SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0655 340572
MWANAMKE 19
ILIPOISHIA
Wakati huo eneo hilo la Mnyanjani lilikuwa kama
kitongoji cha mji huo. Likiwa karibu na ufukwe wa Bahari ya Hindi, lilikuwa
moja ya maeneo ya kiasili ya mji wa Tanga yenye historia iliyosheheni utamaduni
wa jiji hilo.
Eneo hilo
hivi sasa limebadilika na kuwa na nyumba za kisasa na kuwa sehemu ya jiji hilo.
Ili ufike Mnyanjani unapita vitongoji kadhaa pamoja na
viunga vya minazi. Ni mwendo wa karibu kilometa kumi.
Mama alinionesha nyumba ya
mganga huyo iliyokuwa imejengwa kwa miti na udongo na kuezekwa makuti ya
minazi.
Tukasimama na kubisha mlango.
“Karibuni” tukasikia sauti ya
kiume ikitukaribisha.
Tukaingia ndani. Ukumbi ulikuwa giza. Kulikuwa na mwanga hafifu uliotokea
kwenye mlango wa nje na wa uani.
Mganga mwenyewe alikuwa
amekaa kwenye jamvi lililokuwa limetandikwa pale ukumbini. Alikuwa akikatakata
mizizi ya dawa.
“Karibuni” akatuambia tena
huku akitutazama.
“Tumeshakaribia” mama
akamwambia na kisha
kumuuliza hali.
Mimi nikamuamkia. “Shikamoo”
“Marahaba. Karibuni mkae
kwenye jamvi”
Tukakaa kwenye jamvi.
“Tumekuja tuna shida” Mama
akaanza kumwambia mzee huyo aliyekuwa amevaa kikoi cha rangi nyeupe.
“Shida gani?”
SASA ENDELEA
Mama akamueleza mkasa mzima.
Yule mganga naye alishangaa akasema.
“Huyo atakuwa Ummi Subian au
Kamari wa Subian”
“Tunataka aondoke kwa
mwanangu, asimfuate fuate tena”
“Ngoja nimtazame nijue ni
jini gani”
Mganga akachukua kitabu
akakifungua kisha
akatazama saa yake.
“Ni saa nane sasa” alisema
peke yake kisha
akatazama kwenye kitabu.
“Aliyetawala muda huu ni
Zuhra Kadhi Lhawaiju” Mganga aliendelea kujisemea kisha akatutazama.
“Huyu mwanamke wa kijini ni
ruhani aliyechanganya na usubian”
“Yeye mwenyewe pia aliniambia
hivyo hivyo” nikamkubalia mganga huyo.
“Hawa majini ni
ving’ang’anizi sana na ni wabishi, akitaka jambo lake
ni mpaka alitimize”
“Lakini ataweza kumuacha huyu
mwanangu?” Mama akamuuliza kwa wasiwasi.
“Ni kazi kubwa. Huyu jini ni
wa kurithi, zamani aliwahi kuwa na babu yake huyu kijana”
“Ni kweli, bibi yangu
alinieleza leo” nikamwambia mganga huyo.
“Alikuelezaje?”
“Aliniambia kuwa babu yangu
alikuwa na mke wa kijini, anaitwa Zena”
Mganga akamtazama mama.
“Unasikia. Sasa kumtoa jini
wa aina hii inataka kazi kubwa, si kazi ndogo”
“Sasa tufanyeje?” Mama
akamuuliza.
“Nitahitaji mbuzi watatu, wa
rangi nyeupe, rangi nyeusi na rangi mchanganyiko” Mganga alituambia kisha akatuuliza.
“Mtaweza kuwapata?”
“Watapatikana” nikajibu mimi.
“Mbali na hao mbuzi watatu,
mnipatie maji ya bahari lita tatu, mchanga wa pwani unaofikia kilo moja na
kipande cha mti kilichotoka katika eneo lililopiganwa vita”
“Hicho kipande cha mti
tutakipata wapi?” nikamuuliza.
“Najua hiki kitawapa tabu,
nitawapatia mimi”
“Huo mchanga wa pwani na maji
ya bahari pia ungetusaidia wewe, tunaona hapa ni karibu na bahari”
“Gharama yake itakuwa
shilingi elfu kumi na tano”
“Sawa.Tutatoa”
“Hao mbuzi watatu pia mnaweza
kuwapata hapa hapa kama mtataka”
“Watakuwa kiasi gani?”
“Kila mbuzi mmoja ni shilingi
elfu arobaini”
“Kwa hiyo kwa mbuzi watatu
itakuwa shilingi laki moja na ishirini elfu”
“Ingiza na hizi elfu kumi na
tano za vifaa”
“Zitakuwa laki moja na
hamsini na tano elfu”
“Na kazi yangu shilingi laki
moja”
“Jumla laki mbili na hamsini
na tano elfu”
“Hizo pesa zikipatikana,
njooni niwafanyie kazi yenu”
“Pesa zipo lakini zipo
nyumbani, labda utupe muda nikazichukue” nikamwambia mganga huyo.
“Hizo pesa nikizipata leo,
kwanza nitashughulikia kupata hivyo vitu, Kesho saa mbili asubuhi ndio
nitakushughulikia wewe mwenyewe”
“Sawa. Sasa acha turudi.
Baadaye nitakuja na hizo pesa.
Baada ya kukubaliana na
mganga huyo tuliondoka. Nilimpakia mama kwenye pikipiki nikamrudisha nyumbani
kwake kisha
mimi nikaenda nyumbani kwangu kuchukua hizo pesa. Zilikuwa ni pesa zile zile
alizonipa Zena.
Nilitia mfukoni shilingi laki
tatu nikaondoka tena na pikipiki kwenda Mnyanjani. Nilipofika nilimpa yule
mganga shilingi laki mbili na hamsini na tano elfu.
“Sasa nenda, uje kesho saa
mbili asubuhi, utakuta kila kitu kipo tayari” Mganga akaniambia.
“Sasa nilikuwa na ombi moja”
nikamwambia.
“Ndio”
“Nina wasiwasi huyo jini
anaweza kunifuata hii leo kutokana na hivi ambavyo nataka kumshughulikia, sasa
itakuwaje?
“Nitakupa hirizi, kuwa nayo
mfukoni hadi hapo kesho”
“Nikiwa na hiyo hirizi
hatanifuata?’
“Abadani.
Hawezi kukufuata”
“Basi nipatie hiyo hirizi’
Hirizi yenyewe ilikuwa
imeshatayarishwa tayari. Mganga akanipatia. Nikaichukua na kuitia mfukoni.
Nikatoka na kupanda pikipiki
yangu. Sasa kidogo moyo wangu ulikuwa na matumaini. Ile hofu niliyokuwa nayo ya kukutana na Zena
ilikuwa imenitoka.
Wakati nakaribia kulitoka
eneo la Mnyanjani, niliona mtu amesiamama
pembeni mwa barabara chini ya mti wa mwembe. Nilipoukaribia mwembe huo
nilishituka nilipoona mtu mwenyewe alikuwa
Zena. Alikuwa amesimama kama
aliyekuwa akisubiri mtu.
Nikaongeza mwendo ili
kumkwepa na nikajifanya sikumuona. Wakati pikipiki imeshika kasi nikahisi kama kulikuwa na kitu nyuma yangu. Nikageuza uso wangu
kutazama nyuma. Nilishituka tena. Alikuwa ni Zena aliyekuwa amekaa kwenye siti
ya nyuma ya pikipiki yangu!
Sikuweza kujua alipakiaje
kwenye pikipiki yangu wakati alikuwa amesimama
kwenye mti ambao nilikwishaupita, tena nikienda kwa kasi. Kutokana na mshituko nilioupata
mikono yangu ilitetereka nikajikuta ninaanguka na pikipiki. Mimi na Zena tukawa
chini!
Nikainuka haraka. Lakini Zena
alikuwa mwepesi zaidi. Nilimkuta tayari ameshasimama.
DUH! JAMAA AMEKWAMA! KAPEWA
HIRIZI LAKINI JINI KAMTOKEA HIVYO HIVYO. Sijui itakuwaje?
Kama kawaida kwa leo tunaishia hapa lakini kesho
panapomajaliwa tutakuwa tena uwanjani. Usikose kututembelea. Ni TANGA
KUMEKUCHA,
No comments:
Post a Comment