Thursday, November 20, 2014

Watatu wadakwa na dola bandia

Kumekucha Blog, Tanga

Tanga, POLISI kituo kikuu cha Chumbageni Tanga inawashikilia watu watu kwa tuhuma za kupatikana na noti bandia za Kimarekani Dola 11,200 wakati wakiwa katika harakati za kuzibadilisha kwa wabadilishaji wa pesa za mikononi kituo kikuu cha mabasi Tanga.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, kamanda wa polisi Mkoani Tanga, Freisser Kashai, alisema tukio hilo lilitokea juzi saa 5 asubuhi eneo la kituo cha mabasi yaendayo Mombasa nchini Kenya.

Aliwataja watuhumiwa hao kuwani, Julias Kanza(30), Kenedy Binagi(35) na Saddy Muha (33) wote wakiwa ni wakazi wa Ubungo jijini Dar es Salaam na kudai kuwa walikiri kufanya biashara ya pesa za bandia kwa muda mrefu.

Alisema wakati wakiwa katika harakati za kubadilisha pesa hizo mmoja wa watu wanaobadilisha aliweza kutilia shaka pesa hizo hasa kikiwa ni kiwango kikubwa kwa pesa za mikononi na hivyo kupiga simu polisi kwa kutarifu juu ya pesa hizo.

“Mmoja wa kijana wanaobadilisha pesa pale kituo cha mabasi yaendayo Mombasa alizitilia shaka  kwani kwanza nikiwango kikubwa na pili pesa ya kubadilishana ilikuwa ndogo sana” alisema na kuongeza

“Dola za kimarekani elfu kumi na moja sio kiwango kidogo kwa pesa za kubadilisha  juu juu tena kituo cha mabasi----ile yatosha kwa yoyote kutilia shaka na ndio maana mmoja wa wafanyabiashara alishtuka na kupiga simu polisi” alisema kamanda Kashai

Kamanda alisema mahojiano ya awali na watuhumiwa hao wamekiri kufanya biashara hiyo haramu ya kubadilisha pesa za bandia na wamekuwa wakitumia vituo vya mabasi na mipaka  ya nchi jirani  ukiwemo mpaka wa Horohoro.

Alisema uchunguzi utakapokamilika watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili ili kuwa fundisho kwa watu wengine wenye tabia kama hiyo.

Akizungumzia wafanyabiashara kuzitumia taasisi za fedha yakiwemo mabenki katika kubadilisha na kuweka pesa zao ili kuepusha utapeli na wizi, Kashai alisema wizi huo utakoma.

Alisema matapeli wengi wamekuwa wakitumia mwanya huo baada ya kuona wafanyabiashara na matajiri wamekuwa wakibadilisjha pesa kienyeji na hivyo kuwa rahisi  kutekeleza vitendo vya kitapeli.

“ Watu wengi hawatumii mabenki na taasisi za fedha katika kubadilisha na kuweka pesa zao na hivyo matepeli kuutumia mwanya huo kutekeleza unyang’anyi” alisema Kashai

Alisema ili kuweza kutokomeza na kuziba mianya ya kitapeli amewataka kuyatumia mabenki katika kupadilisha na kuweka ili kuepusha utapeli na kuweza kuwa na uhakika wa kufanya biashara zao.

                                     Mwisho

No comments:

Post a Comment