Monday, June 27, 2016

HADITHI , MWANAMKE SEHEMU YA 29

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0713 340572

MWANAMKE 29

ILIPOISHIA JANA

“Yaani nikafukue kaburi?’

“Ndio”

“Si nitaonekana na watu”

“Huendi mchana, unakwenda usiku”

“Mh!” nikaguna nilipofikiria kwenda usiku makaburini na kufukua kaburi.

“kama hutaweza basi, tutakuwa tumeshindwa”

“Nitakupa jibu hapo kesho kama nitaweza au la”

“Kumbuka kwamba nitakuwa hapa Tanga kwa siku tatu. Nikitoka hapa ninakwenda Arusha”

“Nimekuelewa, acha niende. Nitakuja tena kesho”

Nikaagana na yule mganga na kutoka, Nilipanda pikipiki yangu nikaenda nyumani kwa kaka. Kaka mwenyewe sikumkuta, mke wake aliniambia kaka aliondoka tangu saa tisa na hakumwambia anakwenda wapi.

Nikaona niende kwa mama. Nilipofika nilimueleza kwamba kaka alinipeleka kwa mganga aliyetoka Pemba na mganga akanieleza kwamba nimpelekee kucha za maiti.

“Kucha za maiti utazipata wapi?” mama akaniuliza kwa mshangao.

“Tena anataka maiti aliyekwishazikwa”

“Sasa utampataje huyo maiti aliyezikwa ukate kucha zake?”

“Sijui”

“Mh! Hayo ni makubwa”

“Maana yake niende nikafukue kaburi”

“Kaburi gani utakalokwenda kulifukua?”

“Kaburi lolote tu”

“Mh! Si utaonekana ni mchawi!”

“Labda niende usiku”

SASA ENDELEA

“Utaweza kufukua kaburi mpaka uipate maiti kisha uikate kucha?” Mama aliniuliza kwa mshangao.

“Nitajaribu, nikishindwa nitaacha”

“Mh!”

“Sasa nitafanyaje mama?”

“Najua kuwa huna la kufanya”

“Basi ngoja nijaribu”

Nilipoondoka kwa mama nikaanza zoezi la kuzungukia makaburi niliyokuwa nayafahamu. Pale jirani na nyumba niliyokuwa nikiishi paliwa na makaburi lakini yalikuwa karibu na makazi ya watu, ningeweza kuonekana.

Nilikwenda katika eneo la Usagara ambako pia kulikuwa na makaburi. Nikaangalia angalia kisha niliondoka tena nikaenda Gofu. Kulikuwa na makaburi yaliyokuwa kando ya barabara. Mahali hapo ndipo paliponiridhisha.

Laiti ningejua ni balaa gani ambalo ningekutana nalo usiku kwenye makaburi hayo, nisingekwenda na mpango huo ningeuacha kabisa!

Baada ya kupata uamuzi kuwa niende katika makaburi yale wakati wa usiku, nilikwenda katika duka moja la vifaa vya ujenzi nikanunua shepe, viatu vya mvua na mipira ya kuvaa mikononi. Nikavifunga nyuma ya pikipiki yangu kisha nikarudi nyumbani kwangu.

Nilikuwa nimepanga nitoke saa nane usiku ambapo hakutakuwa na watu mitaani na hivyo nisingeweza kuonekana na mtu.

Wakati nimekaa sebuleni nikiwaza nikasikia mlango wa mbele ukigongwa.

Nilisubiri, ulipogongwa tena ndipo nilipoinuka na kwenda kunako mlango huo.

“Nani?” nikauliza.

“Ni mimi Marijani”Sauti ya kaka yangu ikajibu kutoka nje.

Nikafungua mlango.

“Karibu kaka” nikamkaribisha ndani huku nikimpisha kwenye mlango.

Kaka aliingia ndani, nikafunga mlango.

“Umenishitua kidogo” nikamwambia.

“Kwanini?”

“Nilivyokuona umekuja kwangu huu usiku moyo wangu umeshituka”

“Nimekuja na wazo”

“Kaa kwenye sofa” nikamwambia kwa shauku ya kutaka kulisikia wazo alilokuwa amekuja nalo.

“Sitakaa. Nimekuja mara moja tu. Nataka niwahi kurudi”

“Pikipiki ipo nitakurudisha kaka”

“Usijali Amour tunaweza kuzungumza tukiwa tumesimama, sisi bado ni vijana. Tusiogope kusimama”

“Sawa kaka, nieleze hilo wazo ulilokuja nalo”

“Kwanza nilipata salamu kutoka kwa mke wangu kwamba ulikuja nyumbani ulipotoka kwa yule mganga”

“Ndio nilikuja lakini nikaambiwa na shemeji kuwa ulitoka”

“Ni kweli nilitoka, niliporudi ndio nilipata hizo salamu. Nikaenda kumuuliza mama kama ulifika kwake akaniambia ulifika na akanieleza ulivyoelezwa na yule mganga”

“Umeona kuwa mganga wako amenipa mtihani mkubwa”

“Ni mtihani mkubwa. Mama ameniambia ametaka umpelekee kucha za maiti”

“Tena maiti aliyezikwa, yaani niende nikafukue kaburi”

“Sasa mimi nilikuwa na wazo”

“Ndio”

“Kwanini usiwatumie vijana?’

“Kuwatumia kivipi?”

“Yaani unamtafuta kijana wa maskani unampa pesa kisha unamtuma hiyo kazi na unamuahidi kuwa akikuletea hizo kucha za maiti utampa pesa nyingine”

“Ni wazo zuri, sikuwahi kulifikiria wazo hilo”

“Yaani badala ya wewe  kupata kazi ya kufukua kaburi, kazi hiyo unampa yeye. Hawa vijana ukiwapa elfu ishirini tu ya kunywea gongo na bangi wanaweza kukupatia hizo kucha”

“Ni kweli. Nitawatafuta huu usiku”

“Tena makaburi yako pale karibu tu. Kuna vijana wanaovutavuta bangi pale”

“Nashukuru kaka kwa wazo lako, umenisaidia sana”

Baada ya kunipa wazo lake hilo nilimrudisha kaka nyumbani kwake kwa pikipiki yangu.

Wakati narudi nyumbani nikawa nalitafakari lile wazo alilonipa kuona kama lilikuwa la busara.

Kwa upande mmoja wa akili yangu niliona lilikuwa wazo la busara kwa sababu lingenigharimu pesa lakini lingenirahisishia kazi. Badala ya mimi kwenda kufukua kaburi, ningempa pesa mtu mwinginne akanifanyie kazi hiyo.

Wahuni walikuwa wengi tu katika mtaa niliokuwa nikiishi, ningeweza kumtuma mmojawapo na akanifanyia kazi hiyo bila wasiwasi.

Lakini kwa upande mwingine niliona halikuwa wazo zuri. Halikuwa wazo zuri kwa sababu huyo mtu nitakayemtuma hiyo kazi nitamuaminije. Atakaponiletea hizo kucha akaniambia kuwa ni za maiti, nitaaminije kuwa ni kucha za maiti kweli?

Je kama atakwenda kukata kucha zake mwenyewe na kuniletea, nitajuaje?

Muhuni ni muhuni tu, anaweza kuona kazi ya kufukua kaburi ni ngumu na pesa haiachiki hivyo akaenda kujikata kucha zake mwenyewe na kuniletea. Sitaweza kujua kama kucha hizo si za maiti au ni zake mwenyewe.

Hivyo nikajiambia, si vizuri kufanya jambo la kubahatisha. Ni vizuri nifanye jambo la uhakika. Na nitakuwa na uhakika wa kucha hizo endapo nitakwenda mimi mwenyewe kufukua hilo kaburi na kukata kucha hizo.

Nilipofika nyumbani niliingiza pikipiki yangu nikasubiri saa nane ifike. Wakati nimeketi sebuleni nikiendelea kusubiri muda, nikapitiwa na usingizi.

Katika usingizi huo eti nikaota nimekwenda kufukua kaburi. Nikakuta mtoto mchanga aliyezikwa, hana hata kucha, Nikalifukia na kufukua kaburi jingine, hilo nalo nilikuta mtu aliyekuwa amekatwa mikono na miguu. Alikuwa amefariki kwenye ajali ya gari.

Nikalifukia tena na kutafuta kaburi jingine ambalo nilianza kulifukua. Wakati nakaribia kulifikia sanduku mvua ikanyesha kwa kishindo. Kaburi likawa linajaa maji. Kazi ikanishinda! Kutahamaki kulikuwa kunaanza kupambazuka.

Ikabidi niondoke nikiwa nimechukia. Hapo hapo nikazinduka.

Nilitazama saa yangu na kuona ilikuwa saa saba ikielekea kuwa na nusu. Nikaona wakati huo pia ulikuwa muafaka kuondoka. Nikaenda kunawa uso kisha nikarudi sebuleni na kuvaa vile viatu vya mvua kwa ajili ya kujikinga na tope wakati wa kufukua kaburi.

Ile mipira ya mikononi sikuivaa kabisa. Nikatoa pikipiki yangu. Lile shepe nilikuwa nimeshalifunga katika siti ya nyuma ya pikipiki.

Kifaa cha kukatia kucha nilikuwa nimeshakitayarisha. Ulikuwa wembe mpya.

Nikaondoka.

Niliendesha piki piki yangu taratibu hadi nikafika Gofu. Usiku huo kulikuwa kimya. Hakukuwa na gari wala watu waliokuwa wakipita. Nilikuwa na hakika kwamba hakukuwa na mtu yeyote ambaye angeniona.

Nilifika katika lile eneo la makaburi. Nikaiingiza pikipiki yangu ndani ya eneo hilo lililokuwa na mti pamoja na vichaka vidogo vidogo.

Nikaiegesha pikipiki chini ya mti huku nikiangaza macho huku na huku. Mbalamwezi ililiangaza vizuri eneo hilo kiasi kwamba sikupata taabu kuyaona makaburi hayo.

Nilianza kuvaa mipira ya mikononi kisha nikalifungua lile shepe. Nililishika mkononi nikaanza kutafuta kaburi la kuchimba.

Makaburi mengi yalikuwa yamewekewa zege, nikaenda mbele zaidi. Nikakuta kaburi moja ambalo halikuwa limewekewa zege na lilionesha lilikuwa jipya. Huenda kulikuwa na mtu aliyekuwa
amezikwa siku iliyopita.

Nikaanza kulichimba. Kwa vile mchnaga wake ulikuwa laini nililichimba haraka harka huku nikirundika mchanga upande mmoja juu ya kaburi hilo. Shimo lilipokuwa kubwa niliweza kuingia ndani nikaendelea kuchimba.

Baada ya kama nusu saa tu nikawa nimelifikia sanduku lililokuwemo ndani. Nilipofanikiwa kuuondoa mchanga wote uliokuwa juu ya sanduku hilo nikaufungua mlango wa sanduku na kuuacha wazi. Ndani ya sanduku hilo niliona maiti ya mwanamke.

Nikatia mkono mfukoni mwangu na kutoa ule wembe. Niliufungua kwenye karatasi yake nikaushika kisha nikaushika mkono wa ile maiti ya mwanamke. Hapo hapo nikaona mwanga wa tochi unanimulika kutoka juu ya kaburi kisha sauti nzito ikaniuliza.

“Wewe nani na unafanya nini hapa?”

Kwa kweli nilishituka sana. Wembe uliniponyoka. Miguu ikanitepeta. Nikainua uso wangu haraka na kutazama juu ya kaburi hilo.

Nilijuta!

DUH! JAMAA KAFUMWA NA NANI TENA? HAYA ITKUWAJE JAMANI! HUU NI MKASA MWINGINE TENA!

HEBU TUKUTANE TENA KESHO TUONE NINI KITATOKEA.

No comments:

Post a Comment