Saturday, June 18, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 23


SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0655 340572


MWANAMKE 23

ILIPOISHIA

Mama akamuga mwenzake kisha akaingia kwenye kile chumba alichokuwemo mganga akaagana naye kisha akatoka.

Tulitoka nje tukapanda pikipiki na kuondoka.

“Dawa inanuka kweli!” nikamwambia mama.

“Dawa za kufukuza mashetani ndivyo zilivyo, vumilia tu”

Nilipomfikisha mama nyumbani kwake, nikaenda Msambweni nilikokuwa nikiishi.

Licha ya kuwa na hofu sikuona tatizo lolote usiku ule. Nikalala hadi asubuhi.

Wakati naamka, shuka za kitanda na ile niliyojifinika zilikuwa zikinuka ile harufu ya dawa za mganga. Niliziondoa kitandani nikatandika zingine kisha nikaenda kuoga. Licha ya kujisugua kwa sabauni zaidi ya mara moja, ile harufu bado nilikuwa nikiisikia mwilini mwangu.

Nilikwenda mkahawani nikanywa chai kisha nikapanda pikipiki yangu na kuelekea Chuda kwa kaka yangu.

Nilipofika nilimueleza nilivyoshughulikiwa na yule mganga na alivyonieleza kuwa niende tena siku ile.

“Jana usiku yule mwanamke hakukufuata?” akaniuliza.

“Sikumuona lakini nadhani kama nisingekwenda kwa yule mganga wa Amboni, angenifuata. Naamini zile dawa ndizo zilizomzuia”

“Sasa leo utaakwenda na mama au utakwenda peke yako?”

“Nitakwenda kumsikiliza mama, kama atasema twende tutakwenda”

“Hata kama atakwambia uende peke yako wewe nenda tu, ukirudi utakuja kunieleza”

“Sawa  kaka”

SASA ENDELEA

Nyumbani kwa mama nilimkuta mama akinisubiri. Nilipomuuliza kuhusu safari ya Amboni akaniambia tutakwenda sote. Mama yangu alikuwa na huruma sana. Nikampakia kwenye pikipiki tukaenda Amboni.

Tulipofika tulimkuta mganga akiwa kwenye chumba chake cha uganga akishughulika. Tulisalimiana naye akatuambia tumsubiri nje. Baada ya muda kidogo alitoka nje. Uso wake ulikuwa umefadhaika sana. Akatuambia.

“Jana niliwambia mje lakini usiku nilipolala yule jini wako alinifuata na kuniletea vitisho vikali sana. Aliniambia kuwa kama nitaendelea kukushughulikia kitanikuta kile kilichomkuta mganga wa Mnyanjani. Kwa kweli nilipata hofu sana”

“Lakini jana si ulituambia kuwa huyo jini unaweza hata kumpiga makofi?”

“Baba! Ni kweli nilisema lakini sikujua kama jini mwenyewe ni yule aliyenifuata. Yule jini ni mkali. Alipokuja, majini yangu yalinywea”

Maneno ya mganga huyo yalinifanya nimtazame mama. Mama naye akanitazama kwa mshangao.

Kama ambaye aligundua kuwa maneno yake yalikuwa yamemdhalilisha mwenyewe mganga huyo aliendelea kutuambia.

“Sidhani kama utaweza kuepukana na jini yule. Ameniambia kuwa hakuna atakayeweza kuwatenganisha, atakuwa na wewe mpaka kufa”

“Yaani ameshajihakikishia ushindi?” Mama akamuuliza kwa mshangao.

“Yeye mwenzetu ni jini, sisi ni binaadamu. Anatuona lakini sisi hatumuoni mpaka anapotaka mwenyewe” Mganga akasema.

“Sasa unatushauri nini?”

“Lakini huyu jini hana matatizo kama mnavyomdhania, tena ni jini tajiri na kisha ni mganga, kwanini hutaki kuwa naye?” Mganga akaniuliza.

“Siwezi kuwa na mke jini wakati mimi mwenyewe ni binaadamu. Nitaishi naye vipi?” Nikamuuliza mganga.

“Sasa utafanyaje wakati ameshakuchunuka?”

“Nitajitahidi kuhangaika kwa waganga wengine”

“Ukibahatika kwenda Pemba naamini unaweza kupata waganga ambao wataweza kukusaidia. Wapemba ni hodari sana kwa majini”

“Kama hakuna budi nitafika hata huko Pemba”

“Kama utaweza kwenda naamini utafanikiwa”

Tuliondoka kwa yule mganga tukiwa tumenywea. Mategemeo yangu yote yalififia ghafla. Suala lile sasa lilianza kunipa changamoto kali.

“Maneno ya yule mganga yamenitisha sana” Nilimwambia mama wakati namuendesha.

“Hakuna lisilo na mwisho, jini si Mungu, usitishike mwanangu. Endelea kumuamini Mungu. Jini ni kiumbe kama wewe naye ameumbwa na Mungu. Mungu ndiye wa kumuogopa”

Maneno ya mama yalinipa matumaini kidogo. Nilipomfikisha nyumbani kwake aliendelea kuniambia.

“Makosa yetu ndiyo yanayotuponza. Imani za watu zimekuwa ndogo sana katika dini. Watu wanapenda dunia zaidi. Sasa vile vitu ambavyo vilipaswa kuwa chini yetu vinakuwa juu yetu. Mwanaadamu ndiye aliyetakiwa kutawala dunia hii lakini baada ya watu kupunguza kumcha Mungu, sasa majini yanataka kututawala sisi”

“Leo mama umeniambia maneno ya akili na ya kufikirisha sana” nikamwambia mama.

“Rudi nyumbani na muamini Mungu wako, jini hatakufuata”

“Asante mama”

Nikaondoka na pikipiki yangu kurudi nyumbani nikiwa na imani tele. Nilijiambia kama mimi ndiye niliyepaswa kuwa mtawala wa dunia hii sitakubali jini anitawale wala kunitia hofu.

Ni kweli imani ina nguvu, nilikaa wiki nzima bila kuona kitisho chochote. Nikaona kama vile tatizo langu lilikuwa limekwisha.

Wiki iliyofuata nikiwa kazini kwangu, tuliendelea kufanya biashara hadi saa kumi jioni, yaani siku ile kulitokea biashara ya ajabu. Tulipata wateja wengi kutoka vijijini kwa vile ulikuwa msimu wa kuuza mazao.

Nikajikuta nilikuwa na pesa nyingi kwenye dawati langu. Muda huo sikuweza kuzifikisha pesa hizo benki kwa sababu benki zilikuwa zimeshafungwa.

Nilizihesabu pesa hizo, zilikuwa shilingi milioni kumi. Hizo zilikuwa za mauzo ya jioni tu, za mauzo ya asubuhi na mchana zilishapelekwa benki.

Nikaamua kuziacha pesa hizo kwenye dawati langu kwa vile nilifunga kitasa kwa funguo. Tukafunga duka na kuondoka.

Asubuhi ya siku ya pili yake nilikwenda kazini kama kawaida. Nilipofika kitu cha kwanza nilitaka nizitoe zile pesa ili zipelekwe benki. Nilipofungua dawati sikuona kitu.

Nikashituka na kutumbua macho yangu. Sikutosheka kutazama kwa macho, nilitia mkono wangu na kupapasa. Hakukuwa na kitu. Dawati lilikuwa tupu kama mkono uliorambwa!

“Pesa za watu zimewenda wapi jamani?” nikajiuliza kwa fadhaa.

Meza yangu ilikuwa na madawati matatu. Pesa niliziweka katika dawati la juu. Baada ya kuzikosa pesa katika dawati hilo nilianza kuzitafuta katika madawati ya chini yake japouwa nilikuwa na hakika kuwa pesa hizo niliziweka katika dawati la juu.

Nilikuwa kama niliyerukwa na akili. Licha ya kupekua kwenye madawati yote matatu, pesa sikuziona. Akili yangu ilikuwa haiamini kama pesa hizo hazikuwemo kwa sababu niliziweka mwenyewe na dawati nililifunga kwa funguo.

Nikarudi tena kwenye dawati la juu kutazama tena. Nikaja kwenye dawati la pili na la tatu. Lakini hakukuwa na pesa.

Ule mchezo wangu wa kufungua madawati kuanzia la juu hadi la chini na kisha kurudia tena, uliwashitua wafanyakazi wenzangu wakaanza kuniuliza ninachotafuta.

“Amour mbona umeshughulika sana, unatafuta nini?” Mfanyakazi mmoja akaniuliza.

“Natafuta pesa. Jana tulipoondoka niliacha shilingi milioni kumi katika dawati hili la juu, sasa sizioni!” nikamwambia.

“Zimekwenda wapi?”

“Sijui!”

“Kwani ulipoondoka hukulifunga?”

“Nililifunga na funguo niliondoka nazo, sasa nashangaa pesa sizioni!”

“Haiwezekani! Hebu tazama vizuri”

“Nimetafuta sana, pesa hazimo. Sijui nani amezichukua!”

“Na haiwezeani zichuuliwe na mtu wa sababu funguo uliondoka nazo mwenyewe”

Nikanyamaza kimya huku macho yangu yakitanga tanga kwenye meza.

Wafanyakazi wengine waliposikia mazungumzo yetu wakasogea karibu.

“Umepoteza nini,  pesa?” mfanyakazi mmoja akaniuliza.

“Ndio pesa”

“Uliziweka wapi?”

“Nilizizifungia kwenye dawati hili hapa jana jioni tulipotoka kazini, sasa nashangaa pesa sizioni”

PESA ZA WATU ZIMEKWENDA WAPI JAMANI? HII IMESHAKUWA BALAA SASA! TUONANE HAPO KESHO.


No comments:

Post a Comment