilichobaki”
 
“Nipatie”
 
Dokta Kweka alifungua mkoba wake ambao wakati wote amekuwa akitembea nao. Alitoa burungutu la noti, akahesabu shilingi milioni mbili na laki tano akampa Simon.
“Umenipa kiasi gani?”
 
“Milioni mbili na nusu taslim, zihesabu”
 
“Sihitaji kuzihesabu. Kama wewe umehakikisha ni kiasi hicho inatosha”
 
Simon alizitia kwenye mifuko ya koti alilokuwa amevaa.
 
ITAENDELEA kesho hapahapa Usikose Uhondo huu.

No comments:

Post a Comment