Sunday, December 13, 2015

MBUNGE WA MLALO AKEMEA VITENDO VYA UKATILI



Tangakumekuchablog
Mlalo, MBUNGE wa jimbo la Mlalo, Rashid Shangazi (CCM), ameitaka jamii kuishi kwa upendo na ushirikiano na kukemea vitendo vya ukatili na migogoro isiyo na tija.
Akizungumza na waandishi wa habari jana kufuatia tukio la kukatwa kidole gumba mwelemavu wa ngozi (Albino), Ester Maganga (69) mkazi wa kijiji cha Bangoi kata ya Pea Mlalo juzi, Shangazi alisema kitendo hicho kinafaa kulaaniwa na kutoruhusu kutokea tena.
Alisema waliofanya hivyo ni wahuni ambao wanatakiwa kukamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria  na kuwa fundisho kwa watu wengine wenye tabia kama hiyo.
“Tumesikitishwa na wahuni waliomkata bibi yetu kidole na kutoweka nacho----tukio hili ni la kwanza kutokea kwani tulikuwa tunayasikia tu kupitia vyombo vya habari” alisema Shangazi na kuongeza
“Nawaomba viongozi wa Serikali na jeshi la polisi kwa pamoja kuwasaka watu waliofanya kitendo hicho na kukomeshwa kabisa kwani kimetutia kiwewe---natambua kuwa ni watu wa nje ya hapa” alisema
Shangazi ameitaka jamii kupendana na kuishi kwa kushirikiana kwa kila jambo na kuacha mitafaruku ambayo haina tija na kujikita zaidi katika masuala ya maendeleo.
Akizungumzia kuhusu watu kujiunga na mifuko ya Hifadhi ya  jamii, Shangazi alisema ameitaka mifuko hiyo  kufika katika jimbo lake na kutoa elimu ya upatikanaji wa matibabu bure.
Alisema gharama za matibabu ni kubwa jambo ambalo kwa kiasi kikubwa inapelekea maisha ya wananchi kuwa magumu siku hadi siku kutokana na makali ya matibabu.
“Gharama za matibabu ni kubwa sana kulingana na kipato cha mwananchi kwa siku moja----nitaishawishi mifko ya hifadhi ya jamii kuja na kutoa elimu ya upatikanaji wa matibabu bure” alisema
Alisema maendeleo yamekuwa yakishuka siku hadi siku kutokana na pesa nyingi kwenda kwenye matibabu na hivyo kuitaka mifuko ya hifadhi ya jamii kufika jimboni humo na kutoa elimu kwa makundi mbalimbali yakiwemo ya wakulima.
                                                       Mwisho

No comments:

Post a Comment