Monday, June 29, 2015

SOMA HABARI KUBWA ZILIZOPEWA UZITO MAGAZETI YA LEO JUNE 29 TZ

Uchambuzi huu wa magazeti unaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha elimu cha Candle Education Centre Tanga. Kituo kinaongozakufaulisha wanafunzi kidato cha pili hadi cha sita na wanaojiendeleza kielimu. Kituo kiko na Hostel pamoja na kutoa kozi ya Kiingereza na Computer. Wapo Tanga mkabala na Bank ya CRDB simu 0715 772746

TREEE (1)
MWANANCHI
Harusi ya mshambuliaji wa Simba, Mganda Emmanuel Okwi imeacha historia nchini Uganda akitumia dola 80,000 ( Sh 160,000 Mil ) kwa ajiri ya kuifanikisha iliyofanyika Jumamosi jijini Kampala.
Kiasi hicho kinatosha kabisa kukamilisha usajili wa timu zisizopungua tatu za Ligi Kuu Bara, lakini yeye alitumia fedha hizo kwa ajili ya sherehe, huku Gazeti hili lilikuwa Uganda na kushuhudia kila kitu kilivyokuwa kinaendelea wakati Okwi akimuoa Florence Nakalega.
Mshambuliaji wa zamani wa Yanga, Hamis Kiiza na Nabisubi Julian ndiyo walikuwa wasimamizi wao wa harusi hiyo, ilifungwa katika kanisa la Miracle Centre Cathedral lililopo Lubaga, Kampala.
Baada ya hapo shughuli ya kupiga picha za ukumbusho kwa maharusi, ilifanyika katika hoteli kubwa ya kifahali ya Munyonyo Lesort Beach na kumaliziwa na sherehe kamili kwenye Ukumbi wa Main Exbition Hall uliopo ndani ya jengo la UMA maeneo ya Lugogo.
Okwi alitumia magari saba yalikuwa maalumu kuwabeba maharusi, kati ya hayo matano ni aina ya Jaguar na mawili Brevis.
Hata hivyo, msafara wa harusi hiyo ulipata matatizo baada ya magari mawili yaliyowabeba wasimamizi akiwemo Hamis Kiiza kupata ajali, lakini hakuna aliyeumia zaidi ya mishtuko ya kawaida.
Maharusi wabadili nguo mara mbili
Hapa ndipo kulikuwa na utamu kamili, maharusi waliingia ukumbini majira ya saa 11 jioni, mwanaume walivaa suti za bluu na mwanamke gauni na shela nyeupe kabla ya kwenda kubalisha na kuvaa suti za kaki kwa wanaume na bibi harusi alivaa gauni lenye rangi ya kijivu.
Okwi alipokelewa na wachezaji wenzake waliokuwa wameshika mipira kwa juu yeye akapita katikati yao huku wakicheza na baada ya hapo walikabidhiwa mpira na makocha Sam Simbwa na Moses Basena.
Katika hali isiyo ya kawaida, Okwi alijikuta akidondosha chozi alipokuwa anazungumzia wasifu wa mkewe, Florence na alilia baada ya kuona chozi la mkewe ambaye ndiye alianza kuelezea wasifu wa mumewe.
Okwi alipoulizwa alisema: “Nililia kutokana na furaha kwani tumepita katika mazingira ya kila namna, magumu na raha.
“Nimefurahi sana kukamilisha shughuli hii na sasa nina mke ambaye tutatengeneza familia moja na atakuwa mshauri wangu,”  Okwi.
MWANANCHI
Zikiwa zimesalia siku nne, kabla ya kumalizika kwa uchukuaji na urudishaji fomu za kuwania urais CCM, kada wa chama hicho Banda Sonoko (46) amechukua fomu akijigamba kwamba yeye ni greda linalokuja kusawazisha nchi.
Wagombea wote wanatakiwa kumaliza michakato yao ndani ya wiki hii na hadi kufikia Ijumaa, kila mmoja awe amewasilisha vielelezo vyake ikiwamo majina ya wadhamini 450 kutoka mikoa 15, kati ya hiyo mitatu ya Zanzibar kupisha vikao vya kujadili na kuchuja wagombea vitakavyofanyika kuanzia mwishoni mwa wiki ijayo.
