Friday, March 20, 2015

HADITHI SEHEMU YA (3)

 
NILIJUA NEMEUA (3)
 
ILIPOISHIA
 
Habours ilikuwa klabu ya starehe ambayo ilikuwa ikitumiwa kwa maonesho ya miziki hasa miziki ya taarab.
 
“Unataka nikufuate hapo Habours Club?”  nikamuuliza.
 
“Ndiyo”
 
“Nikupeleke wapi?”
 
“Nyumbani”
 
“Ulikuwa kwenye mziki?”
 
“Ndiyo”
 
SASA ENDELEA
 
Nilisita kumpa jibu. Kwa upande mmoja sipendi kukatisha usingizi wangu kwani nilihitajika kuamka saa kumi na mbili asubuhi niingie kazini. Kurudi kwangu nyumbani ni saaa sita au saba usiku.
 
Lakini kwa upande mwingine sikutaka kumkatisha tamaa mteja wangu. Kwa vile ilikuwa ni kazi ya usiku nilijua ingeniingizia pesa nzuri. Nikaona nimfuate.
 
“Unasemaje, utanifuata?”  Sauti ya Mariam ikakatisha mawazo yangu.
 
“Mko wangapi?” Nikamuuliza ili kupanga masilahi yangu.
 
“Tuko wawili, mimi na rafiki yangu”
 
“Nisubirini, nakuja”
 
“Sasa ukifika nipigie unishitue kwani tuko ndani”
 
“Sawa, nitakupigia”
 
Mariam akakata simu.
 
Niliondoka kitandani na kuanza kuvaa. Nilikuwa nikiishi eneo la Msambweni kwenye nyumba yangu mwenyewe. Ilikuwa nyumba ya urithi. Tuliirithi mimi na mdogo wangu wa kiume baaada ya baba yetu kufariki dunia.
 
Mdogo wangu Kabwe naye hakumaliza hata miaka miwili akafariki. Alifariki Afrika Kusini alikokwenda kutafuta maisha.
 
Nilipta habari kuwa alipigwa na kuuawa na wenzake na kisha kuzikwa huko huko na serikali baada ya ndugu zake kutoonekana.
 
Mimi nilikuja kufahamishwa na marafiki zake walionipigia simu kutoka Capetown. Wakaniambia kuwa Kabwe aliuawa na kuzikwa huko huko.
 
Baada ya kifo cha Kabwe nikaimiliki mimi nyumba yetu. Ilikuwa na vyumba sita vya ndani na vinne vya uani ambavyo nilikuwa nimevipangisha isipokuwa chumba kimoja ambacho nilikuwa nikiishi mwenyewe.
 
Wakati huo sikuwa na mke na pia sikuwa na mawazo ya kuoa, pengine ni kwa sababu sikuwa na wazazi wa kunipa msukumo wa kuoa.
 
Mara tu baada ya kuvaa nilichukua  funguo ya gari nikatoka. Nilimuamsha mpangaji wangu wa chumba cha mbele na kumwambia afunge mlango wa mbele.
 
Teksi yangu ilikuwa barazani mwa nyumba yangu. Nilifungua mlango wa dereva na kujipakia. Nikawasha gari na kuondoka.
 
Nusu saa tu baadaye nilifika Habours Club ambayo ilikuwa eneo la Bombo. Nilikuta teksi nyingi pamoja na msongamano wa watu waliokuwa wakitoka katika klabu hiyo. Nilitafuta sehemu yenye nafasi nikaiegesha teksi na kuwasiliana na Mariam.
 
“Tayari nimeshafika” nikamwambia kwenye simu.
 
“Uko kwa wapi?”
 
Nakamuelekeza mahali nilipokuwa namsubiri.
 
“Tunakuja sasa hivi” akaniambia.
 
Baada ya kusubiri kwa dakika kumi hivi nikaona wasichana wawili wakifungua milango ya teksi yangu na kujipakia.
 
“Habari ya saa hizi?” Mariam akanisalimia.
 
“Nzuri” nilimjibu huku nikiirudisha gari kinyume nyume kisha nikabadili gea na kuondoka.
 
Wakati teksi ikiwa katika mwendo Mariam aliniambia.
 
“Mimi ninakwenda barabara ishirini na mwenzangu anakwenda Kange. Sijui utaanza wapi?”
 
Eneo la Kange liko karibu kilometa tano nje ya jiji. Kwanza niliwaza gharama ya mwendo wangu hadi huko kisha nikamwambia.
 
“Nitakupeleka wewe kwanza”
 
Kwa vile hawakuniuliza itakuwa kiasi gani sikuona haja ya kuanza mimi kuwaambia. Nikanyamaza kimya.

ITAENDELEA KESHO na usikose kufuatilia uhondo huu wa kusisimua nini kitatokea wakati wa safari kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com

No comments:

Post a Comment