Saturday, June 11, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 17

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0655 340572

MWANAMKE 17

ILIPOISHIA

Pakapita ukimya wa sekunde kadhaa. Bibi alikuwa akiendelea kusuka ukili wake na mimi nilikuwa nikiumiza kichwa kwa kuwaza. hatimaye nikauondoa ule ukimya.

“Kwa mfano mimi nikipata mke wa kijini, unanishaurije nioane naye?” nikamuuliza.

Bibi akacheka.

“Bibi mbona unanicheka?”

“Unanichekesha. Huyo mke wa kijini utampata wapi?”

“Kwani babu alimpata wapi?”

“Yule ni mpaka akuchunuke mwenyewe”

“Sawa. Je akinichunuka na kuniambia anataka tuoane, nikubaliane naye?”

“Hayo ni mawazo yako sasa, mimi nikushauri nini?”

“Unaweza kunishauri kwamba nioane naye au la”

“Hilo sio jambo la kushauriwa, ni uamuzi wako na huyo jini kama utampata. Kwani na wewe unataka kupata utajiri?”

“Hakuna asiyetaka utajiri bibi”

“Angalia sana, utajiri mwingine una matatizo. Ni bora uishi masikini hivyo hivyo”

Baada ya kimya kingine kifupi nikamuaga bibi. Wakati nataka kuondoka nikampa shilingi elfu ishirini. Bibi akanishukuru.

“Haya bibi nakwenda” nikamuaga bibi na kupanda pikipiki yangu.

“Uende salama, nisalimie wenzako”

“Nitakusalimia”

SASA SONGA NAYO

Nikawasha pikipiki yangu na kuondoka. Wakati narudi mjini mawazo yalikuwa yamesonga katika kichwa changu kuhusu yale maneno  aliyonieleza bibi.

Sikuwa nikijua kama babu yangu alimuacha mke wake na kuoa mke wa kijini. Kwa vile babu mwenyewe alikufa zamani habari zake zilikuwa zimeshahaulika.

Lakini nilijiuliza Zena alijuaje habari ile? Nikawa na shaka sana kwamba huyo Zena aliyetajwa na bibi ndiye Zena yule yule.

Nikakumbuka kwamba aliniambia alikuwa na mimi kwa miaka mingi isipokuwa hakuwa amejitokeza kwangu hivyo nilikuwa sijui kama nina jini aliyenichunuka.

Pamoja na kufahamu ukweli wote huo bado nilikuwa na mtihani mgumu mbele yangu, mtihani wa kukubali kuoana na Zena kama alivyoniambia au kumkataa.

Mpaka muda ule naondoka kwa bibi sikuwa na uamuzi wowote. Nilitegemea kupata ushauri kwa kaka yangu na kwa mama yangu.

Nilikwenda moja kwa moja nyumbani kwa kaka. Nikamwambia.

“Ninatoka Mwambani kwa bibi”

“Umezungumza naye?” akaniuliza kwa shauku.

“Nimezungumza naye na anawasalimia”

“Amekuelezaje kuhusu madai ya babu kuoa mke wa kijini?”

“Amesema ni kweli, babu alioa mke wa kijini baada ya kumuacha yeye”

Kaka akashituka.

“Kumbe babu alioa mke wa kijini!”

“Tena alikuwa anaitwa Zena, jina lile lile la huyu anayenifuata mimi”

Kaka alikuwa amepigwa na butwaa.

Nikamueleza kwa kirefu maelezo ya bibi ambayo yalimshangaza sana.

“Isije kuwa jini huyo ndiye huyu huyu amejitokeza tena”

“Hata mimi nimekuwa nikijiuliza swali hilo hilo”

“Huyo bibi alikwambia aliwahi kumuona?’

“Ameniambia hakuwahi kumuona”

“Mimi nadhani jini mwenyewe ndiye huyo huyo, amejitokeza kwako”

“Inawezekana lakini nitakuja kumuuliza tupate uhakika”

“Sasa umeamua nini?”

“Bado ninakabiliwa na maswali mengi. Ninahitaji ushauri wenu ili niweze kuamua”

“Nenda nyumbani umueleze mama, usikilize atakwambia nini”

“Kwa upande wako unanishauri nini?”

“Hili ni suala la kujadiliana sote kwa pamoja lakini kwanza nenda kamueleze mama tusikie kauli yake”

“Sawa. Nitakwenda kumueleza mama”

Baada ya kuzungumza kirefu na kaka nikaondoka nyumbani kwake na kwenda nyumbani kwa mama.

Wakati nafika nyumbani, mama alikuwa amelala. Mjukuu wake alikwenda kumuamsha chumbani. Alipoamka akaja sebuleni.

“Shikamoo” nikamwamkia.

“Marahaba. Habari za huko?” Mama akaniuliza.

“Huko ni kwema. Natoka Mwambani kwa bibi?”

“Ndio ulikwenda kumuuliza kuhusu babu yako?”

“Nimemuuliza ameniambia kwamba babu yetu alimuacha yeye akaoa mke wa kijini”

“Unaniambia ukweli mwanangu?” Mama akaniuliza kwa mshituko.

“Ameniambia bibi mwenyewe”

“Kumbe babu yako alioa mke wa kijini?”

“Alioa, na bibi anasema waliishi pamoja hadi babu alipofikiwa na umauti, yaani wiki moja kabla ya babu kufariki jini huyo alitoweka”

“Kama ni hivyo inaelekea babu yenu alikuwa mtu hatari sana!”

“Bibi ameniambia babu alipomuoa jini huyo alipata utajiri mkubwa, yaani yule jini alimpa utajiri lakini alipokufa utajiri wake ukapotea”

“Hata kama alipata utajiri, si jambo la kukubaliana nalo kirahisi”

“Sasa kitu ambacho kimenitisha ni kuwa huyo jini alikuwa anaitwa Zena kama jini huyu anayenifuata mimi!”

“Isije kuwa ndiye jini huyo huyo. Kwanini alikuwambia uende ukamuulize bibi yako”

“Inawezekana ndiye jini huyo huyo”

“Sasa sikiliza mwanangu, huyo jini epukana naye mara moja!”

“Kwanini mama?”

“Atakuharibia maisha yako, kama ni kuoa oa binaadamu mwenzako si jini”

“Kwa hiyo unanishauri hivyo?”

“Inawezekana ni ushauri au ni amri yangu na naomba unisikilize”

“Sawa, nitakusikiliza. Nilitaka tu nijue una maoni gani”

“Atakapokufuata tena mwambie mimi siwezi kukuoa wewe, nitaoa binaadamu mwenzangu. Kwani majini madume hakuna mpaka akufuate wewe!”

“Ndio nashangaa!”

“Huyo mke wa kijini kweli utamuonesha kwa wa watu, uwambie mke wangu huyu!”

“Hiwezekani”

“Kwanza watu watakushangaa na hawatakuja kwako. Mimi pia sitakuja”

Mama alikuwa amekasirika, sikutaka tena kumjibu kitu. Nikanyamaza kimya.

“Upuuzi mtupu! Amekutia katika misuko suko chungu nzima halafu uje uishi naye kama mke wako, kwanza hao watoto mtakaozaa watakuwa ni watoto wa aina gani...epukama na huyo shetani asikuletee mikosi. Kama ndiye huyo aliyeolewa na babu yako atokomee huko huko alikokuwa. Mimi simtaki!” Mama aliendelea kuniambia kwa hasira.

“Sawa mama nimekusikia”

Nilipoondoka kwa mama nikarudi nyumbani kwangu. Kusema kweli nilikuwa na mawazo mengi sana. Maneno ya mama yalikuwa yameingia akilini mwangu na wakati huo huo nilikuwa nafikiria endapo nitamueleza yule jini kwamba siwezi kuoana naye atanifanya nini.

Wakati naendelea kutafakari nikasikia mlango wangu wa mbele unabishwa. Nikanyanyuka na kwenda kuufungua.

