Saturday, June 18, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 22

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI

MWANAMKE 22

ILIPOISHIA

Baada ya sekunde chache yule mganga akaanza kusema maneno niliyodhani kuwa yalikuwa ya lugha ya Kijerumani.

Nilisikia maneno kama “Dachi…pontia…na mengine ambayo sikuweza kuyakariri.

Wakati huo uso wake alikuwa ameufunika ndani ya shuka. Ghafla akafunua shuka na kuutoa uso wake. Alikisogeza kile chetezo pembeni kisha akatutazama.

“Dachi…jerumani nimekuja hapa” akasema lakini hatukuelewa maana ya maneno yale.

Mke wa mganga akatueleza.

“Anasema yeye ni jini wa Kijerumani anaitwa Dachi, amekuja kuwasikiliza”

“Sawa, tumemuelewa” Mama akamjibu.

“Asalaam aleykum” mganga akaendelea kwa kutupa salamu.

“Wa alaykumu salaam” tukamuitikia.

“Nini shida yenu?”

“Mwanangu anasumbuliwa na jini mwanamke” Mama akamwambia.

“Mwanao yuko wapi?”

“Huyu kijana niliyenaye hapa”

“Oh mwano amepata mchumba wa kijini, anaitwa Zainush”

Mgnga huyo alipotuambia hivyo mimi na mama tukatazamana. Tulitazamana kwa mshangao kwa jinsi alivyoweza kujua lile jina la Zena ambalo hatukuwa tumelitaja.

“Mwanangu hataki mchumba wa kijini, tunataka aondoke asimfuate tena mwanangu” Mama akamwambia.

SASA ENDELEA

“Yule jini ni mkorofi, ameshaua watu watatu” Mganga huyo aliendelea kutuambia.

Tukatazamana tena na mama. Mama hakulieleza suala hilo la watu waliouawa, yaani yule mganga wa Mnyanjani na wale vijana wawili walioiba mkoba wa Zena.

Tukawa tunajiuliza amelijuaje tukio hilo la kuuawa kwa yule mganga na wale vijana.

Kama ambaye aliyagundua mawazo yetu, mganga huyo akacheka.

“Huyo jini anakufuata wewe kila wakati, ameshapata wasiwasi. Anajua unataka kumfukuza” akatuambia.

Alinyamaza kimya kisha akaendelea.

“Lakini mimi haniwezi, naweza kumpiga makofi mara moja”

“Sasa utatusaidiaje?” nikamuuliza mganga huyo.

“Mimi naweza kumuita halafu nitamfunga kamba, hataweza kukufuata tena”

“Utamuita lini?” nikamuuliza tena.

“Nitamuita kesho”

“Sasa leo akija kunidhuru usiku?”

“Nitamzuia” Mganga akaniambia kisha akaitenga shuka na kunyanyuka.

“Nisubirini hapa hapa” akatuambia na kutoka.

Tulisubiri kwa karibu nusu saa. Mke wake alituambia kuwa mganga huyo alikuwa amekwenda kuchuma dawa makaburini.

Aliporudi alikuwa ameshika rundo la majani, akampa mke wake.

“Yaroweke kwenye maji” alimwambia.

Mke wake aliyekuwa ameketi na sisi aliinuka na kuyachukuaa yale majani.

“Changanya na huu mvuje” Mganga aliendelea kumwambia mke wake huku akielekea kwenye meza iliyokuwa na chupa na makopokopo. Alichukua kopo mojawapo akachota kiasi cha mvuje uliokuwa umesagwa na kumpa mke wake.

Baada ya hapo mganga alirudi kwenye kigoda chake.

“Nimekutayarishia dawa ambayo utakwenda kuoga na nyingine utajifukiza” akaniambia.

“Sawa. Kwa hiyo nitakwenda kuoga nyumbani?”

“Hapana. Utaoga hapa hapa na utajifukiza hapa hapa”

“Sawa”

Baada ya kama dakika tano hivi mke wa mganga alirudi akiwa amebeba ndoo ya maji ambayo aliitia yale majan.

“Tayari” akasema.

“Sasa nenda kamuwekee chooni” Mgnaga akamwambia.

Mwanamke huyo akaibeba tena ndoo hiyo na kutoka nayo.

Mganga akanitazama.

“Mfuate, utakwenda kuyaoga yale maji yote” akaniambia.

Nikanyanyuka na kumfuata yule mwanamke. Tulitoka uani mwa ile nyumba. Mwanamke huyo aliingia kwenye choo akaiweka ile ndoo kisha akatoka.

“Haya nenda sasa’ akaniambia.

Nikaingia kwenye kile choo. Nilivua nguo nikazitundika kwenye mlango wa choo. Niliona kata iliyokuwa imetiwa kwenye ndoo nyingine niliyoikuta mle chooni, nikaichukua na kujimwagia yale maji. Yalikuwa yakinuka harufu mbaya sana isiyovumilika.

Lakini kwa vile nilikuwa na shida nilivumilia hivyo hivyo. Nilipomaliza nilijifuta futa maji kwa mikono kisha nikavaa nguo zangu na kutoka na ile ndoo ambayo niliiacha pale uani.

Nilienda kule chumbani kwa mganga huku maji yakiwa yametosa shati langu.

“Umeshaoga?” Mganga akaniuliza.

“Nimeoga” nikamjibu.

“Umemaliza maji yote?”

“Nimeyamaliza yote”

“Sasa bado dawa ya kujifukiza” Mganga aliniambia kisha akawageukia mke wake na mama yangu.

“Hebu mpisheni ajifukize dawa” akawambia.

Mama yangu na yule mwanamke wakatoka.

Mganga akanipa shuka.

“Vaa shuka. Vua nguo zako kisha chutama ujifukize dawa”

Nikajifunga ile shuka kiunoni kisha nikavua suruali yangu pamoja na shati. Mganga alinisogezea kile chetezo cha moto. Akakitia aina fulani ya dawa ya unga. Chetezo kikawa kinatoa moshi.

Nilikuwa nimeshachutama. Ile shuka ndio nilijifunika kukinga ule moshi uingie mwilini mwangu. Harufu yake ilifanana na yale maji niliyooga.

Wakati ule moshi ukinipata mwilini. niliisikia sauti ya mganga akisema maneno kwa lugha ambayo sikuweza kuijua huku akilitaja jina la Zainush.

Moshi ulipokwisha, mganga aliniambia nininuke na nivae nguo zangu. Nikainuka na kuvaa nguo.

“Sasa kazi yako imekwisha kwa leo, rudi nyumbani ila kesho asubuhi uje tena” Mganga akaniambia.

“Hii kazi yaa leo ni shilingi ngapi?” nikamuuliza mganga huyo.

“Kwa leo utanipa shilingi elfu ishirini”

“Nikatoa shilingi elfu ishirini na kumpa mganga huyo.

“Sasa mnaweza kwenda zenu”

“Yule jini hataweza kunifuata tena leo?” nikamuuliza.

Mganga akatikisa kichwa.

“Hawezi kukufuata. Hiyo harufu unayonuka hataweza hata kukusogelea”

“Nashukuru sana’

“Ila kumbuka kitu kimoja. Ukifika nyumbani usioge tena. Lala hivyo hivyo”

“Sawa”

Baada ya kumalizana na mganga huyo nilitoka ukumbini. Mama yangu alikuwa amekaa na mke wa mganga, nikamwambia.

“Twenzetu”

“Umeshamaliziwa?” Mama akaniuliza.

“Tayari”

Mama akamuga mwenzake kisha akaingia kwenye kile chumba alichokuwemo mganga akaagana naye kisha akatoka.

Tulitoka nje tukapanda pikipiki na kuondoka.

“Dawa inanuka kweli!” nikamwambia mama.

“Dawa za kufukuza mashetani ndivyo zilivyo, vumilia tu”

Nilipomfikisha mama nyumbani kwake, nikaenda Msambweni nilikokuwa nikiishi.

Licha ya kuwa na hofu sikuona tatizo lolote usiku ule. Nikalala hadi asubuhi.

Wakati naamka, shuka za kitanda na ile niliyojifinika zilikuwa zikinuka ile harufu ya dawa za mganga. Niliziondoa kitandani nikatandika zingine kisha nikaenda kuoga. Licha ya kujisugua kwa sabauni zaidi ya mara moja, ile harufu bado nilikuwa nikiisikia mwilini mwangu.

Nilikwenda mkahawani nikanywa chai kisha nikapanda pikipiki yangu na kuelekea Chuda kwa kaka yangu.

Nilipofika nilimueleza nilivyoshughulikiwa na yule mganga na alivyonieleza kuwa niende tena siku ile.

“Jana usiku yule mwanamke hakukufuata?” akaniuliza.

“Sikumuona lakini nadhani kama nisingekwenda kwa yule mganga wa Amboni, angenifuata. Naamini zile dawa ndizo zilizomzuia”

“Sasa leo utaakwenda na mama au utakwenda peke yako?”

“Nitakwenda kumsikiliza mama, kama atasema twende tutakwenda”

“Hata kama atakwambia uende peke yako wewe nenda tu, ukirudi utakuja kunieleza”

“Sawa  kaka”

WASOMAJI MPO? MAMBO YATAENDELEA KESHO.
MSIKOSE.

No comments:

Post a Comment