Friday, March 27, 2015

RC , MAGALULA ACHOSHWA NA UCHOMAJI MOTO MISITU

Tangakumekuchablog
Handeni,MKUU wa Mkoa wa Tanga, Said Magalula, amesikitishwa na vitendo vya baadhi ya watu kuchoma moto misitu na nyasi na kuwaagiza Wakuu wa Wilaya Tanga kuwachukulia hatua za kisheria  wote wenye tabia hiyo.

Akizungumza katika maadhimisho ya siku ya Kutundika Mizinga ya Nyuki kitaifa yaliyofanyika kijiji cha Bogolwa Wilayani Handeni Mkoani Tanga  juzi, Magalula alisema vitendo vya uchomaji moto misitu na nyasi umekuwa ukiwakimbiza nyuki na viumbe hai.

Alisema hali hiyo pia imekuwa ikichangia  uhaba wa mvua  katika maeneo hayo na kusababisha ukame na hivyo kuwa chanzo cha kuibuka kwa uhaba wa chakula na njaa kuingia majumbani.

“Uchomaji wa moto misitu na nyasi umekithiri Tanga na hili sitokubali kuona linaendelea----vitendo hivi vimekuwa vikichangia kwa kiasi kikubwa uharibifu wa mazingira na ukame” alisema Magalula na kuongeza

“Tumekuwa tukiona baadhi ya maeneo kukumbwa na balaa la njaa kutokana na kukosa mvua--- tumekuwa tukipata mvua zaidi ya mara tatu kwa mwaka halafu sisi wenyewe tunaikimbiza kwa kukata miti na kuchoma moto misitu” alisema

Katika kulikomesha hilo, Magalula aliwaagiza Wakuu wote wa Wilaya Tanga kuwachukulia hatua kali za kisheria watu wenye tabia ya kuchoma moto  misitu na nyasi na kuweza kulitokomeza jambo hilo kwa maslahi ya wananchi.

Akizungumza katika sherehe hizo, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Misitu na Nyuki , Gladness Mkamba, amewaondoa hofu wafugaji nyuki kuwa soko la Asali liko ndani na nje ya nchi na hivyo kuwataka kuongeza mizinga ya ufugaji nyuki.

Alisema kwa sasa soko hilo linaendelea kukua kwa kasi katika  masoko ya Ulaya na Amerika na hivyo ni fursa za wafugaji kuyatumia masoko hayo pamoja na soko la pamoja la Afrika Mashariki.

“Soko la asali linazidi kukua kwa kasi kila siku na hii ni fursa kwa wafugaji na vijana kuchangamkia masoko---hii ni pamoja na hili la kwetu la Afrika Mashariki” alisema Mkamba

Alisema Idara ya Misitu na Nyuki itafanya makongamano na vijana kuhamasisha ufugaji nyuki kwani watu wengi hawana elimu hiyo na kuadhimiria kutembelea  kila Wilaya.

                                                     Mwisho

No comments:

Post a Comment