Saturday, June 25, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 28

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0655 340572

MWANAMKE 28

ILIPOISHIA

Niliporudi ofisini na polisi Zena alikuwa yuko sambamba na mimi hadi zile pesa zipoonekana.

Sasa wakati ule navuka barabara nikiwa na kaka alijipitisha kusudi ili nimuone kisha akapotea.

Nikazinduka usingizini. Wakati nazinduka niliisikia sauti ya Zena ikiniambia.

“Hilo ni onyo!”

Nikadhani kwamba zena alikuwa mule chumbani. Nilipofumbua macho nikainuka na kuketi, nikaanza kutazama huku na huku kwa hofu kwamba ningemuona Zena mle chumbani. Lakini sikumuona.

Nikashuka kitandani na kutoka sebuleni ambako nilikaa kwenye kochi na kuifikiria ile ndoto.

Hapo ndipo nilipoanza kufahamu kuwa zile pesa zilikuwa zimechukuliwa na Zena ili kunikomoa. Nikajiambia kama asingezirudisha ndio ningekiona cha moto.

“Huyu msichana ataendelea kuniamndama hadi lini?” nikajiuliza.

Nilihisi kwamba kama sitachukua hatua thabiti za kuhakikisha kwamba ninaepukana naye, mwisho wake anaweza kunitia katika matatizo makubwa.

Baada ya kufkiri sana nilitoa pikipiki yangu nikaenda kumueleza mama kuhusu ile ndoto. Mama naye alistaajabu.

“Kumbe bado anakufuatilia!” akaniambia

“Huyu jini atakuja kunitia kwenye matatizo makubwa hapo baadaye” nikamwambia mama.

“Sasa fanya mpango wa kwenda huko pemba”

“Inabidi nipate mwenyeji au mtu wa kufuatana naye ndio nitaweza kufika”

SASA ENDELEA

“Ulizia kwa marafiki zako unaweza kupata mtu anayekwenda. Hapa Tanga watu wa Pemba wako wengi” Mama akaniambia.

“Nitaanza kuuliza uliza kwa watu. Nikipata mwenyeji au mtu anayekwenda huko itabidi niende”

Baadaya kuzungumza na mama nilikwenda kwa kaka, naye nikamueleza kuhusu ile ndoto.

“Mimi naamini majini wana matatizo sana na huyo jini hawezi kukuachia kirahisi lakini kwa vile humuhitaji nitakusaidia kukuulizia waganga kwa wenyeji wa Pemba” Kaka akaniambia.

“Na mimi mwenyewe pia nitakuwa naulizia ulizia kwa jamaa”

Ikapita wiki moja. Siku moja ya jumapili kaka yangu akaja nyumbani. Hakuwa na kawaida ya kufika kwangu, hivyo nilipomuona nilishituka.

Akaniambia kulikuwa na mganga aliyetoka Pemba amefikia katika gesti moja pale Chuda. Katika matangazo yake ameeleza pia kuwa anafukuza majini wabaya.

“Nataka twende umueleze matatizo yako anaweza kukusaidia” Kaka akaniambia.

Nilipopata habari zile nilimwambia kaka anisubiri. Baada ya dakika chache tukawa njiani tukielekea Chuda. Nilikuwa nimempakia nyuma ya pikipiki yangu.

Tulipofika Chuda alinipeleka katika gesti alikofikia huyo mganga aliyeniambia. Ilikuwa mtaa wa pili na ule aliokuwa akiishi yeye.

Wale watu niliowakuta hapo nje wakisubiri zamu ya kuingia kwa mganga huyo walinipa matumaini kwamba huyo mganga alikuwa mganga kweli.

Alikuwa ameweka tangazo lake mbele ya gesti lililoandikwa matatizo aliyokuwa akiyashughulikia likiwemo tatizo la majini.

“Ninafukuza majini mabaya katika mwili au nyumba. Pia ninatuliza wale majini wa kichwa wanoleta maradhi na matatizo mengine” Ilisema sehemu ya tangazo hilo.

Mwisho wa tangazo lake aliandika.

“Njoo ujaribu kwani wengi wamefanikiwa. Nitakuwa Tanga kwa siku tatu”

Kutokana na wale watu niliowakuta kuwa wengi nilitaka kumwambia kaka turudi baadaye, watu watakuwa wamepungua lakini nilivyoona pameandikwa kuwa mganga atakuwa Tanga kwa siku tatu nikaamua nisubri hapo hapo.

Siku tatu ni chache sana. Kama ningemkosa siku ile na pengine siku inayofuata, uwezekano wa kumpata tena ungekuwa mdogo sana. Nilijiambia.

Watu tuliowakuta walifikia arobaini. Nilimwambia kaka kama hatakuwa na muda wa kusubiri hapo aende zake.

“Niache niendelee kusubiri hata kama itafika jioni” nilimwambia.

“Sawa, basi wewe subiri ikifika zamu yako utaingia na utamueleza tatizo lako. Ukitoka hapa utakuja nyumbani kuniambia”

Tulipokubaliana na kaka aliondoka akaniacha pale. Mpaka inafika saa nane mchana walikuwa wamebaki watu kumi nikiwemo mimi. Nikaendelea kusubiri hadi saa kumi jioni ndio ikafika zamu yangu.

Nikaingia.

Chumba cha mganga kilikuwa cha kwanza cha mkono wa kushoto. Niliingia katika chumba hicho nikamkuta mganga aliyekuwa amekaa chini kwenye mswala. Kando yake alikuwa amechoma udi wa kijiti uliokuwa unafuka moshi.

Mbele yake kulikuwa na vitabu kadhaa vya kiarabu pamoja na chupa za dawa za kiasili.

Alikuwa amevaa kofia ya darize aliyoiweka katika muundo wa jahazi. Pia alikuwa amevaa shati jeupe na shuka nyeupe. Hakuwa amevaa suruali.

“Karibu” akaniambia alipoona nimesita baada ya kuingia humo chumbani.

“Asante” nikamjibu.

“Kaa kwenye kiti”

Kulikuwa na kiti kilichokuwa kando ya ukuta kushotoni kwake. Nikaenda kuketi.

“Niambie shida yako” akaniambia.

Nikamueleza matatizo yangu mwanzo hadi mwisho.

“Umepata bahati sana. Kule kwetu ukiwa na jini kama huyo tayari unajihesabu kuwa ni tajiri” Mganga akaniambia baada ya kunisikiliza.

“Huko kwenu kuna watu waliooa majini”

“Enhe! Wapo”

“Mimi simuhitaji huyu jini”

“kama wewe umuhitaji ndipo anapokutia kwenye matatizo”

“Ndio nimekuja kwako unisaidie”

“Unataka nikusaidieje?”

“Umuondoe”

“Una uhakika kuwa umuhitaji kabisa, usije ukajuta baadaye”

“Hapana, siwezi kujuta”

“Kwangu mimi si kazi kubwa kama utanipatia vitu ninavyotaka”

“Unataka vitu gani?”

“Ninahitaji kucha zako na kucha za maiti aliyezikwa. Unaweza kuzipata kucha za maiti?”

“Mh! Itakuwa ngumu!”

“Bila kupata kucha za maiti kazi itakuwa ngumu. Nenda kanitafutie kucha za maiti. Ukizipata niletee nitamuondoa huyo jini siku hiyo hiyo. Mimi nikalipo (nitakuwepo) hadi kesho kutwa. Ukiniletea kesho itakuwa bora”

“Bila hizo kucha haitawekana?” nikamuuliza”

Mganga akatikisa kichwa.

“Itakuwa vigumu”

Nikawaza kidogo kisha nikamwambia.

“Basi acha niende nikafikirie nitakavyoweza kuzipata hizo kucha halafu nitakuja hapo kesho”

“Sikiliza. Kucha zenyewe ni lazima ziwe za maiti aliyezikwa si za maiti ambaye hajazikwa”

“Sasa maiti ambaye amezikwa nitampata wapi?”

“Kaburini”

“Yaani nikafukue kaburi?’

“Ndio”

“Si nitaonekana na watu”

“Huendi mchana, unakwenda usiku”

“Mh!” nikaguna nilipofikiria kwenda usiku makaburini na kufukua kaburi.

“kama hutaweza basi, tutakuwa tumeshindwa”

“Nitakupa jibu hapo kesho kama nitaweza au la”

“Kumbuka kwamba nitakuwa hapa Tanga kwa siku tatu. Nikitoka hapa ninakwenda Arusha”

“Nimekuelewa, acha niende. Nitakuja tena kesho”

Nikaagana na yule mganga na kutoka, Nilipanda pikipiki yangu nikaenda nyumani kwa kaka. Kaka mwenyewe sikumkuta, mke wake aliniambia kaka aliondoka tangu saa tisa na hakumwambia anakwenda wapi.

Nikaona niende kwa mama. Nilipofika nilimueleza kwamba kaka alinipeleka kwa mganga aliyetoka Pemba na mganga akanieleza kwamba nimpelekee kucha za maiti.

“Kucha za maiti utazipata wapi?” mama akaniuliza kwa mshangao.

“Tena anataka maiti aliyekwishazikwa”

“Sasa utampataje huyo maiti aliyezikwa ukate kucha zake?”

“Sijui”

“Mh! Hayo ni makubwa”

“Maana yake niende nikafukue kaburi”

“Kaburi gani utakalokwenda kulifukua?”

“Kaburi lolote tu”

“Mh! Si utaonekana ni mchawi!”

“Labda niende usiku”

MAKUBWA! MAMBO SASA NI YA KUFUKUA ,AKABURI! MMH! KAZI  IPO JAMANI!

HAYA TUKUTANE TENA HAPO KESHO TUONE NINI KITATOKEA.

No comments:

Post a Comment