Thursday, June 25, 2015

SOMA MAKUBWA YALIYOANDIKWA MAGAZETINI LEO, JUNE 25 TZ

Uchambuzi huu wa magazeti unaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha Elimu Cha Candle Education Centre Tanga. Kituo kinaongoza kufaulisha wanafunzi kidato cha pili hadi cha sita na wanaojiendeleza kielimu. Kituo kinatoa kozi ya Kiingereza na Computer na kutoa Cheti. Wapo Tanga mkabala na Bank ya CRDB simu, 0715 772746


HEAD

TANZANIA DAIMA
Mtoto anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka mitano hadi sita ameuwa kikatili jijini Dar es salaam baada ya kubakwa na kasha kunyongwa shingo huku akidaiw akunyofolewa sehemu za siri.
Mwili wa mototo huyo unadaiwa kutelekezwa katika moja ya nyumba iliyokuwa haijaisha na kugunduliwa na kijana aliyekuwa akiokota chupa tupu za maji eneo la tabata kisiwani, Dar es salaam.
Baadhi ya mashuhuda walisema  walilaani tukio hilona kusema na ukatili  huo ni wa kwanza kutokeo mtaani hapo.
“Sisi tupo jirani na yumba hii na hatujasikia kelele zozote na ndio maana tunasema tukio hili halikufanyika hapa” walisema baadhi ya mashuhuda.
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa huo Christopher Victory alikiri ytokea kwa tukio hilo na ofisi yake ilipokea taarifa hizo juzi na kulazimika kytoa taarifa kituo cha Polisi cha Tabata.
Kamanda wa Polisi Ilala Lukas Mkondya alisema taarifa ya unyama huo itawekwa wazi leo baada ya kupokea ripoti ya daktari.
MWANANCHI
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeifuta kesi ya mauaji ya kukusudia iliyokuwa ikimkabili mfanyabiashara Marijan Abubakar, maarufu kama Papa Msofe na mwenzake, Makongoro Joseph.
Hakimu Mkazi, Renatus Rutta aliifuta kesi hiyo chini ya kifungu cha 91 (1) cha sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai.
Aliifuta baada ya Wakili wa Serikali Wankyo Simon, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini ( DPP) kuonyesha kuwa hana nia ya kuendeleza mashtaka dhidi yao.
Msofe na Makongoro wamesota rumande kwa takriban mwaka mmoja sasa kutokana na kile kinachelezwa ni upelelezi kusubiriwa ukamilike.
Msofe kwa mara ya kwanza alifikishwa kortini Agosti 2012.
Hata hivyo baada ya kuachiwa huru Makongoro aliruhusiwa huku Msofe akifunguliwa kesi nyingine ya kughushi.
Katika kesi hiyo mpya, Msofe anadaiwa kuwa Desemba 23, 2004 katika Wilaya ya Ilala kwa nia ya kudanganya alighushi nyaraka ya kuhamisha haki ya umiliki wa nyumba namba 288 ambayo ni mali ya mfanyabiashara wa madini Onesphory Kituli (kwa sasa marehemu).
Ilidaiwa kuwa Msofe kwa nia ya kudanganya alighushi nyaraka hiyo akionyesha Desemba 13,2004, Kituli alihamisha haki yake ya umiliki wa nyumba hiyo kwake wakati akijua ni uongo.
Mbali na shtaka hilo, Msofe anadaiwa kuwa kati ya Desemba 23,2004 na Machi 30, 2005 akiwa na nia ya kidanganya alitoa nyaraka hizo za uongo kwa Kamishna wa Ardhi kwa lengo la kuhamisha umiliki kutoka kwa Kituli kwenda kwake.
Upande wa mashtaka ulidai mahakamani hapo kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.
Kesi imeahirishwa hadi Julai 9, 2015 na ametakiwa kuwa na wadhamini wawili ambao kila mmoja atasaini bondi ya Sh 10 milioni.
MWANANCHI
Baraza la Taifa la Elimu la Ufundi (NACTE) limefuta usajili wa vyuo vitatu na kuvishusha hadhi vingine 16 kutokana na kukiuka masharti ya usajili.
Vyuo vilivyofutiwa usajili ni Dar es Salaam College of Clinical Medicine, Ndatele School of Medical Laboratory Sciences, vinavyohusika na elimu ya tiba, na Institute for Information Technology kinachofundisha elimu ya teknolojia ya habari na mawasiliano (Teknohama).
Akitangaza uamuzi huo jijini hapa jana, kaimu katibu mtendaji wa Nacte, Dk Adolf Rutayuga alisema vyuo hivyo vimeshindwa kurekebisha kasoro ambazo baraza hilo lilizibaini na kuvitaka kufanya marekebisho.
Alisema baraza hilo lilitoa notisi ya siku 30 likivitaka vyuo vyenye upungufu katika usajili na ithibati kutoa maelezo na kufanya marekebisho.
Kaimu mkurugenzi huyo alisema baadhi ya vyuo vilifanya marekebisho kama vilivyoogizwa.
Alitaja makosa yaliyokiukwa kuwa ni kumalizika kwa muda wa usajili, kutoanza mchakato wa kupata uthibitisho wa kufikia viwango vilivyowekwa, kumalizika muda wa ithibati na kutoomba upya usajili pamoja na vyuo kuamua kusitisha mafunzo.
Alisema mbali na vyuo hivyo vitatu vilivyofutiwa usajili, vingine 16 vimezuiwa kusajili wanafunzi au kushushwa hadhi.
Alisema Darmiki College of Educational Studies imezuiwa kusajili wanafunzi baada ya kubainiki kinadahili bila kusajiliwa.
Alivitaja vyuo vilivyoshushwa hadhi kuwa ni Sura Technologies, Institute of Management and Information Technology, Techno Brain, Ministry of Agriculture Training Institute Igurusi, Mbozi School of Nursing, KCMC AMO Ophthalmology School, KCMC AMO Anaesthesia School, Advanced Pediatrics Nursing KCMC.
Vingine ni AMO Training Centre cha Tanga, CATC Sumbawanga, CATC Songea, COTC Maswa, COTC Musoma, Dental Therapists Training Center, Ngudu School of Environmental Health Sciences Kwimba na KCMC AMO General School Moshi.
MWANANCHI
Kazi ya uandikishaji wapigakura imezidi kukumbwa na matatizo baada ya wananchi kuwafgungia waandikishaji ndani ya kituo kutokana na kupata taarifa kuwa muda uliopangwa kwa ajili ya mitaa ya Buhalahala, Kisesa na Moringe umekwisha, huku wakiwa hawajapata nafasi ya kusajiliwa.
Wakati vurugu hizo zikitokea, wananchi wa kata nne za wilayani Bukombe wanahofia kukosa nafasi ya kuandikishwa kutokana na maeneo yao kutoingizwa kwenye mfumo wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), huku watu watatu, wakiwamo watoto wawili wilayani Hanang wakikamatwa kutokana na kujiandikisha mara mbili huku wakiwa hawajafikia umri unaotakiwa.
Tukio la Geita limetokea siku chache baada ya mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kuwataka wananchi mkoani Kilimanjaro kutoruhusu mashine zinazotumika kuandikishia wapigakura kwa njia ya kielektroniki (BVR) kuondolewa vituoni endapo kuna watu ambao hawajaandikishwa.
Uandikishaji mkoani Geita ulianza Juni 17, mwaka huu kwa kata tatu za Buhalahala, Mwatulole na Kalangalala na muda uliopangwa kumalizika ni juzi. Hali ilikuwa mbaya kwenye kata hizo baada ya wananchi kukaa vituoni hadi usiku wakisubiri kuandikishwa, na walipopata taarifa kuwa kazi hiyo haitaendelea kwa kuwa siku zilizopangwa zimemalizika, walichukua uamuzi huo wa kuzuia waandikishaji hadi watakapoandikisha wote waliokuwa wamesalia.
“Nimekuja hapa nina siku ya tano leo (juzi). Kila nikija sipati nafasi ya kuandikishwa wengine wanakesha vituoni siku ya tano, lakini hawajaandikishwa na leo ndiyo mwisho,” alilalamika mkazi wa Mwatulole, Marwa Ernest.
Mkazi mwingine, Neema Charles alisema:“Mwandikishaji anatuambia macho hayaoni, kwa hiyo sisi tufanyeje, tunataka kitambulisho kwani ndiyo cha msingi mwaka huu.”
Wananchi hao ambao walionekana kuwa na jazba, huku wakitishia kuchoma mashine kama wasingeandikishwa, walidai kuwa shughuli hiyo imetawaliwa na rushwa.
Hali hiyo ilikikumba kituo cha Shule ya Sekondari ya Kalangalala, ambako hadi saa 1:30 usiku mwandishi alishuhudia zaidi ya wananchi 200 wakiwa kituoni wengine wakipigana na kusukumana kila mmoja akitaka kuandikishwa.
“Hapa muda unaisha na leo (juzi) ndiyo mwisho, hatujui hatima yetu, wananchi wengi hatujaandikishwa, tumeshaomba tuongezewe mashine lakini hatusikilizwi zaidi tunashuhudia wenye fedha ndiyo wanaandikishwa, alisema mkazi wa Kisesa, Mariana Peter.
Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Geita, Hellen Kahindi alikiri kuwapo kwa vurugu hizo na kwamba walikosea kuweka vituo pembezoni mwa mji, jambo lililosababisha wananchi wa mjini kukimbilia maeneo hayo wakihofia kutoandikishwa.
Alisema vurugu hizo zilisababisha magari mawili ya Serikali kuvunjwa vioo, huku waandikishaji wakiponea chupuchupu kutokana na kuwapo na vurugu kubwa eneo la kutokea hadi polisi walipoingilia kati.
MWANANCHI
Kada wa CCM, Elidephonce Bilohe, mkulima anayeomba kupitishwa na chama chake kuwania urais, amesema anatumia usafiri wa mabasi ya umma kuzunguka mikoani kusaka wadhamini.
Wakati Bilohe akitumia usafiri huo, wagombea wenzake wanatumia au walitumia mabasi waliyokodi na kuyafanyia maboresho ndani, magari madogo na ndege kutafuta wadhamini 450 kutoka mikoa 15 inayotakiwa kwa mujibu wa taratibu za CCM.
Bilole alisema ameshafika mikoa tisa ambayo ni Dodoma, Kigoma, Geita, Mwanza, Simiyu, Shinyanga, Tabora, Morogoro na Dar es Salaam, tangu alipochukua fomu hiyo Juni 9.
“Huko kote nimekuwa nikienda kwa kutumia usafiri wa mabasi ya abiria na daladala. Kwa kweli nimepata ushirikiano mzuri kutoka kwa makatibu wa CCM, nawashukuru sana,” alisema.
Bilohe alisema atakwenda mikoa 15 tu kama inavyotakiwa na chama chake, tofauti na watiania wengine ambao baadhi wamekwenda zaidi ya mikoa 20.
“Kwenda mkoa mmoja natumia siku mbili ama tatu kufika na kupata wadhamini. Gharama ni nyingi sana, lakini kwa kuwa nimeshaamua kuwatumikia Watanzania nitakwenda,”alisema.
Alisema kuwa atazirudisha fomu hizo Juni 30 au Julai Mosi kulingana na ratiba yake ya kukusanya wadhamini.
Jumla ya makada 39 wamejitokeza kuwania nafasi hiyo na Bilohe ndiye mgombea pekee aliye na elimu ndogo ya darasa la saba, tofauti na sheria ya nchi inayotaka mgombea wa nafasi hiyo ya juu kisiasa awe na shahada.
Bilohe ni mmoja wa makada wachache waliojitokeza kuomba ridhaa ya CCM ambao hawajawahi kushika madaraka makubwa serikalini au ya kisiasa.
Katika kinyang’anyiro hicho kuna mawaziri wakuu watatu, mawaziri 12 wa sasa, Jaji Mkuu mstaafu, maofisa wa juu wa Idara ya Usalama wa Taifa, maofisa waandamizi wa Serikali ambao wamestaafu na wabunge.
MWANANCHI
Jeshi la Polisi, Uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Nyerere (JNAI), linamshikilia, raia wa Kuwait, Hussein Mansoor, kwa kukutwa na kobe hai 173 aliokuwa akiwasafirisha kueleka nchini kwake.
Kaimu Mkurugenzi wa Uwanja wa JNIA, Clemence Jingu alisema abiria huyo mwenye hati ya kusafiria yenye namba 003870237, alikamatwa usiku wa kuamkia jana akijitayarisha kupanda ndege ya Emirates iliyokuwa ikielekea Kuwait kupitia Dubai.
Jingu alisema raia huyo alikamatwa saa tano usiku katika eneo la abiria wanaoondoka, baada ya polisi wa JNIA kwa kushirikiana na maofisa wa Wizara ya Maliasili kufanya ukaguzi na kugundua kobe hao wakiwa wamefichwa kwenye masanduku makubwa mawili.
“Hii ni moja ya kazi kubwa ambazo tunazifanya kwa sasa hapa JNIA, ila tutahakikisha kuwa hakuna nyara za Serikali zitakazotaifishwa na kupitishwa hapa kwa kuwa tumeimarisha ulinzi maradufu,” Jingu.
Jingu alisema kobe hao wenye thamani ya Sh 30 milioni ni miongoni mwa nyara muhimu za Serikali ambazo zimekuwa zikitaifishwa kupitia mbinu mbalimbali.
Pamoja na kuimarisha ulinzi, lakini tutahakikisha JNIA inakuwa bora kuliko viwanja vingine vya Afrika Mashariki na zaidi hasa kuhakikisha ulinzi unapewa kipaumbele” alisema.
Kamanda wa Polisi wa JNIA, Khamis Suleiman, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa mtuhumiwa huyo anashikiliwa na jeshi hilo kwa uchunguzi zaidi.
Tukio hilo lilithibitishwa pia na Kamishna wa Interpol, Tawi la Tanzania, Gustav Babile ambaye alisema raia huyo alikamatwa na wanyama hao huku akiwa na vibali halali.
Mmoja wa wafanyakazi wa JNIA alisema kabla ya kukamatwa, ilionekana kuna mpango umefanywa ili kumpitisha raia huyo bila kugundulika kwani taa za eneo la ukaguzi zilizimwa kwa saa kadhaa uwanjani hapo.
“Si kawaida taa kuzimwa lakini wakati yeye anapita taa zilizima jambo linaloonyesha kuwa ni njama zilizopangwa lakini hata hivyo hazikufanikiwa,” kilisema chanzo hicho.
Tukio hili linafanana kwa kiasi kikubwa na lile lililotokea Januari 8, mwaka huu, ambapo raia mwingine wa Kuwait, Ahmed Ally Mansour alikamatwa uwanja wa JNIA akiwatorosha kenge hai 149 wenye thamani ya Sh 6.3 milioni.
NIPASHE
Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya Arumeru na Diwani wa kata ya Mlangarini wilayani humo, Mathias Manga, amenusurika kuuawa baada ya watu wasiojulikana waliokuwa wakimfuatilia kumpiga risasi nje ya geti la nyumba yake
Manga ambaye pia ni mfanyabiashara maarufu wa Tanzanite huko Mirerani, mkoani humu ni mmoja kati ya marafiki wakubwa wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, ambaye ametangaza nia ya kuomba ridhaa ya CCM  kumteua kuwa mgombea wa kiti cha urais katika uchaguzi mkuu mwaka huu.
Manga alikuwa Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya kumtafutia wadhamini Lowassa mkoani Arusha, kazi ambayo ilikamilika jana baada ya kupata wadhamini 12o,339.
Haijafahamika rasmi iwapo tukio la kupigwa risasi na kujeruhiwa kwake, lina uhusiano wowote wa kibiashara au kisiasa, kwa sababu Manga mwenyewe hakutaka kuzungumza na waandishi wa habari kuhusiana na suala hilo.
Awali alisema angezungumza na waandishi wa habari baada ya nusu saa kwa vile alikuwa katika mazingira ambayo hayakuwa mazuri kuzungumza, lakini alipopigiwa tena simu alisema hawezi kuzungumza chochote.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo eneo la Ngarenaro  na risasi hiyo ilimparaza Manga maeneo ya ubavu wa kulia.
Alitoka katika shughuli zake za kawaida na alipokuwa anarejea nyumbani kwake eneo la Ngarenaro kwenye nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa, ghafla aliona gari likimfuata kwa nyuma na alipokuwa akitembea kwa kasi nalo liliongeza mwendo, akahisi watu hao wanamfuata, hivyo akazidi kuongeza mwendo hadi alipofika getini kwake na lile gari pia lilieggeshwa kwa nyuma yake,” alisema.
Alisema kwa maelezo ya Manga watu hao walikuwa watano na wote walikimbia bila kuchukua kitu chochote na yeye alipelekwa Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru kwa matibabu ambako alipata matibabu na kuruhusiwa kurudi nyumbani kutokana na kutoumia sana.
Lowassa jana wakati wa kudhaminiwa mkoani Arusha jana, alimpa pole Manga kutokana na tukio hilo kinalidaiwa kufanywa na majambazi.
NIPASHE
Bunge limesikia maoni ya wadau ya kuuondoa Bungeni Muswada wa Sheria ya Haki ya Kupata Habari 2015 ambao ulitarajiwa kusomwa kwa mara ya pili Juni 27, mwaka huu.
Katibu wa Bunge, Dk. Thomas Kashililah, alithibitisha hayo jana kwenye viwanja vya Bunge wakati akihojiwa kutaka kujua iwapo ushauri wa kamati umemfikia Spika na uamuzi juu ya suala hilo.
“Ushauri wa kamati umezingatiwa, Muswada umeondolewa Bungeni,” Dk. Kashilillah.
Aidha, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju, alisisitiza kuwa maoni ya wadau hayawezi kupuuzwa katika uandaaji wa Muswada wa Sheria ya Haki ya Kupata Habari, 2015.
“Hatutapuuza maoni ya wadau hasa yanayolenga kuboresha muswada husika. Utungaji wa sheria yoyote ni lazima uwe shirikishi, hivyo maoni ya wadau yamesikikizwa kama ilivyokuwa awali walishauri Muswada huo na ule wa Huduma kwa Vyombo vya Habari, usije kwa hati ya dharura, tulizingatia na uliondolewa,” alibainisha.
Juni 22, mwaka huu, wadau mbalimbali wa habari waliokutana jijini Dar es Salaam, walipinga miswada hiyo kwa kile kinachoelezwa kuwa inakiuka sheria za kimataifa, Katiba ya nchi na kuwanyima haki raia kupata taarifa na kuua ndoto ya vijana wanaotarajia kunufaika na tasnia ya habari.
Wadau hao ni Chama cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari Tanzania ( MOAT), Baraza la Habari Tanzania (MCT), Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika (MISA) Tawi la Tanzania na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu ( THRDC).
Mmiliki wa Kampuni ya New Habari Corperation, Rostam Aziz, alisema muswada huo ni mbaya kwani unazuia dhana nzima ya uwazi na ukweli hivyo kulirudisha taifa nyuma na kuitaka serikali kutopeleka bungeni hadi wadau wote wa tasnia ya habari watakapotoa maoni.