Nilimuona mzee mmoja aliyekuwa amevaa koti jeusi na kanzu ya darizi pamoja na baraghashia. Nikamuamkia.

“Shikamoo mzee?”

“Marahaba, waonaje hali yako?”

“Nzuri, karibu”

“Asante. Nadhani hunifahamu?” akaniuliza.

“Ndiyo sikufahamu mzee wangu”

“Ninaishi mtaa wa pili. Kuna mwanangu mmoja ndiye aliyenielekeza hapa kwako”

“Una tatizo gani?” nikamuuliza kistaarabu.

“Unakumbuka jana majira ya saa nne asubuhi mpaka tano ulikuwa wapi?”

“Nilikuwa maeneo ya mjini”

“Bila shaka ulikuwa umekaa katika Bustani ya Uhuru na msichana mmoja?”

“Ndio nilikuwa nimekaa hapo”

“Nimeambiwa kwamba wakati yule msichana uliyekuwa naye anaondoka, kuna vijana wawili waliokuwa na baiskeli walimpora yule msichana mkoba wake na kukimbia nao, ni kweli?’

“Ni kweli’

“Yule mzee alinyamaza kimya akitafakari kwa sekunde zisizopungua tano kisha akaniuliza.

“Huyo msichana ni nani wako?”

“Tunafahamiana tu, tulikuwa tumekaa tunazungumza”

“Sasa nataka kukueleza kitu kimoja. Mmoja wa wale vijana waliompora huyo msichana ni mwanangu. Jana usiku aliporudi nyumbani hatukulala”

“Kwanini?”

“Yule kijana alipoingia chumbani mwake tulisikia anapiga kelele. Mimi nikaenda kumuuliza ana matatizo gani, akaniambia kwamba kila anapopitiwa na usingizi anamuona mwanamke anampiga bakora. Nikamuuliza ni mwanamke gani huyo, ndio akanieleza kwamba kuna mwanamke walimpora mkoba wake na ndiye huyo anayemuona anampiga bakora.

“Hiyo hali iliendelea hadi asubuhi, kila akifumba macho tu anamuona, anamtandika. Bakora zimeota mgongoni mwake. Huyo mwanamke haonekani, anamuona yeye tu pale anapolala.

“Hii asubuhi tukaenda kwa huyo mwenzake, kumbe na yeye hali ni hiyo hiyo. Amepigwa bakora usiku kucha. Bakora zimeota kwenye mgongo wake. Kwa kweli nimewagombesha sana wale vijana kwa kututia aibu sisi wazazi wao kwa kujihusisha na vitendo vya kihalifu wakiwa bado wadogo, kuibia watu, kupiga watu na kuvuta bangi. Imebidi niwaulize ni mwanamke gani huyo waliyempora mkoba wake ndipo mwanangu aliponielekeza kwako. Kumbe alikuwa anakufahamu.

“Sasa mwanangu nimekuja, nakuomba unioneshe yule mwanamke nimlipe ule mkoba wake na nimuombe radhi ili wale vijana waondokewe na ile hali”

Yale maneno aliyonieleza yule mzee yalinishangaza na kunishitua. Wakati yule mzee ananieleza mimi nilikuwa natokwa na jasho.

“Kwani mpaka hii asubuhi wanaendelea kuchapwa bakora?’ nikamuuliza.

“Labda wakae bila kusinzia au kulala. Wanapolala kidogo tu tayari wanapiga kelele wanasema wanachapwa. Ni mpaka hii asubuhi hawajalala tangu jana wako macho tu. Wameshadhoofika. Kama hii hali itaendelea watakufa”

“Mzee wangu nikwambie ukweli, yule mwanamke tulikutana pale pale. Sijui anapoishi na sidhani kama nitamuona tena”

MMMH! MAMBO HAYO!!! LOH KUMBE YULE MWANAMKE BALAA!!! KWAKWELI ANATISHA!!! HAYA HAWA VIJANA WA WATU ITAKUWAJE JAMANI!!! MIMI MWENYEWE NIMESHIINGIA UOGA.

No comments:

Post a Comment