Monday, June 22, 2015

SOMA HABARI KUBWA ZILIZOPEWA UZITO MAGAZETI YA LEO JUNE 22 TZ

Uchambuzi huu wa magazeti unaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha Elimu Cha Candle Education Centre Tanga. Kituo kinaongoza kufaulisha wanafunzi kidato cha pili hadi cha sita na wanaojiendeleza kielimu. Wapo Tanga mkabala na Bank ya CRDB simu 0715 772736

sabaaa
JamboLEO
Madereva wa kiume wa pikipiki maarufu kama bodaboda na wengine wanaotumia usafiri huo kwa muda mrefu wapo katika hatari ya kuwa wagumba.
Tafiti nyingine zilizofanywa zinazonyesha kuwa huenda wakakabiliwa na uhaba wa mbegu za kiume na hatimaye kushindwa kutoa mbegu za kiume zenye uwezo wa kutunga mimba.
Hali hiyo inatokana na sehemu za siri zinazozalisha mbegu muda mwingi kuwa katika hali ya joto kitu ambacho kitaalamu kimebainisha kuwa kinafanya mishipa ya damu kutofanya vyema na kuchochea uzalishaji mbegu hizo.
Maelfu ya vijana nchini wamejiajiri kupitia usafiri wa bodaboda huku wengi wakiwa katika umri mdogo wa kati ya miaka 18 hadi 50, kutokana na tafiti hizo huenda Tanzania ikaathirika zaidi kwa kuwa na vijana wengi wanaoweza kuwa wagumba.
Utafiti unaonyesha kuwa vijana wengi wanaokaa katika kiti cha pikipiki hupambana na joto kutokana na ngozi laini iliyopo katika korodani,mirija ya damu hushindwa kupitisha virutubisho kutokana na msuguano mkali uliopo.
MWANANCHI
Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema na watu wengine 24 juzi walijikuta wakiwekwa mikononi mwa polisi kwa saa nne kutokana na purukushani za uandikishaji wa wapigakura katika mfumo wa BVR.
Tukio hilo lilitokea juzi jioni kwenye kituo cha uandikishaji kituo cha Osunyai, Kata ya Sombetini ambako watu hao akiwamo mbunge walitiwa mbaroni.
Diwani wa Kata ya Sombetini, Ally Bananga alisema mbunge huyo na watu wengine walikamatwa huku wengine 13 wakijeruhiwa katika tukio hilo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema juzi kuwa tukio hilo alikuwa amelisikia juujuu lakini hakuwa amepata taarifa zaidi.
Mmoja wa washuhuda wa tukio hilo, Amiri Ally alisema juzi saa 12.20 jioni Lema alifika katika kituo hicho na kuuliza kinachoendelea na kuhamasisha waandikishaji kufanya haraka katika kuandikisha lakini walitokea vijana kadhaa waliodhaniwa ni wanachama wa CCM na kuanza kumzuia mbunge huyo asiingie ndani.
“Kila jioni Lema huwa anazungukia vituo kuangalia maendeleo lakini hakuna jambo linalotokea ila leo (juzi) kuna vijana ambao huwa tunawaona kwenye misafara ya CCM kama walinzi, walianza kumzuia Lema asiingie ndani, walianza kusukumana na wananchi nao waliingilia kati, ndio vurugu zikaanza,” alisema.
“Vurugu zilipopamba moto polisi walikuja na kuwakamata baadhi ya watu na kuondoka nao akiwamo Lema na watu wengine wakaanza kukimbia ovyo,”Amiri.
Mmoja wa watu waliojeruhiwa, Abduli Adam alisema baada ya kuona mbunge anasukumwa hovyo na vijana walioonekana kama ni kutoka kwa walinzi wa CCM aliingilia kati kutaka kumsaidia lakini alichomwa kisu cha kichwa na kuvuja damu nyingi.
“Mimi nilikuwa kwenye foleni nikashangaa kelele upande wa pili kuangalia nikamuona Mbunge Lema katikati, hivyo nikajitosa kumsaidia nikachomwa kisu cha kichwa sijui aliyenichoma na sasa niko njiani naelekea hospitali ya Mkoa Mount Meru kutibiwa,” alisema.
