Friday, November 21, 2014

Waiomba Serikali kulegeza masharti ya leseni ufunguaji wa kampuni



Kumekucha Blog

Tanga,WAHITIMU wa mafunzo chuo cha Ufundi  Ustadi (Veta) Tanga wameitaka Serikali kulegeza masharti ya leseni kufungua kampuni lengo likiwa ni kuweza kujiajiri ili ujuzi wao usiwe wa mifukoni na makabatini.

Wakizungumza wakati wa mahafali ya 38 chuoni hapo jana, wahitimu hao wamesema kwa sasa ni vigumu kupata ajira Serikalini na hivyo kutaka ujuzi wao kuweza kuutumilia kwa kufungua makampuni yao na kuweza kuisaidia Serikali katika kutoa ajira.

Wamesema kufanya hivyo kutawawezesha kutoa ajira kwa wengine wasio na kazi jambo ambalo litasaidia kupunguza vijana wasio na kazi mitaani pamoja na watumiaji wa madawa ya kulevya na waporaji wa kutumia nguvu.

“Tuko na furaha ya kuhitimu kozi zetu ila changamoto kubwa iko katika kupata ajira iwe serikalini ama taasisi binafsi----hii ni kutokana na kuwa na wasomi wengi wasio na kazi” alisema Devid Elias

“Jambo zuri ambalo Serikali inatakiwa kufanya hasa sisi ambao tumetokea katika vyuo ni kutulegezea masharti ya upatikanaji wa leseni za kampuni----itakuwa msaada kwetu na vijana wasio na kazi”alisema Elias

Kwa upande wake mhitimu wa kunyoosha bodi za magari, Rose John, amewataka wanafunzi wanaomaliza elimu ya msingi na sekondari kuacha kukata tamaa na badala yake wajiunge na vyuo vya ufundi.

Alisema kuna wanafunzi wengi ambao humaliza elimu ya sekondari wamekuwa wakikata tamaa ya masomo na kusahau kuwa viko vyuo vya ufundi ambavyo vinaweza kuwatoa kimaisha kama vilivyo vyuo vyengine.

“Tatizo hasa liko kwa wazazi mtoto anapoamaliza naona ndio mwisho wa masomo na kumuingiza katika biashara au kumuacha akipotea---wanasahu kuwa viko vyuo vya ufundi” alisema Rose

Aliwataka wazazi kukumbuka kuwa vyuo vya ufundi vinaweza kuwabadilisha watoto wao katika maisha yao mbeleni pamoja na ya kwao na hivyo kutambua kuwa elimu na ujuzi sio wa shuleni peke yake.

Aliwakumbusha kuwa kumuacha mtoto wakati yuko na elimu ya kiwango cha chini ni jambo la hatari linaloweza kuwatumbukiza katika magenge ya kihuni pamoja na biashara haramu za uuzaji unga na uvutaji bangi.

                                                      Mwisho

No comments:

Post a Comment