Sonoko ambaye anakuwa kada wa 42 wa CCM kuchukua fomu alisema ameamua kufanya hivyo kwa sababu anazo sifa, vigezo na uwezo kwamba ndiye anayeweza kuvaa viatu vya Mwalimu Julius Nyerere… “na hivi viatu sina haja ya kuvifuata Mwitongo (Kijiji alichozaliwa Mwalimu), hivi viatu anavyo mchezaji mmoja, aliwahi kucheza aliwahi kucheza nchini hapa. Huyo mchezaji alipocheza alifunga magoli mengi sana na kama Taifa, tukafaidika.
Hivi viatu havijakwenda Mwitongo, sihitaji kwenda Butiama, anavyo mtu fulani ni kiasi tu cha kwenda na kumwambia naomba viatu hivi nivivae. Kilicho kizuri ni kwamba navifahamu mpaka na namba na alama zake. Kiatu cha kulia cha Mwalimu Nyerere kina alama mbili ya kwanza ni nchi kujiendesha kwa kodi zetu. Kodi hizi zitathiminiwe, zidaiwe kwa muda na hilo liwe jambo la msingi, misaada iwe suala la mjadala,” alisema.
Alisema nchi ina raslimali nyingi za kutosha na kinachotakiwa ni usimamizi katika eneo hilo.
Alisema CCM imefanya mambo makubwa katika uongozi wake ikiwamo kutengeneza miundombinu ya kutosha na sasa kinachotakiwa kuisawazisha… “Miji yetu imeshakaa vizuri sasa nchi yetu inahitaji greda liweze kusawazisha… na greda ni mimi, nitaweza kusawazisha matatizo yaliyobaki na kuweza kuhakikisha lindi la umaskini linaondolewa.”
Sonoko alisema rais anayehitajika kwa wakati huu ni yule anayejali muda na kuwa na uamuzi, mambo ambayo yote anayo.
Alisema kaulimbiu yake ni kutokomeza umaskini na kwamba anaamini katika usimamizi jambo hilo mkazo endapo atafanikiwa kuwa rais.
Vipaumbele vingine ni kufufua uchumi wa viwanda, kuwekeza katika uchumi wa kilimo na kwamba tangu alipoondoka, Mwalimu Nyerere hakuna kiongozi ambaye amekuwa tayari kuimba wimbo wa kuboresha kilimo.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, amesema CCM na Serikali yake, haviwezi kutishwa na mtu yeyote katika kutekeleza uamuzi wowote kutokana na kuwa na historia, msimamo usioyumba na uongozi thabiti.
Membe aliwataka Watanzania wakatae vitisho na ulaghai kutoka kwa mtu yeyote katika maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
MWANANCHI
Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe amesema kama angekuwa ni msaliti na kibaraka wa Chama cha Mapinduzi (CCM), asingeweza kuongoza mapambano ya kuwang’oa mawaziri 13 kwa miaka mitatu katika Serikali ya Rais Jakaya Kikwete.
Aliyasema hayo jana alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Mabawa uliolenga kukitangaza rasmi chama chake kwa wakazi wa Mkoa wa Tanga na vitongoji vyake.
Zitto alisema mwaka 2012 aliongoza mapambano ya kuwang’oa mawaziri wanane wakati mwaka 2013 walijiuzulu mawaziri wanne kwa kashfa ya Oparesheni Tokomeza, wakati mwaka jana, mawaziri watatu na Mwanasheria Mkuu wa Serikali walilazimika kuachia ngazi kutokana na kashfa ya Akaunti ya Tegeta escrow.
“Wananchi wa Tanga jiulizeni, hivi msaliti anawezaje kuwang’oa mawaziri wote hao ndani ya kipindi cha miaka mitatu?” alihoji Zitto na kusisitiza kuwa kuna watu wamelenga kutumia hoja hiyo kwa lengo la kumchafua.
Zitto alisema ni kutokana na kunyanyaswa na kuonewa na viongozi wa ngazi ya juu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), hivyo aliona njia mbadala ni kutafuta jukwaa lingine la siasa ili aweze kuwatumikia Watanzania.
