Tuesday, March 24, 2015

MKUU WA MKOA WA TANGA, SAID MAGALULA AWAZINDUA WAGANGA WAKUU WA HOSPITALI TANGA

Tangakumekuchablog

Tanga, MKUU wa Mkoa wa Tanga, Said Magalula, amevitaka vituo vya afya Tanga  kutumia fursa ya mikopo itolewayo  na Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) ikiwemo vifaa tiba na madawa  na kuweza kuwa msaada kwa wananchi katika kupata huduma zilizo  bora.

Akizungumza katika kikao cha uhamasishaji mpango wa mikopo ya vifaa tiba  kilichofanyika hospitali ya Mkoa ya Bombo, Magalula aliwaagiza waganga wakuu wa hospitali Mkoa na Wilayani kuitumia nafasi hiyo itolewayo na Bima ya Afya.

Alisema kelele za wananchi kulalamikia huduma mbovu zitolewazo katika vituo  imezidi wakati ziko fursa za kupunguza kero hizo kwa kukopa vifaa pamoja na ukarabati wa majengo jambo ambalo ni nadra kuipata nafasi hiyo.

“Kumbe kuna fursa kama hizi zitolewazo na wadau wetu wa afya mimi nilikuwa sijui-----kwa nini sasa hamuzichangamkii na kupunguza kelele za wananchi kulalamikia huduma mbovu zikiwemo uhaba wa madawa” alisema na kuongeza

“Kwa maana hiyo natoa agizo kwa waganga wakuu wa hospitali zote za mjini na Wilayani kuhakikisha wanaitumia ipasavyo fursa hii na kumaliza manung;uniko kutoka kwa wananchi juu ya hospitali na vituo vyetu vya afya” alisema Magalula

Alisema kuna baadhi ya vituo vya afya majengo yake yako katika mazingira hatarishi na mengine kufikia hatua ya  kutaka kuanguka na hivyo kuwaagiza kuchangamkia nafasi inayotolewa na mfuko wa bima ya afya.

Alisema majengo mengi yako katika hali mbaya ikiwemo miundombinu ya kupitishia maji na uchakavu wa majengo jambo ambalo linaondoa taswira ya mazingira ya afya kwa wananchi.

Kwa upande wake Meneja wa Taifa Mfuko wa Bima ya Afya Mkoa wa Tanga, Ali Mwakababu, alisema mbali ya elimu na matangazo mengi lakini hadi sasa ni vituo vichache ambavyo vimejitokeza kutaka mikopo.

Alisema elimu bado inahitajika na hivyo kuitaka Wizara ya Afya Mkoa kutoa elimu kwa Waganga wakuu wa Wilaya kuomba mikopo ambayo inaweza kusaidia kuimarisha huduma zao zikiwemo matibabu na ukarabati wa majengo.

“Toka mwaka 2007 Bima ya Afya ilipoanzisha huduma ya kutoa mikopo ni vituo vichache ambavyo vimeomba mikopo-----ukiangalia majengo mengi ni chakavu na havina vifaa tiba” alisema Mwakababu

“Vituo vyetu viko na uhaba wa madawa wakati mfuko wa bima umeandaa utaratibu wote wa kupata huduma hizo----kuna hospitali nyingi hazina huduma za Ex ray na hii pia  tunatoa” alisema

Meneja huyo aliwataka waganga wakuu wa Wilaya kuhakikisha wanamaliza changamoto wanazokabiliana nazo katika vituo vyao  lengo likiwa ni kuboresha huduma  kwa wananchi.

  Mwisho

 Meneja wa Mfuko wa Bima ya Afya Mkoa wa Tanga, Ali Mwakababu akitoa risala wakati wa kikao cha Uhamasishaji Mpango wa Mikopo na Vifaa Tiba kwa watoa huduma  kilichofanyika ukumbi wa hospitali ya Mkoa ya Bombo na kuwashirikisha waganga wakuu wa Wilaya na wadau wa Afya Mkoa wa Tanga.



 Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Said Magalula, akifungua kikao cha Uhamasishaji mpango wa mikopo na vifaa tiba kwa watoa huduma kilichoandaliwa na Mfuko wa Bima ya Afya Tanga   kilichofanyika ukumbi wa hospitali ya Mkoa ya Bombo na kuwashirikisha waganga wakuu wa Wilaya  na madaktari pamoja na  wadau wa afya.
 Washiriki wa kikao cha Uhamasishaji mpango wa mikopo na vifaa tiba kwa watoa huduma kilichoandaliwa na Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF)Tanga  na kuwashirikisha waganga wakuu , madaktari na wadau wa Afya kilichofanyika ukumbi wa hospitali ya Mkoa ya Bombo



No comments:

Post a Comment