Thursday, November 20, 2014

Watafutwa kwa mauaji, Kilindi



Kumekucha Blog, Tanga

Tanga,JESHI la polisi Wilayani Kilindi Mkoani Tanga linawatafuta watu wawili kwa tuhuma za kumuuwa mtoto wa jamii ya wafugaji, Said Omar (19) na kisha  maiti yake kuitundika juu ya mti wa mkunazi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, kamanda wa polisi Mkoani Tanga, Fresser Kashai, alisema tukio hilo lilitokea juzi sa 1 usiku katika bonde la Kimbe kijiji cha Nyadigwa tarafa ya Kibirashi.

Alisema watu waliofanya kitendo hicho waliichukua maiti ya mtoto huyo na kuining’iniza juu ya mkunazi  kisha kutokomea kusikojulikana na hivyo polisi inaendelea kufanya uchunguzi pamoja na  kuwasaka wauaji  hao.

“Tunaendelea kuwasaka waliohusika na taarifa za awali ni kuwa wamekimbilia milimani na wamekuwa wakirejea majumbani kwao nyakati za usiku----tuna uhakika tutawatia mbaroni” alisema na kuongeza

“Kitendo ambacho wamekifanya ni cha kikatili na hakikubaliki katika jamii---tutahakikisha tunawatia mikononi na kuwafikisha katika vyombo vya sheria” alisema Kashai

Akizungumzia kuhusu jamii kuishi kwa maelewano na kushirikiana kwa kila jambo, kamanda Kashai aliwataka wafugaji na wakulima kuwa na utaratibu wa kukutana kila baada ya mwezi mmoja kuzungumza changamoto wanazokabiliana nazo.

Alisema jamii  hizo zinapaswa kuwa na utaratibu wa kukutana mara kwa mara kujadili na kuzungumza changamoto ambazo wamekuwa wakikumbana nazo  jambo ambalo litasaidia kuondosha vitisho vya uhasama.

“Haya matukio ya ugomvi ugomvi wa wakulima na wafugaji tatizo ni kuwa hakuna utaratibu wa kukutana na kujadili mambo yawahusuyo hasa mashamba na mifugo” alisema

“Kama kungelikuwa na utaratibu huo katu tusingelisikia ugomvi pande mbili hizi popote katika ardhi yetu ya Tanzania---hivyo natoa ushauri Serikali za vijiji kuandaa mikutano hiyo nasi kama polisi tutaibariki” alisema Kashai

Kamanda Kashai alisema mikutano hiyo polisi kwa kushirikiana na vyombo vyengine vya usalama vitashirikiana na wakulima na wafugaji kuandaa mikutano hiyo lengo likiwa ni kuleta mahusiano mema pande mbili hizo.

                                                       Mwisho

No comments:

Post a Comment