Wednesday, June 22, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 25

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0655 340572

MWANAMKE 25

YAAP! TUMEKUTANA TENA. JANA TULIISHIA WAPI? TULIISHIA HAPA……

TUJIKUMBUSHE.

Nilipofika nyumbani kwa kaka Chuda, ilikuwa ikikaribia kuwa saa sita mchana.

“Leo hukwenda kazini?” kaka akaniuliza.

“Nimekwenda lakini kumetokea matatizo”

“Matatizo gani?”

“Kuna pesa zimeibiwa kwenye dawati langu”

“Lini?”

“Leo hii”

“Kiasi gani?”

“Shilingi milioni kumi”

Kaka akashituka. Enzi hizo pesa hizo zilikuwa nyingi sana.

“Zimeibiwaje?”

Nikamueleza kaka jinsi wizi huo ulivyotokea.

“Inawezekana huyo jamaa alikuwa na ufunguo mwingine ambao aliutumia kufungua dawati lako akaiba hizo pesa”

“Ndio hivyo lakini  sasa dhima imeniangukia mimi”

“Kwa hiyo umeambiwa nini”

Nitoke nikatafute pesa za shirika nizirudishe, nimepewa siku mbii tu”

SASA SONGA NAYO…

“Kama hukuzipata itakuwaje?”Kaka akaniuliza.

“Suala hilo litapelekwa polisi”

“Ukisikia balaa ndio hilo, wadhani utazipata wapi milioni kumi?”

“Hiki ni kifungo kinaningoja”

Kaka akatikisa kichwa kusikitika.

“Nakuhurumia sana mdogo wangu sijui nitakusaidiaje?”

“Msaada ni kupata hizo pesa na pesa hazipo”

“Umekwenda kumueleza mama?”

“Nimekwenda, nimemueleza”

“Amesemaje?”

“Hakuwa na usemi, amesikitika tu”

Wakati ninasema hivyo nilimuona kaka amezama katika fikira. Nikajua lile tatizo lilikuwa limeugusa moyo wake.

“Sasa itabidi tusubiri tuone uamuzi wa wakuu wako” Kaka akaniambia baada ya kimya kifupi.

“Uamuzi! Kuna uamuzi gani tena kaka zaidi ya kufunguliwa kesi ya wizi. Kwani si nimeshaambiwa kama pesa hazitapatikana baada ya siku mbili, hili suala linafikishwa polisi!” Nikamwambia kaka.

Kaka alikuwa amejishika kichwa akisikitika.

“Kilichobaki sasa ni kuomba Mungu hizo pesa zipatikane”

Wakati kaka akisema hivyo mimi nilikuwa kimya.

“Mungu amtie imani huyo aliyeziiba azirudishe kabla ya hizo siku mbili” Kaka aliendelea kuniombea.

Hakuna mwizi au jambazi anayerudisha kile alichokiiba lakini kwa vile kaka yangu alikuwa akiniombea ilibidi nimsikilize.

Siku ile nilishinda bila furaha na kusema kweli nilishindwa hata kula chakula. Nilikwenda nyumbani kulala tu.

Siku ya pili yake nilikwenda kazini. Mhasibu aliponiona akaniita ofisini kwake. Nilipokwenda aliniuliza kama nimefanikiwa kupata zile pesa.

“Sijazipata bosi” nikamwambia.

Uso wa mhasibu ukaonesha kuhamaki.

“Unajua kuwa zile ni pesa za shirika?” akaniuliza kwa ukali kidogo.

“Ninajua bosi”

“Na unajua kuwa nilikupa siku mbili urudishe zile pesa?”

“Ninajua”

“Kama unajua hivyo sawa. Kesho uje na hizo pesa vinginevyo sitakuelewa”

Sikuwa na jingine la kumjibu zaidi ya kumuitikia. Nilishajua kuwa nisipokuja na pesa hizo atanifikisha polisi. Na mimi nilikuwa nimeshajitolea kwenda jela.

Siku ile nilishinda kazini hadi muda wa kutoka kazini nikatoka na wenzangu. Tulipokuwa nje baadhi ya wafanyakazi wenzangu waliniuliza kuhusu upotevu wa zile pesa. Kila mtu alionekana kushangaa jinsi pesa hizo zilivyoibiwa.

“Nimepewa siku mbili nizirudishe hizo pesa vinginevyo suala litafikishwa polisi kwa hatua zaidi” nikawambia.

Kila mtu aling’aka na kunihurumia.

“Sasa ni nani aliyefanya mchezo huo. Hapa kazini kweli hakuna mchezo wa kuibiana pesa” Mfanyakazi mmoja akaniambia.

“Hata mimi nashindwa kuelewa”

Baadhi ya wafanyakazi wenzangu walikuwa wamenizunguka wakinisikiliza na kunihoji. Baadaye tulichangukana tukarudi majumbani.

Lakini mimi sikurudi nyumbani. Nilikwenda nyumbani kwa mama. Ukiwa na mama, hata ukiwa mtu mzima utamdekea tu. Pale kwa mama ndipo nilipopaona mahali muafaka wa kupeleka kilio changu ingawa hakuwa na uwezo wowote lakini alikuwa ni mama.

Nikamueleza mama yaliyojiri huko kazini kwangu. Nikamwambia kwamba kesho ndio natakiwa kupeleka hizo pesa vinginevyo ninafikishwa polisi.

“Itabidi hapo kesho uende kazini na kaka yako ili litakalotokea aweze kulijua” Mama akaniambia.

Jioni ile ile nilikwenda kwa kaka nikamueleza na tukakubaliana kwamba nimpitie asuhuhi anisindikize kazini.

Siku ile nilipanga vizuri vitu vya nyumbani nikijua kwamba kesho yake ninakwenda jela. Usiku wake sikupata usingizi kwa mawazo.

Nakumbuka nilipata usingizi majira ya saa kumi alfajiri nikaota ndoto ya kutisha. Niliota nimesimamishwa kizimbani nikihukumiwa kwa kosa la wazi wa fedha za shirika.

Hakimu aliniambia. “Ushahidi uliotolewa hapa mahakamani umeonesha na kuthibitisha bila shaka yoyote kwamba umeiba shilingi milioni kumi fedha za shirika ukiwa mfanyakazi wa shirika hilo. Hivyo mahakama hii imekutia hatiani”

Hakimu akainua uso wake na kunitazama kisha akaniuliza.

“Una lolote la kuiambia mahakama hii kwanini isikupe adhabu kali?”

“Mheshimiwa hakimu ninaiomba mahakama yako tukufu isinipe adhabu kali kwa kuzingatia kuwa fedha zenyewe sikuziiba mimi na kwa kweli sijui zimeibiwa na nani” nikasema.

Hakimu akaandika maelezo yangu kisha akainua tena uso wake na kuniambia.

“Maelezo yako hayawezi kuizuia mahakama hii isikupe adhabu kali. Ninakuhukumu kifungo cha miaka thelathini jela ili iwe fundisho kwa wengine”

Hapo hapo nikaacha mdomo wazi kwa mshangao kama ambaye sikuamini kuwa nilihukumiwa kifungo hicho. Uso wangu ukiwa umenywea nilimtazama mama yangu na kaka yangu waliokuwa wamekaa katika safu za mbele.

Nikamuona mama yangu anaangua kilio akinililia…

Sauti yake ya kizee ndio iliyoniamsha usingizi. Wakati nazinduka moyo ulikuwa ukinienda mbio na mwili wote ulikuwa umenitota jasho. Nilijiinua kitandani nikaketi.

Nikajiuliza, je ndoto ile ndio inanitabiria hatima yangu, kwamba nitahukumiwa kifungo cha miaka thelathini kama jambazi?

Kama ni hivyo, niliendelea kujiambia, nitafia jela. Sitamuona tena mama yangu, sitamuona tena kaka yangu.

Wazo la kufungwa miaka thelathini lilinifanya nitaharuki. Nikajiambia “…sijui nikimbie nisiende tena kazini…”

Lakini nikajiuliza nitakimbilia wapi katika Tanzania hii ambapo mkono wa serikali hautakuwepo?

Kukimbia ni kama kujidanganya na kuonesha kuwa zile pesa niliiba mimi wakati sivyo, nikajiambia, la msingi ni kwenda kazini, litakalotokea na litokee. Kama ni kufungwa au kuachiwa, ingawa tegemeo la kuachiwa sikuwa nalo.

Mpaka inafika saa moja kamili asubuhi nilikuwa nimeshafika nyumbani kwa kaka. Nilitangulia kwenda kwa mama nikaagana naye. Mama aliniombea Mungu kile ‘kikombe’ kiniepuke.

Nilisubiri kaka ajitayarishe hadi saa moja na nusu ndipo tulipoondoka.

Tulifika kazini saa mbili kama na robo hivi nikaingia ndani na kaka. Tulikwenda katika ofisi ya mhasibu. Mhasibu aliponiona tu akaniuliza.

“Umekuja na pesa?”

Nikatikisa kichwa taratibu.

“Sikufanikiwa bosi”

“Mimi ni kaka yake” Kaka yangu akajitambulisha na kumuuliza mhasibu.

“Mheshimiwa kwani hiwezekani kumkata katika mshahara wake wa kila mwezi hadi hizo pesa zikaisha?”

Mhasibu akakasirika.

“Nyinyi mnaleta utani na kazi. Huu ni wizi, huyu hakukopa pesa hapa hadi tumkate kila mwezi. Shilingi milioni kumi tutamkata kwa miaka mingapi wakati pesa za shirika zinahitajika? Nimeshamwambia kama hakuja na pesa leo atakwenda kujieleza polisi” Mhasibu alifoka na kuinuka kwenye kiti, akaniambia.

“Twende!”

Tukatoka mle ofisini na akawaambia wafanyakazi wengine kuwa tunakwenda kituo cha polisi. Tulikuwa tuna magari mawili ya shirika yenye madereva wake. Tukapanda kwenye gari mojawapo. Kaka yangu tulimuacha pale pale.

Wakati napelekwa polisi na nikijua kuwa ninakwenda kufungwa nilimlaani sana yule aliyeiba zile pesa. Nilipata uchungu nilipowaza kwamba mimi ninakwenda kufungwa, yeye yuko ofisini akiwa ameficha shilingi milioni kumi nyumbani kwake.

Tulikwenda kituo cha polisi cha Chumbageni. Tulipoingia katika kituo hicho mhasibu akatoa maelezo yote kuhusiana na wizi huo.

DUH! JAMAA ANATIA HURUMA KWELI! SI ATAFUNGWA TU HUYU? Jamani Tumuombee mwenzetu, yuko kwenye wakati mgumu.

No comments:

Post a Comment