“Kuanzisha chama kipya siyo kazi nyepesi, lakini kwa sababu tulikuwa na dhamira ya dhati tumeweza kufyeka mapori na sasa tumefanikiwa na leo hii tunakileta kwenu ili mkipokee kwa sababu ACT ni yenu,” Zitto.
Alisema chama hicho kina mpango wa kuhamasisha ufufuaji wa zao la mkonge mkoani hapa ili lilimwe na wakulima wadogo badala ya wakubwa kwa sababu katika nchi zilizofanikiwa kuleta mapinduzi ya mkonge zimesaidiwa na wakulima wadogo.
Alisema kupitia ACT atahakikisha hoja yake aliyoiwasilisha bungeni na kupingwa na wabunge wa majimbo ya Mkoa wa Tanga ya kulifufua zao la mkonge inatekelezwa.
Mjumbe wa ACT, Seleman Msindi maarufu ‘Afande Sele’ alisema hajajiunga na ACT – Wazalendo kwa sababu ya urafiki wake na Zitto, bali amebaini kuwa ndiyo chama chenye mlengo makini wa kuipeleka nchi kunakostahili mara kitakapofanikiwa kushika dola.
HABARILEO
Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa ambaye anawania kuchaguliwa kuwania nafasi ya urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) amemwagia sifa Rais, Dk Jakaya Kikwete kwa kuliongoza Taifa vizuri huku likiwa bado na amani na utulivu mkubwa wakati akielekea kumaliza muda wake wa kuliongoza Taifa kwa vipindi viwili.
Aliyasema hayo jana mjini Kibaha wakati wa kuomba wanachama wa CCM mkoani Pwani wamdhamini ikiwa ni taratibu kwa wanachama wanaowania Urais kupitia chama hicho kudhaminiwa.
Lowassa alisema kuwa anampongeza Rais Kikwete kwa kuongoza nchi vyema na kuendeleza sifa ya nchi ya Tanzania kuwa na amani ambayo baadhi ya nchi zimeifanya kama mfano wa kuigwa kwa utawala bora.
“Rais Dk Kikwete kafanya kazi kubwa ya kupongezwa kwani anaicha nchi ikiwa kwenye hali nzuri kwa umoja na mshikamano mkubwa,” Lowassa.
Aidha alisema kuwa mkoa wa Pwani ndipo Rais Dk Kikwete alipoanzia safari yake ya kuwa Rais na yeye anaamini Mungu akimjalia atapata nafasi hiyo.
Alisema kuwa endapo atachaguliwa atahakikisha matatizo ya hospitali ya Tumbi anayatatua ndani ya mwaka mmoja pamoja na changamoto za miundombinu na barabara Naye Mwenyekiti wa CCM Kibaha Mjini Maulid Bundala alisema kuwa anaomba vikao vinavyohusika vimpitishe ili aweze kuwania nafasi hiyo na wasiangalie mtu bali waangalie maslahi ya chama.
Jumla ya wanachama wa CCM mkoa wa Pwani wapatao 78,500 walimdhamini kwenye nafasi hiyo kutoka wilaya sita za mkoa huo ikiwa ni pamoja na Kibaha Mjini 25,500, Bagamoyo 16,000, Mkuranga 11,200, Kibaha Vijijini 10,200, Rufiji 7,800 na Kisarawe 7,000.
HABARILEO
Zaidi ya wahamiaji haramu 50 wanaoishi katika kijiji cha Tamau wilayani Bunda, mkoani Mara, akiwemo mwenyekiti wa kijiji hicho wamezuiwa kujiandikisha kwenye daftari hilo.
Ofisa uhamiaji wa Mkoa wa Mara, Ally Dady jana amethibitisha kuzuiwa kwa watu hao wanaodaiwa kuwa ni raia wa nchi jirani Kenya. Dady alisema taratibu za kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria watuhumiwa hao zinafanyika na kuongeza kuwa baadhi yao, wapo ambao walikamatwa wakiwa tayari wamekwishajiandikisha katika daftari hilo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, waliobainika kuwa ni wahamiaji haramu ni pamoja na mwenyekiti wa kijiji hicho, John Seda, ambaye anatafutwa baada ya kutoroka.