Wengine waliokamatwa ni pamoja na mwanasheria wa Chadema, mwenyekiti wa Mtaa wa Osunyai, viongozi mbalimbali wa chama na wananchi waliokuwa wanajiandikisha kituoni hapo.
Kukamatwa kwa watu hao kulisababisha shughuli ya uandikishaji kusitishwa kutokana na vurugu kuzuka kwenye kituo hicho saa 12 jioni badala ya saa 2:00 usiku kama ilivyopangwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.
Akizungumzia tukio hilo, Lema alisema, “Nimeshindwa kuelewa kukamatwa kwangu baada ya kutoa taarifa polisi, inawezekana vipi mlalamikaji akakamatwa na wahalifu wakawa huru.
MWANANCHI
Waziri Mkuu Mizengo Pinda amewashukuru wanachama waliojitokeza kumdhamini, huku akieleza kuwa anaondoka mkoani Iringa na msemo mpya; “Yeye anatosha na chenji inabaki.”
Pinda alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza na wanachama wa CCM waliofika kwenye ofisi za chama hicho kumdhamini.
Akiongoza wanachama hao wakati wa utambulisho wa watu waliohudhuria hafla hiyo, Katibu Mwenezi wa CCM Mkoa wa Iringa Dk Yahya Msigwa alisema: “CCM oyee, wanachama wakajibu oyeee, Pinda oyeee wanachama wakajibu oyeee. Pinda anatosha hatoshi? wanachama wakajibu anatosha, Dk Msigwa akaongeza: “Pinda anatosha na chenji inabaki.”
Katika shukrani zake, Pinda alisema: “Niwashukuru wanachama wa CCM mkoani hapa mliofika kunidhamini, lakini pia katika mkoa huu nimepata neno jipya na ninaondoka nalo. ‘Mimi natosha na chenji inabaki…sijui chenji inayobaki ndiyo nani.”
Katika hafla hiyo, Waziri Pinda aliitaka CCM kupitisha majina ya wagombea wa nafasi ya urais, ubunge na udiwani kwa kuzingatia matakwa ya wananchi ili kuepuka chama kupoteza nafasi kwa jamii.
Alionya kama chama kitapuuza matakwa wananchi, kinaweza kupata pigo kama ilivyotokea katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2010 katika Jimbo la Iringa na majimbo mengine kadhaa nchini.
“Mimi ni mlezi wa Mkoa wa Iringa kichama, nawaombeni wekeni masilahi ya chama mbele badala ya masilahi ya mtu binafsi na mnapokwenda kutafuta viongozi wa ngazi ya kata, jimbo na urais. Hakikisheni wagombea mnaowaleta ni wale wanaokubalika na jamii ya eneo husika,” Pinda.
Akiwa mjini Morogoro jana, Pinda alizungumzia kauli yake aliyotoa bungeni akilitaka Jeshi la Polisi kuwapiga wanaokiuka amri halali kuwa ilikuzwa sana na vyombo vya habari.
Pinda alisema, “Niwashukuru waandishi wa habari kwa kujitokeza kwa wingi kuliko mikoa yote niliyopita kuomba wadhamini lakini na nyinyi mkisikia jambo mnalikuza.”
Alitolea mfano kauli hiyo kisha akasema, “baadhi ya vituo vya redio vimefikia hatua ya kuitengeneza sauti ile kama naulizwa swali na kusikika nikitoa amri ya kumpiga mhusika aliyefanya kosa.”
Pinda alisema yeye ni muumini mkubwa wa kudumisha amani na utulivu.
NIPASHE
Baadhi ya wabunge wa Viti Maalum, wamelalamika kwamba wamekuwa wakidharauliwa na jamii kutokana na uteuzi wao.
Waliyatoa malalamiko hayo walipokuwa wakiingia kwenye semina ya uelewa wa mchakato wa uchaguzi mjini hapa jana.
Semina hiyo ipo chini ya uwezeshaji wabunge ambayo iliandaliwa na Bunge kwa ufadhili wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP).
Mbunge wa Viti Maalum (Cuf), Zahara Ali Hamad, alisema Katiba imetoa viti maalum kwa mkono mmoja, lakini imekataa kwa upande mwingine.
Alitoa mfano kwa sheria inayotaka waziri mkuu atokane na jimbo la uchaguzi wakati mawaziri wengine wanaweza kutokana na jimbo ama viti maalum.
Naye Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Taulida Nyimbo, alisema wanawake wa viti maalum wanadharauliwa na kutopendana.
“Siamini kuwa wanawake hatupendani, ukiweka mtu hauziki hawezi kupata hata kura za wanawake wenzake,” alisema.
Aidha, alisema viti maalum vimekuwa vikisumbua kwa sababu watu hawafahamu jinsi gani vinapatikana.
Mbunge wa Kilwa Kusini (CUF), Suleiman Bundara, alisema taabu kubwa ni wanawake wenyewe kutopendana.
Mwenyekiti wa semina hiyo, Anna Abdallah, alitaka vyama vikubwa vya siasa kuonyesha mfano kwa kuwapa wanawake vyeo katika vyama.
Hata hivyo, Mbunge wa Manyovu (CCM), Albert Ntabaliba, alisema ni vyema wanawake wakaanzisha vyama vyao vya siasa ili nafasi ya juu ziwe zao.
Sijaona wanawake walioanzisha vyama vya siasa na sheria inaruhusu kufanya hivyo. Waanzishe ili wachukue nafasi zote za juu,” alisema.
Akijibu hoja za wabunge hao, Mkurugenzi wa Utetezi wa Kituo cha Haki za Binadamu Nchini (LHRC), Harold Sungusia, alisema ili kuondoa dharau kwa viti maalum, mambo ya msingi ya kuyafanya ni kuweka utaratibu muafaka utakaowekwa katika sheria wa jinsi ya kuwapata wabunge.
“Pia majukumu ya wabunge yajulikane kisheria ili wawajibike katika eneo hilo walilopangiwa,” alisema.
Aidha, alitaka elimu itolewe kwa umma ili waelewe upatikanaji wa wabunge hao na majukumu yao.
NIPASHE
Umoja wa Madereva Tanzania (UMT), umesema umepanga kwenda bungeni kuonana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, pamoja na Wabunge kwa madai kuwa Kamati iliyoundwa na Waziri Mkuu inaonekana kushindwa kutatua madai yao ya muda mrefu dhidi ya waajiri wao.
Aidha wamesema kuwa katika kikao cha kamati hiyo kitakachokaa Juni 23, mwaka huu, wanataka kiwe cha mwisho na kupata majibu na kuwa kama Serikali haitatoa majibu yanayoridhisha, Ijumaa wiki hii watasimamisha usafiri nchi nzima ili mazungumzo yaendelee.
Wamefikia uamuzi huo  baada ya kikao cha Ijumaa iliyopita cha kamati hiyo kushindwa kutoa majibu huku wamiliki wa vyombo vya usafirishaji wakishindwa kuudhuria bila taarifa.
Katibu Mkuu wa UMT, Rashid Salehe, alisema Serikali na wamiliki wanawachezea mchezo mchafu, huku madereva wakiendelea kuteseka na kufanya kazi katika mazingira magumu bila mikataba wala bima za matibabu.
“Tumepanga kuwa madereva wote tutakodi basi kwenda bungeni Dodomaili kuonana na Waziri Mkuu pamoja na wabunge watusaidie kwani kila siku hii kamati inatuzungusha bila kuta majibu yanayoeleweka, hivyo in wazi wameshindwa kazi,” alisema.
Alisema kuwa awali  walitaka kikao cha Ijumaa iliyopita kuwa cha mwisho na kutoa majibu ya matatizo yao, lakini haikuwa hivyo kwani inaonekana wazi kuwa Serikali inawasikiliza wamiliki kuliko madereva.
MTANZANIA
Waziri mkuu wa zamani Edward Lowassa amesema hana wasiwasi wa kukatwa jina lake ndani ya vikao vya CCM vitakavyochuja majina ya makada wa chama hicho wanaoteuliwa kuwa wagombea Urais kwa kuwa na hakuna mgombea aliyefikia rekodi yake ya utendaji.
Lowassa aliwataka wanachama wake kutokuwa na wasiwasi wowote wa jina lake kukatwa na vikao vya chama.
“Nikitazama majina ya wagombea, hakuna anayenifikia rekodi yangu, nimeanza kazi mwaka 1977, sijafanya kazi nyingine zaidi ya CCM, Sasa leo anayekata jina langu anatoka wapi?, ngoja niulize anakata kwa sababu gani? sioni kosa la kukatwa jina langu na Watanzanai hawaoni, kwa hiyo msiwe na wasiwasi” Lowassa.
Lowassa alisema anapata ujasiri kwa sababu kuna Watanzania wengi wanamuunga mkono na kwamba CCM itatenda haki katika uteuzi wa majina.
HABARILEO
Ofisi ya Taifa ya Takwimu imetoa makadirio ya idadi ya watu wanaotarajiwa kupiga kura katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 2015 ambao wanakisiwa kuwa watafikia milioni 24.2 nchi nzima.
Taarifa hizo ni makadirio ya idadi ya watu wanaostahili kupiga kura katika majimbo ya uchaguzi Tanzania kwa mwaka 2015.
Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, idadi ya wapigakura waliojiandikisha ilikuwa 20,137,303, lakini waliopiga kura Oktoba 31 mwaka huo walikuwa 8,626,283 sawa na asilimia 42.84 ya wapiga kura wote waliojiandikisha.
Takwimu hizi zimetolewa katika ngazi ya Mkoa, Wilaya, Jimbo la Uchaguzi na Kata au Shehia kama yalivyokuwa mwaka 2010. Makadirio ya idadi ya wapigakura yametokana na Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2012.
Kwa mujibu wa ripoti iliyo kwenye kitabu maalumu cha takwimu za wapiga kura mwaka huu, ambayo nakala yake imepatikana kupitia Ofisi ya Takwimu ya Mkoa wa Arusha, idadi hiyo imepatikana kwa kutumia mbinu za kidemografia zinazohusisha mabadiliko katika viwango vya uzazi, vifo, uhamaji na uhamiaji katika ngazi ya Taifa, Mkoa, Wilaya, Majimbo ya Uchaguzi na Kata au Shehia husika.
Inakadiriwa kuwa ifikapo siku ya uchaguzi, Tanzania itakuwa na watu wapatao 48,522,229 ambapo watakaokuwa na umri wa kupiga kura watakuwa ni watu 24,252,927 iwapo wote watafanikiwa kuandikishwa upya.
Mkoa wa Dar es Salaam wenye majimbo nane unatarajiwa kuwa na wapiga kura wengi zaidi watakaofikia milioni 3, ukifuatiwa na Mbeya itakayokuwa na wapiga kura milioni 1.5, Mwanza milioni 1.4 na Morogoro itakayokuwa na wapigakura milioni 1.3 katika nafasi ya nne.
Mikoa mingine inayotarajiwa kuwa na wapiga kura wengi ni pamoja na Kagera itakayokuwa na wapigakura milioni 1.2, Tabora inayokadiriwa kuwa na idadi ya wapiga kura milioni 1.1, Tanga nayo kwa idadi kama hiyo ya milioni 1.1 pamoja na Dodoma itakayokuwa na wastani wa wapigakura milioni moja.
Maandalizi ya kitabu cha idadi tarajiwa ya wapigakura yameshirikisha maofisa kutoka Wizara, Idara na Taasisi za Serikali ikiwemo Ofisi ya Taifa ya Takwimu na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali Zanzibar, pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Tume ya Uchaguzi Zanzibar na Chuo cha Takwimu Mashariki mwa Afrika (EASTC).
Kwa habari, matukio na michezo ni hapa hapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment