Sunday, November 30, 2014

Mahafali ya shule ya awali Hill View Korogwe somo kwa wazazi

Kumekucha Blog

Korogwe, WAZAZI na walezi wenye watoto wametakiwa kuwapa malezi mazuri watoto wao na kuwapeleka shule ili kuweza kupata elimu na kuwa msaada  katika maisha yao ya baadae.

Akizungumza na wazazi na walezi wakati wa mahafali ya 14 shule ya awali ya Hill View Korogwe, Padri wa Parokia ya Korogwe, Joseph Sekija, alisema kuna baadhi ya wazazi wanashindwa kutambua kuwa elimu ndio msingi wa maisha ya kila mtu.

Alisema kuna wimbi la watoto mitaani wakiwa wamezagaa na chanzo ni  wazazi kutowapa matunzo na  kuwapeleka shule na hivyo kujingiza katika magenge ya wabwiaji unga na waporaji wa wizi wa mifukoni.

“Leo toka nifike hapa nimekuwa na bumbuwazi na kushindwa kupata majibu---sijaona shule ya awali kufanya mahafali kama haya---watoto wamependeza na huu ni mfano kwa shule nyengine za awali” alisema Sekija

“Kwa vile hapa wapo wazazi na walezi ni nafasi ya kukumbusha na kupelekeana salamu kwa ambao hawapo---tutambue kuwa elimu ndio msingi wa mambo yote hivyo kila mmoja wetu kumpeleka mtoto wake shule kwa wakati na kufuatilia maendeleo shuleni” alisema

Aliwataka wazazi na walezi kuhakikisha wanafuatilia maendeleo ya watoto wao shuleni na kuacha kusubiria ripoti za mwisho wa mwaka jambo ambalo linaweza kuchangia kuwa na matokeo mabaya.

Akizungumza katika mahafali hayo, Mkurugenzi wa shule hiyo ya awali, Silvester Mgoma, amewataka walimu kuzidisha bidii darasani lengo likiwa ni kuibua vipaji na kuweza kutoa vijana wenye akili.

Alisema walimu wako na mchango mkubwa kwa kushirikiana na wazazi katika kuwajenga katika misingi ya maadili ya kiroho na hivyo kuwataka kushirikiana ili kuibua vijana wenye vipaji.

“Mimi nasaha yangu kwenu wazazi na walimu ni kudumisha ushirikiano na mahusiano mema ili kuwajenga watoto wetu katika maadili mema ya kiroho shuleni na majumbani” alisema Mgoma

Alisema endapo kutakuwepo mahusiano mema ya  pande mbili hizo ni wazi kuwa Taifa litakuwa na vijana wenye elimu na vipaji na kuondokana na tatizo la uhaba wa  fani ikiwemo ya sayansi.

                                               Mwisho

No comments:

Post a Comment