Aidha, ilielezwa kuwa wale ambao tayari walikuwa wamekwishajiandikisha katika daftari hilo, wameamriwa kurudisha vitambulisho hivyo kwa ofisa mtendaji wa kijiji na wa kata hiyo ya Kunzugu.
Ilidaiwa kuwa tayari watu hao wamepewa fomu maalumu ya kujieleza na ofisi ya uhamiaji wilayani hapa, ambapo vyanzo vya habari vinasema kuwa wahamiaji hao wamo askari polisi kutoka nchini Kenya ambao wanaishi kijijini hapo kinyume cha sheria.
Aidha, vyanzo hivyo vya habari vimedai kuwa watu hao wanaishi kijijini hapo kinyemela na kwamba mwenyekiti huyo aliyechaguliwa katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliopita alitumia mbinu nyingi ya kupata uongozi huo ikiwa ni pamoja na kutoa rushwa.
Pia vyanzo hivyo vinasema kuishi kijijini hapo kwa wahamiaji hao kwa kipindi chote hicho ni kutokana na viongozi wa serikali kuwahalalisha watu hao kuishi hapo baada ya kupewa kitu kidogo, yaani pesa, mbuzi na ng’ombe.
Hata hivyo, Kaimu Ofisa Mtendaji Bernard Methew alipotafutwa na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu, alisema kuwa hana taarifa yoyote juu ya jambo hilo na wala hakuna wahamiaji haramu kijijni hapo.
“Hizo habari umezipata wapi wewe, mbona mimi sijui….. kama ni uhamiaji nenda uwaulize huko huko” alisema Ofisa mtendaji huyo na kukata simu.
Gazeti hili lilimtafuta msimamizi msaidizi wa uchaguzi katika Wilaya ya Bunda, ambaye pia ni mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo Lucy Msoffe, ambaye alisema kuwa hana taarifa zozote kuhusu wahamiaji hao haramu.
Aidha, Lucy aliahidi kufuatilia zaidi suala hilo, ambapo baadaye alipiga simu na kusema kuwa ni kweli wahamiaji haramu zaidi ya hamsini wamezuiwa kujiandikisha katika daftari hilo kijijini hapo na kwamba taratibu za kisheria zinafanywa na watu wa uhamiaji.
Hivi karibuni wahamiaji haramu watatu walikamatwa wakiwa wamejiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura, huku baadhi yao wakiwa wamejiandikisha zaidi ya mara moja katika vituo tofauti wilayani hapa.
Wakati huo huo, Ofisa uhamiaji huyo wa Mkoa wa Mara, alisema kuwa wahamiaji haramu wengi wako katika vijiji vya Nyaburundu, Karukekere na Tamau, katika Wilaya ya Bunda, na katika vijiji vya Bugwema na Masinono katika Wilaya ya Butiama, katika halmashauri ya wilaya ya Musoma vijijini.
HABARILEO
Taasisi ya Utafiti wa Maendeleo ya Elimu Tanzania (TEDRO) imetoa matokeo ya utafiti kuhusu wagombea ambao hotuba zao ziligusa mahitaji wa wananchi kuwa Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba ndiye aliyeibuka kidedea.
Mkurugenzi wa TEDRO, Jacob Kateri alisema lengo la utafiti huo ilikuwa kujua ni kwa kiasi gani Watanzania wanafuatilia mchakato mzima wa kuelekea uchaguzi mkuu, hususani kipindi hiki cha watu kutangaza nia na kutambua mchango wa vyombo vya habari kufikisha elimu ya uraia kwa umma tunapoelekea uchaguzi mkuu.
Alisema utafiti huo umefanywa katika za Njombe Mjini na Vijijini, Mbeya Mjini, Rombo, Arumeru, Kinondoni, Kilombero na Kibaha vijijini. Wakati wilaya walizohojiwa kwa simu ni zingine zilizosalia kwa kuzingatia kwamba kumbukumbu za wahojiwa za simu zinapatikana katika ofisi yetu.
Mkurugenzi huyo alisema uchambuzi wa kujua nani anayewafaa wananchi kupitia vipaumbele vilivyoainishwa na watangaza nia, kutathmini hotuba iliyo bora kwa kuzingatia yaliyomo na mahitaji ya Watanzania na nini yaweza kuwa agenda ya msingi tunapotarajia kumpata Rais wa awamu ya tano.
Alisema katika sehemu ya uadilifu usiotiliwa shaka, matokeo yanaonesha kuwa Naibu Waziri wa Fedha Mwigulu Nchemba anaongoza kwa kupata asilimia 15. Aliyefuata ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe 13 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Kazi Maalumu, Mark Mwandosya 13.
Waziri Mkuu Mizengo Pinda asilimia nane, Naibu Waziri Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba nane, Jaji Mkuu Mstaafu, Augustino Ramadhani saba, Waziri Mkuu wa aliyejiuzulu, Edward Lowasa 10, Makongoro Nyerere tano na waliosema hakuna msafi ni wananchi 12.
Pia kuhusu kipengele cha hotuba bora Mwigulu aliongoza kwa kupata alama A, akifuatiwa na Januari, Wasira, Profesa Mwandosya, Profesa Muhongo , Wasira na Membe walifungana kwa kupata alama B+, Lowasa, Mbunge wa Sengerena William Ngeleja walifungana kwa kupata alaba B.
“Tathmini ya hotuba imezingatia utulivu katika uwasilishaji, mkusanyiko wa mambo yanayohusu wananchi wa makundi yote ya jamii katika hotuba, uwezo wa kujibu maswali na ufafanuzi wa mambo mtambuka ya kiuchumi ikiwamo kushuka kwa thamani ya shilingi, na njia za utatuzi kwa nchi kama Tanzania,” alisema.
Kuhusu kipengele cha mtangaza nia wenye uwezo wa kupambana na vita ya rushwa na kuboresha utawala bora, matokeo yalionesha kuwa Mwigulu anaongoza asilimia 17, Dk Magufuli 14, Membe 11, Lowasa 6.10, Jaji Ramadhani sita.
Profesa Mwandosya, Pinda na Mwakyembe walifungana kwa kupata asilimia nane, Januari saba, Waziri wa Uchukuzi Samuel Sitta sita, Kigwangala tatu, na wengine nne.
NIPASHE
Mtoto wa Rais Jakaya Kikwete anayesoma shule ya kimataifa ya Feza, Khalfan Jakaya Kikwete ameiwakilisha vema Tanzania katika shindano la kusaka wanafunzi wenye akili nyingi ‘Genius Olympiad’ lililofanyika Oswego, Marekani mwaka huu.
Shindano hilo huandaliwa na Idara ya Sayansi na Elimu ya Chuo Kikuu cha New York likishirikisha shule za kimataifa duniani likihusisha kazi za masuala ya sayansi, sanaa, biashara na mazingira.
 Kwa mujibu wa mtandao wa www.geniusolympiad.org, mwaka huu nchi 69 zilishiriki kwa kupeleka kazi 1,171. Kazi 401 zilikidhi vigezo na kupokewa. Shule za kimataifa za Feza ziliwasilisha kazi nne na kushinda medali moja ya dhahabu na tatu za shaba.
 Kazi iliyoshinda medali ya dhahabu iliitwa ‘Vcardin’ iliyoandaliwa na kuwasilishwa na Khalfan na Seif Yahya Mhata ambao wote ni wanafunzi wa shule za Feza.
 Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita, Khalfan alisema kazi yao imelenga kurahisisha mawasiliano ya kimataifa kwa kuwa na njia ya uhakika ya kuwasiliana.
“Mradi huu unahusu kubadilishana kadi za mawasiliano kwa njia ya mtandao. Ni muhimu sana kwa mawasiliano hasa ya wafanya biashara, lakini inahitaji uwe na simu ya kisasa yenye intaneti au kifaa kingine chenye intaneti,” alisema Khalfan aliyekuwa amefuatana na Mhata.
Kazi nyingine kutoka Feza zilizoshinda medali za shaba ni ‘The Fault of Humanity’ iliyoandaliwa na Prince Mwemezi ambaye alipiga picha ya moto ukiunguza miti eneo la Tanganyika Packers, Kawe jijini Dar es Salaam na kuonyesha athari za mazingira zitokanazo na uchomaji misitu.
Medali nyingine ya shaba imeletwa katika shule ya Feza na wanafunzi wawili Goodluck Komba na Sajjad El-Amin ambao walianza kazi inayoonyesha namna mkaa unavyoweza kupatikana kupitia karatasi na takataka badala ya kukata miti.
 Veronica Ndomba, mhitimu wa kidato cha sita mwaka huu katika shule ya Feza Girls, aliandaa kazi ya kuzuia uchafuzi wa mazingira ya bahari kwa kuelimisha watu kuhusu kutotupa taka, mafuta na uvuvi haramu baharini na kushinda medali ya tatu ya shaba.
NIPASHE
Rais Jakaya Kikwete ameomba radhi kwa Watanzania aliowakosea wakati wa utumishi wake wa miaka kumi Ikulu huku akisisitiza hakuna binadamu aliyemkamilifu.
Aliyasema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita, wakati akizungumza kwenye sherehe ya kuadhimisha miaka miwili ya Upapa wa Baba Mtakatifu Francis iliyofanyika nyumbani kwa Balozi wa Vatican nchini, Oysterbay jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali.
 Rais Kikwete alitumia pia nafasi hiyo kuwaaga viongozi hao wakuu wa Kanisa Katoliki akiwasisitizia kuwa anaacha nyuma nchi yenye amani na utulivu  huku akiwataka viongozi hao kufanyakazi vizuri na kiongozi mpya na kudumisha amani na utulivu wa kijamii kama walivyofanya kwake.
Alisema anaamini kuwa hakuna asiyekosea katika maisha kwani yeye alijaribu alivyoweza na kwa kadri ya uwezo wake lakini inawezekana kukawa na watu ambao aliwakosea hivyo wamsamehe na waelewe ukomo wa uwezo wa binadamu.
“Napenda pia kusisitiza kuwa hakuna binadamu aliyekamilifu na kwa wale ambao niliwakosea  naomba waelewe ukomo wa uwezo wa binadamu naacha nyuma nchi yenye amani na utulivu, nchi ambayo inapitia katika kipindi cha ustawi wa kiuchumi na kijamii ambao haujapata kutokea katika historia ya Tanzania,” alisema na kuongeza kuwa:
“Nina hakika kuwa mrithi wangu ataendeleza kazi nzuri ambayo nimeifanya katika miaka 10 iliyopita hasa ile ya kujenga na kuimarisha uhusiano kati ya Dola na Kanisa.”
Aidha, aliwaomba viongozi wa dini nchini kusaidia kuendeleza jadi nzuri ya Tanzania kwa kuhakikisha   nchi inabaki na amani, kabla, wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu, 2015.
Alilishukuru Kanisa Katoliki nchini kwa kuendeleza ushirikiano wake na serikali wa kutoa huduma za jamii katika maendeleo mbali mbali likiwamo la elimu na afya.
Kikwete pia alisema kuwa kwa sababu Dola na Kanisa ni taasisi zinazoendeshwa na binadamu, inatokea wakati mwingine uhusiano kati ya taasisi hizo mbili ukapitia katika mawimbi lakini ni uhusiano unaoendelea kuwapo na kuimarishwa.
Wengine waliohudhuria sherehe hiyo iliyoandaliwa na Balozi Askofu Mkuu Francisco Padalli, ni  Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Katoliki  Dar es Salaam,  Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo na maskofu wa karibu majimbo yote ya kanisa hilo nchini.
“Kila miaka mitano, Tanzania hupiga kura kupata ridhaa ya wananchi ya kuongoza. Makabidhiano ya madaraka katika Tanzania limekuwa suala la amani na tunabakia mfano wenye kung’ara katika Afrika kwa kuruhusu makabidhiano ya amani,” alisema.
“Kwa utaratibu huu mzuri, nitamaliza muda wangu wa uongozi na kukabidhi madaraka kwa rais mpya. Naamini kuwa Kanisa Katoliki litasaidia sana kuhakikisha mchakato wetu wa uchaguzi na makabidhiano ya uongozi vinakuwa  vya amani.”
 Kuhusu miaka miwili ya uongozi wa Papa Francis,  Kikwete, alisema kiongozi huyo ameleta matumaini mapya duniani, ujumbe mpya wa amani, heshima kwa utawala wa sheria amani na utulivu.
“Ujumbe wake kuhusu changamoto nyingi duniani, likiwamo lile la tabianchi, umeongeza sauti yenye nguvu sana kwa namna dunia yetu inavyoendeshwa.”
NIPASHE
Hatimaye kile kikao cha Baraza la Ushauri la Wazee wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinachowahusisha pia marais wastaafu Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa, kinatarajiwa kufanyika wakati wowote wiki hii kujadili mwenendo wa mchakato wa kumpata mgombea urais wa Tanzania kupitia chama hicho.
Taarifa kutoka chanzo kimoja ndani ya CCM kimeeleza kuwa Mwinyi, Mkapa na wazee wengine wanaounda Baraza la Wazee la Ushauri, watapasua kichwa wiki hii kujadili mwenendo wa urais ikiwa ni siku chache kabla ya kufikia Julai 2, mwaka huu, inayoonyeshwa katika ratiba ya uchaguzi ya CCM kuwa ndiyo siku ya mwisho ya kurejesha fomu kwa wanaowania urais.
Lengo la kikao cha Wazee ni kujadili kwa kina mwenendo wa mchakato wa kumpata mgombea urais na mwishowe kutoa mapendekezo yao juu ya namna bora ya kumpata mgombea kwa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM (CC)
“Kikao hiki ni muhimu kwa hatma ya mchakato wa uchaguzi… baada ya kutofanyika wiki iliyopita, sasa kitafanyika wiki hii, tena wakati wowote kuanzia kesho (leo),” chanzo kilieleza.
Awali, kikao hicho kilitarajiwa kufanyika Jumatano iliyopita jijini Dar es Salaam lakini kikaahirishwa na Katibu wa Baraza la Ushauri la Wazee, Pius Msekwa, kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni baadhi ya viongozi wakuu wa CCM kuwa safarini.
Kikao cha Baraza la Ushauri la Wazee ni mahususi kwa ajili ya ushauri juu ya watia nia 42 wa urais waliojitokeza kutaka kuteuliwa na CCM kupeperusha bendera yake katika Uchaguzi Mkuu wa Rais, wabunge na madiwani utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu.
Wanaounda Baraza la Ushauri la Wazee kwa mujibu wa mabadiliko yaliyofanywa na CCM mwaka 2012 katika katiba yake ni marais wastaafu Mwinyi (Mwenyekiti), Mkapa (Mjumbe), Amani Abeid Karume (Mjumbe) na Dk. Salmin Amour (Mjumbe).
Wengine ni Waziri Mkuu mstaafu na Makamu wa Kwanza wa Rais, John Malecela (mjumbe) na Pius Msekwa (Katibu).
Mkutano huo wa Baraza la Wazee CCM ni utangulizi wa mfululizo wa vikao vingine vya chama hicho vitakavyoanza Julai 5, mwaka huu.
Vikao vingine ambavyo viko katika maandalizi ya kukutana ni Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa itakayokutana Julai 7 na Kamati Kuu (CC) itakayokutana Julai 8, chini ya Rais Kikwete, ikifuatiwa na kikao cha NEC Julai 9, mwaka huu.
Jina la mgombea urais atakayepeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu litajulikana Julai 12 baada ya kupigiwa kura na Mkutano Mkuu wa Taifa wa CCM, ambao ni maalum kwa ajili kuchagua jina la mgombea mmoja kati ya watatu.
Hatimaye kile kikao cha Baraza la Ushauri la Wazee wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinachowahusisha pia marais wastaafu Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa, kinatarajiwa kufanyika wakati wowote wiki hii kujadili mwenendo wa mchakato wa kumpata mgombea urais wa Tanzania kupitia chama hicho.
Kwa habari, matukio na michezo ni hapa hapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment