Friday, June 17, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 21

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI

MWANAMKE 21Inaletwa kwenu na kituo cha Elimu Cha New Age Centre Tanga, New Age ni mabingwa wa Ufundishaji na Ufaulishaji wanafunzi wanaorisiti na kujiendeleza, New Age wapo Tanga mkabala na TOYOTA, wanapokea wanafunzi wa kozi fupi na ndefu pamoja na wanaojiendeleza kielimu maofisini, simu 0717 713866

ILIPOISHIA

Nikatazamana tena na mama yangu, sasa kwa mshituko.

“Dakika chache tu zilizopita si nilikuwa naye hapa?” nikauliza.

“Kufariki kwake kulikuwa kwa miujiza sana. Niliambiwa alikuwa akizungumza na mteja wake mmoja aliyefika na pikipiki, nafikiri ulikuwa wewe”

“Nadhani nilikuwa mimi kwani si muda mrefu sana nilipoondoka hapa”

“Basi mara tu ulipoondoka, yule mganga aliingia chumbani mwake. Mke wake alikuwa jikoni akasikia sauti ya mume wake akipiga kelele kuwa anakabwa na mwanamke. Mpaka mke wake anaingia chumbani alimkuta ameshakufa”

“Nikaguna na kumtazama mama.

“Mama umelisikia hilo tukio?”

“Nimelisikia” Mama akajibu kwa sauti iliyonywea kisha akaniambia.

“Basi twende zetu”

“Nilikuwa nimempa pesa kwa ajili ya kunifanyia kazi yangu ambayo tulipatana aifanye kesho lakini nitamsamehe” nikasema.

“Ulimpa kiasi gani?’ yule mtu akaniuliza.

“Kama laki mbili hivi. Lakini nitasamehe”

“Kama umeamua kuzisamehe ni jambo zuri”

“Poleni sana kwa msiba huo” nikamwambia na kupanda kwenye pikipiki yangu.

“Haya kwaheri baba” Mama akumuaga yule mtu kabla ya kukaa nyuma yangu. Tukaondoka.

SASA ENDELEA

“Mama umeona mambo hayo!” nikamwambia mama wakati ninaendesha pikipiki kurudi mjini.

“Nimeona. Kwa kweli ni kifo cha kushangaza sana”

“Mimi nadhani ni yule jini amekuja kumuua yule mganga”

“Itakuwa ndiye yeye, kwa sababu alisema kuna mwanamke anamkaba. Sasa alikuwa mwanamke yupi kama sio yule jini?”

“Sasa haya yamekuwa mapambano!”

“Tutatafuta mganga mwingine”

“Sasa usalama wangu utakuwa wapi? Nimeshashuhudia watu wawili waliouawa leo. Yule kijana aliyekuwa anatandikwa na huyu mganga. Bado kuna na yule kijana mwingine. Naona pia atakuwa ameshakufa”

“Tukifika tutakwenda kulizungumza vizuri hili suala pamona na kaka yako”

“Sasa nimeshaona huyu mwanamke ni wa hatari”

Nilimpeleka mama nyumbani kwake kisha nikaenda  Chuda kumchukua kaka.

Nilimueleza kwa kifupi hayo matukio.

“Mama ameniambia nije nikuchkue twende tukayazungumze haya mambo”

Ule muhutasari wa habari niliomueleza kaka tayari ulikuwa.

Nikampakia kwenye pikipiki yangu tukaondoka.

Tulipofika nyumbani kwa mama tukalizungumza lile suala ambalo kaka lilimshitua sana.

“Kumbe yule jini ni hatari sana. Tulivyomuona pale mahakamani siku ile alionekana ni msichana mpole sana” Kaka akasema kwa mshangao.

“Lile umbile ulilomuona nalo ni la kujipachika, si umbile lake halisi. Katika umbile lake halisi anatisha” nikamwambia kaka.

“Kwa kweli inabidi muepukane haraka, sasa tutafanyaje wakati mtaalamu muliyemtegemea ndio ameuawa kwanza?”

“Itakuja kuwa yeye!” Mama akamalizia akimaanisha mimi.

“Sasa tufanyeje jamani, jua linakuchwa hili!” nikawahimiza wenzangu.

“Hapa la kufanya ni kumuona mganga mwingine haraka iwezekanavyo” Kaka akashauri.

“Bila kupata mganga mwingine, mimi leo sitalala, nina hofu” nikawambia.

“Usijali, tutkwenda kwa mganga wa Amboni. Yeye pia namfahamu. Ni hodari” Mama akasema.

“Sasa twende sasa hivi kwa sababu jua linakuchwa”

“Ingekuwa kaka yako anapafahamu angekupeleka lakini itabidi nikupeleke mimi”

“Mpeleke tu halafu mtakuja kunijulisha” Kaka akamwambia mama.

Dakika chache baadaye tulikuwa tumetoka nje, nilimpakia mama kwenye pikipiki. Kaka yangu naye akaondoka kurudi kwake kwa miguu.

Amboni ni kitongoji cha mji wa Tanga kinachokuwa kwa haraka. Kipo katika barabara ya Horohoro inayokwenda Mombasa nchini Kenya. Kutoka Tanga hadi Amboni ulikuwa mwendo upatao kilometa nane hivi.

Kitongoji hicho kimepata umaarufu kutokana na mapango yaliyoko katika eneo hilo, maarufu kama Mapango ya Amboni.

Wakati tunafika Amboni jua lilikuwa limeshakuchwa. Matumaini yangu yalikuwa madogo sana kupata huduma katika muda ule. Hofu yangu kubwa ilikuwa ni kwa usiku. Kama Zena alikusudia kunifanyia jambo baya lolote, nilijua kuwa alikuwa akisubiri usiku nikiwa niko nyumbani peke yangu.

Hapo Amboni palikuwa na eneo linaitwa Mafuriko. Eneo hilo liliwahi kupata mafuriko makubwa katika miaka ya nyumba na kusababisha kupewa jina hilo.

Mganga tuliyemuendea alikuwa akiishi katika eneo hilo. Kwa vile mama aliwahi kufika kwa mganga huyo katika siku za nyuma hatukusumbuka kuuliza. Tulikwenda moja kwa moja kwenye nyumba yake.

Tulikuta mzee aliyeketi barazani mwa nyumba hiyo akivuta Mtemba. Alikuwa amekaa kwenye kiti cha uvivu kando ya mlango wa nyumba yake.

Kumbe alikuwa ndiye mganga mwenyewe tuliyemuendea.

Tulisaliana naye. Mama akamwambia kuwa tulikuwa tumemfuata yeye.

“Karibuni ndani” akatuambia.

Nikapata matumaini kidogo.

Mganga huyo alikuwa na chumba chake maalum cha uganga. Tulipoingia katika chumba hicho alitukaribisha kwenye majamvi, yeye mwenyewe aliketi kwenye kigoda kidogo kilichokuwa kwenye pembe moja ya ukuta.

“Habari za huko mtokako?” akatuuliza.

“Habari si nzuri. Tuna matatizo” Mama akamwambia.

“Matatizo gani?”

“Ni matatizo ambayo si ya kawaida. Huyu niliyenaye hapa ni mwanangu. Yeye ndiye anayehusika na hayo matatizo….”

Mama akamueleza matatizo yaliyokuwa yametupeleka. Mganga akatuambia.

“Subirini kidogo niwaite wenyewe muwaeleze”

Akamuita mke wake. Mwanamke huyo alipokuja alimwambia amletee moto. Baada ya muda kidogo mwanamke huyo alileta makaa ya moto kwenye chetezo ambacho alikiweka mbele ya mganga huyo.

“Niletee mavumba yangu na shuka yangu” Mganga akaendelea kumuagiza.

Mwanamke huyo alikwenda pembeni mwa chumba hicho ambako kulikuwa na meza iliyokuwa na vitabu pamoja na vichupa na vikopo kopo. Alichukua kikopo kimoja, akatungua na shuka moja ya rangi nyeupe iliyokuwa imetundikwa kwenye ukuta.

Alikwenda navyo kwa mganga akakiweka kile kikopo mbele yake kisha akamfinika ile shuka pale alipokuwa amekaa.

“Na wewe ukae hapa hapa, usiondoke” Mganga akamwambia mwanamke huyo.

Mwanamke huyo akakaa karibu yetu.

Mganga alikisogeza kile chetezo cha moto karibu yake kisha akakifungua kile kikopo kilichokuwa na mavumba akachota kidogo na kuyatia kwenye ule moto kisha akajifinika shuka vizuri ili ule moshi uliokuwa unafuka uingie ndani ya ile shuka.

Baada ya sekunde chache yule mganga akaanza kusema maneno niliyodhani kuwa yalikuwa ya lugha ya Kijerumani.

Nilisikia maneno kama “Dachi…pontia…na mengine ambayo sikuweza kuyakariri.

Wakati huo uso wake alikuwa ameufunika ndani ya shuka. Ghafla akafunua shuka na kuutoa uso wake. Alikisogeza kile chetezo pembeni kisha akatutazama.

“Dachi…jerumani nimekuja hapa” akasema lakini hatukuelewa maana ya maneno yale.

Mke wa mganga akatueleza.

“Anasema yeye ni jini wa Kijerumani anaitwa Dachi, amekuja kuwasikiliza”

“Sawa, tumemuelewa” Mama akamjibu.

“Asalaam aleykum” mganga akaendelea kwa kutupa salamu.

“Wa alaykumu salaam” tukamuitikia.

“Nini shida yenu?”

“Mwanangu anasumbuliwa na jini mwanamke” Mama akamwambia.

“Mwanao yuko wapi?”

“Huyu kijana niliyenaye hapa”

“Oh mwano amepata mchumba wa kijini, anaitwa Zainush”

Mgnga huyo alipotuambia hivyo mimi na mama tukatazamana. Tulitazamana kwa mshangao kwa jinsi alivyoweza kujua lile jina la Zena ambalo hatukuwa tumelitaja.

“Mwanangu hataki mchumba wa kijini, tunataka aondoke asimfuate tena mwanangu” Mama akamwambia.

ENDELEA KUFUATILIA HAPO KESHO UJUE NINI KITAKACHOTOKEA.


No comments:

Post a Comment