“Serikali isifanye haraka, muswada huu utaturudisha nyuma kama taifa. Usitishwe kupelekwa bungeni hadi pale wadau wote watakapotoa maoni yao,” Rostam.
Katibu Mtendaji wa MCT, Kajubi Mukajanga, alisema baraza hilo limetoa ombi hilo kwa sababu wadau wa habari hawakuwa na muda wa kutosha kutoa maoni yao baada ya kusomwa kwa mara ya kwanza wiki iliyopita.
HABARILEO
Rais Jakaya Kikwete amewashangaa wanasiasa wanaokosoa kitendo cha Serikali yake kukopa fedha nje ya nchi kuwa kinazidisha deni la taifa, kwamba hawana ufahamu na kufafanua kuwa katika kuharakisha maendeleo ya nchi, kukopa ni jambo la kawaida.
Alisema hata mataifa makubwa yaliyopiga hatua kubwa kwenye maendeleo yamekuwa yanakopa na akasisitiza kuwa uamuzi wa serikali kwenda nje kukopa amekuwa anaufanya ili kupata fedha kwa ajili ya kujenga miundombinu ambayo itaifanya nchi ipige hatua kubwa kimaendeleo.
Alitoa mfano kuwa hata kama mtu anaendesha duka ni lazima akakope benki kama anataka kuendeleza duka lake, kama hatafanya hivyo kwa kuamini kuwa fedha anazopata kwa kuuza bidhaa zitalitunisha duka hilo basi asubiri miujiza ya kumpatia faida.
Aliyasema hayo wakati akizungumzia uamuzi wa serikali yake kuwenda kukopa nje kwa ajili ya kujenga miundombinu mbalimbali, ikiwemo ujenzi wa mkongo wa taifa ambao alisema lengo lake ni kuweka misingi ya miundombinu wakati taifa linapoelekea kwenye utekelezaji wa ujenzi wa viwanda vya kisasa.
Rais Kikwete alisema baada ya kufanya uamuzi huo aliamua pia kuwekeza kwenye utafiti kwa kuhakikisha kuwa Serikal inatenga fedha kwa ajili ya kuwasomesha watafiti, kununua vifaa vya utafiti na kukarabati vituo vya utafiti ambayo alisema vingi vilikuwa kwenye hali mbaya.
“Tulianza na Sh bilioni 10, tunashukuru sasa hivi tupo kwenye Sh bilioni 60 na naamini kuwa Rais atakayekuja ataendeleze juhudi hizi kwa kutenga fedha zaidi kwa ajili ya tafiti maana nikiangalia hali ya baadaye ya maendeleo ya nchi hii inategemea watafiti, wanasayansi na wabunifu,”  Rais Kikwete.
Rais alisema anajivuna kwamba anaondoka madarakani wakati shughuli za utafiti zimepata uhai na kwamba juhudi zilizofanywa na Serikali yake za kuwaendeleza wabunifu zimezaa matunda mengi kwani kwa sasa nchi ina watafiti wazee na vijana wanaofanya mambo makubwa yanayotambulika kimataifa.
Alisema fedha zilizotolewa na serikali yake zimesaidia kusomesha watafiti 517 katika kozi za shahada ya uzamili na uzamivu na vituo 20 vimekarabatiwa na miradi 70 ya utafiti imetekelezwa.
Mkurugenzi Mkuu wa Costech, Dk Hassan Mshinda alisema kongamano hilo la nne limewakusanya wanasayansi, watafiti, watunga sera na wabunifu mbalimbali.
Alisema mada 80 zitajadiliwa ikiwemo tafiti mbalimbali zilizofanywa na watafiti wa ndani, kujadiliana changamoto za kupeleka utafiti sokoni na upatikanaji wa teknolojia na jinsi ya kuhuisha sayansi asili na sayansi ya kisasa.
Kwa habari, matukio na michezo ni hapa hapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment