Tuesday, March 24, 2015

SOMA MAKUBWA YALIYOANDIKWA MAGAZETINI LEO,MARC 24 TZ

Mkusanyiko huu kutoka magazetini unaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha elimu cha Candle Education Centre Tanga. Kituo kinaongoza kufaulisha wanafunzi kidato cha pili hadi cha sita. wapo Tanga mkabala na Bank ya CRDB simu 0715 772746

6efaf3e09963adb3a83252d5803074e1
MWANANCHI
Rais Jakaya Kikwete amelikata Jeshi la Polisi nchini kujiandaa kikamilifu ili kukabiliana na vurugu zozote zitakazojitokeza wakati wa uandikishaji wapigakura, upigaji Kura ya Maoni ya kupitisha Katiba Inayopendekezwa na Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, mwaka huu.
Akifunga mafunzo ya maofisa warakibu wasaidizi katika Chuo cha Taaluma ya Polisi, Dar es Salaam jana, Rais Kikwete alisema dalili zinaonyesha kwamba kuna watu wenye nia ya kuhatarisha amani katika matukio hayo.
Tunayoyasikia na tunayoyaona yanaashiria kuwapo kwa dalili za wenzetu kukwamisha shughuli hizi za kitaifa kwa kufanya vurugu, Jeshi la Polisi jiandaeni na vitendo vyote vitakavyofanywa kwa lengo la kuhatarisha amani,” alisema akijibu maombi ya kupatiwa vifaa yaliyowasilishwa kwake na Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Ernest Mangu.
Alisema Serikali itahakikisha kazi ya uandikishaji katika daftari la wapigakura, upigaji wa kura ya maoni na uchaguzi mkuu vinafanyika kwa amani na utulivu kwa gharama zozote.
Alisema ili kufanikisha kazi hiyo, Serikali italiwezesha Jeshi la Polisi ili litekeleze kikamilifu majukumu yake ya kulinda amani na utulivu.
Tutawawezesha kwa kuwapa vifaa ili kuhakikisha mnafanya kazi yenu ya kutunza amani kwa umakini zaidi,” alisema Rais Kikwete anayemaliza muda wake wa mihula miwili ya urais baada ya uchaguzi mwaka huu.
Iwapo mambo yote yatakwenda kama yalivyopangwa, Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa itapigwa Aprili 30 wakati Uchaguzi Mkuu utafanyika Oktoba.
Akizungumzia kauli hiyo ya Rais Kikwete, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alisema, “Rais Kikwete yeye ndiye mtu wa kwanza kuivuruga amani kwa kutangaza tarehe ya kufanyika kwa kura ya maoni wakati siyo jukumu lake na jukumu hilo ni la NEC, Serikali yake kushindwa kuratibu vyema mchakato wa uandikishaji.
MWANANCHI
Mbunge wa Iringa Mjini Peter Msigwa amesema zaidi ya asilimia 80 ya wabunge waliopo kwa sasa bungeni  hawakustahili kuwa wabunge kutokana na baadhi yao kuwa na uwezo mdogo kiakili na uliolinganishwa na GB moja ya kompyuta.
Msigwa alisema kwa maoni yake ni asilimia 20 pekee ya Wabunge ndiyo wenye uwezo na vigezo vinavyostahili kupata nafasi hiyo ya uwakilishi wa wananchi katika chombo hicho cha kutunga sharia.
Alisema wakati umefika kwa taifa kuweka vigezo maalum vya kuwapata viongozi wa kisiasa wakiwemo wabunge na Rais.
“Tatizo la watanzania hatuna vigezo na uwezo wa  tunavyoviweka kwa ajili ya mtu anayetaka kuwa kiongozi, yaani tujue mtu anayekuja kuomba uongozi anatakiwa awe mtu wa aina gani” Msigwa.
Alisema kigezo kinachozingatiwa kwa siasa ili mtu awe Mbunge cha kujua kusoma na kuandika hakitoshi na siyo sahihi hivyo kinapaswa kitazamwe upya ili kupata wawakilishi watakaoweza kutimiza wajibu wao ipasavyo.
Wabunge wengi hawamuelewi Tundu Lissu kwa sababu vichwa vyao vina GB moja za ubongo, sasa kukusanya mambo yote yale ya bunge kichwa kinapata moto na ilikupata majibu rahisi wanasema Lissu kichaa maana hawawezi kufikiria kiwango kile kutokana na akili zao kuwa ndogo” Msigwa.
MWANANCHI
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Makazi, William Lukuvi ameziagiza halmashauri zote za wilaya kutenga ardhi kwa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ili lijenge nyumba za bei nafuu.
Lukuvi alisema hayo juzi wilayani Babati mkoani Manyara, wakati akizindua mradi wa nyumba za gharama nafuu zilizojengwa katika eneo la Mrara.
Katika mradi huo, nyumba 40 zenye vyumba viwili vya kulala zitauzwa kwa Sh34 milioni, wakati zile zenye vyumba vitatu, zitauzwa Sh45 milioni.
Alisema lengo la ujenzi wa nyumba hizo ni kuhakikisha wananchi wanapata nyumba za bei nafuu ili kuishi kwenye makazi bora.
Tunataka halmashauri zote zitenge maeneo maalumu, kwani tunatarajia miradi kama hii iendelezwe mikoa yote nchini,” alisema Lukuvi na kuongeza:
“Naamini, bei ya nyumba hizi wananchi wa kawaida wanaweza kuzimudu na hivyo kutimiza ndoto za kuishi kwenye makazi bora yanayokwenda na wakati.”
Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Nehemia Mchechu alisema mpango wa ujenzi wa nyumba za makazi ya gharama nafuu unaojulikana kwa kauli mbiu; ‘Nyumba yangu, maisha yangu’, ulibuniwa ili kupunguza uhaba wa nyumba.
Mchechu alisema nyumba nyingine za aina hiyo zinatarajiwa kujengwa katika maeneo 23 katika halmashauri mbalimbali.
Ujenzi wa nyumba hizi utawapa fursa wananchi kuishi kwenye nyumba za kisasa, bora na gharama nafuu. Lakini pia mradi huu unapendezesha mandhari ya miji na kuongeza wigo wa kodi ya majengo,” Mchechu.
MWANANCHI
Miaka ya karibuni Jiji la Dar es Salaam limeshuhudia kuporomoka kwa maghorofa matano katika maeneo tofauti likiwamo tukio la mwaka 2013, ambapo ghorofa lililokuwa Mtaa wa Indira Ghandi lilianguka na kupoteza maisha ya watu wapatao 34.
Ajali zote hizo zimeacha idadi kubwa ya majeruhi, baadhi wakibaki na ulemavu maisha, lakini hakujawa na taarifa rasmi kutoka tume zilizoundwa au mamlaka husika zilizochunguza matukio hayo.
Hata hivyo, ukweli unabaki kwamba majanga hayo ya kuporomoka kwa maghorofa yanahusishwa na ujenzi ulio chini ya kiwango au taratibu zilikiukwa.
Ujenzi wa majengo mengi ya sasa, unafanyika kwa kuvunja majengo ya kale yenye urefu usiozidi ghorofa tano, majengo mapya huwa ni marefu zaidi ya yale ya awali.
Mbali na kuendelea kutumia miundombinu ya awali ya maji, umeme na majitaka, majengo mapya hayana maeneo kwa ajili ya maegesho pengine hata huduma nyingine za kijamii.
Profesa Kumbwa eli Salewi anayeiwakilisha taasisi ya makandarasi ya ‘Institution of Civil Engineers’ (ICE) ya New Zealand nchini anasema ujenzi unaofanyika sasa wa hadi ghorofa 30 unasababisha kukosekana uwiano wa huduma za msingi.
Anasema kwamba tafiti mbalimbali zinabainisha kuwa Dar es Salaam ni jiji ambalo ujenzi wa majengo mbalimbali unaoendelea sasa hauliweki salama pale yatakapotokea majanga ya kibinadamu, asili au hata shambulio la kigaidi.
Anasema kwa bahati mbaya likitokea shambulio, tetemeko la ardhi au kimbunga, maafa yake huenda yakawa makubwa kuliko inavyofikiriwa na kusababisha idadi kubwa ya vifo ambavyo vingeweza kuepukika.
Profesa huyo anasema maeneo mengi ulimwenguni, ujenzi huzingatia uwepo wa maeneo ya wazi yanayoweza kutumika kuwakusanya majeruhi au waathirika wa janga lolote linaloweza kutokea.
“Ingawa mabaya hayaombwi yatokee lakini iwapo itatokea, vifo vitakuwa vingi kuliko inavyofikiriwa. Itakuwa ni kazi kubwa kulifikia na kuwapo kwa nafasi kwa ajili ya uokoaji,” anasema.
Profesa Salewi anasema mitaa ya Azikiwe, Samora, Bibi Titi na Barabara ya Morogoro ilipaswa kuwa na eneo kubwa la wazi kama ilivyo nchi nyingine, lakini hali ilivyo ni tofauti, kwani maeneo yote yamejengwa majengo marefu ya biashara. Anasema nchini sekta ya ujenzi inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa pamoja na ukosefu wa uadilifu unaofanya kandarasi kuzingirwa na rushwa, hivyo ujenzi kuwa chini ya kiwango.
MTANZANIA
Mvua zinazoendelea kunyesha jijini Dar es Salaam zimesababisha watu waliopoteza maisha kwa kufariki dunia kufikia saba, huku nyumba zaidi ya 200 zikiwa zimezingirwa na maji katika maeneo mbalimbali ya jiji hilo.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa katika maeneo ya Buguruni Kwa Mnyamani baadhi ya nyumba bado zimengirwa na maji na kusababisha wananchi wanaoishi kwenye maeneo hayo kuhama kwa muda.
Mkazi wa Buguruni kwa Mnyamani, Mussa Abdallah, alisema kuharibika kwa miundombinu ya makaravati kumechangia maji kutuama kwenye makazi yao.
“Hakuna daraja ndiyo maana maji yametuhama kwenye nyumba zetu, tunaiomba Serikali iweze kuchukua hatua za dharura kwa kujenga daraja ili tuweze kupunguza hali hii,” alisema Abdallah.
Alisema kutokana na mvua hizo, wamepata hasara kubwa ikiwamo kuharibika kwa mali zao vikiwamo vyombo vya ndani jambo ambalo linawafanya waishi katika mazingira ya umasikini.
“Vitu vyangu vyote vimeondoka na maji na kubaki masikini, jambo ambalo limenirudisha nyuma kimaendeleo, kutokana na hali hiyo, ninaiomba Serikali inisaidie,” alisema.
Alisema licha ya mvua kusomba vitu hivyo, lakini hawezi kuhama kwa sababu hawana mahali pa kwenda, na kwamba Serikali imeshindwa kuwasaidia kwa lolote.
Hadi sasa hatujapata msaada wowote kutoka serikalini na kwamba hatuna pa kwenda, jambo ambalo linanifanya nishindwe kuhama kwenye nyumba yangu,” alisema.
Katika maeneo ya Tandale kwa Mtogole na Mkunduge, Kigogo Bonde la Mto Msimbazi, Kinondoni Bonde la Mkwajuni, Jangwani na Magomeni Sunna, pia baadhi ya nyumba bado zimezingirwa na maji huku wananchi wakiwa wamehama kwa hofu ya kupoteza maisha.
Nyumba zetu zimechukuliwa na maji kutokana na mvua zinazonyesha, hali iliyosababisha kuhamia nyumba za jirani kwa ajili ya kuomba hifadhi,” Juma Hussein mkazi wa Tandale kwa Mkunduge.
Kutokana na mafuriko hayo, wameiomba Serikali kurekebisha miundombinu ya maji ikiwamo kujenga mifereji ya kisasa itakayoweza kusafirisha maji kwenda kwenye mkondo wa Mto Ng’ombe.
MTANZANIA
Joto la Uchaguzi wa Rais ndani ya CCM linazidi kupanda huku makada na viongozi wa chama hicho wakipigana vijembe hadharani.
Hali hiyo inatokana na kile kinachojitokeza sasa, kuibuka kwa makundi ya jamii, wakiwamo wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu, kuwashawishi makada kadhaa wa CCM wawanie nafasi hiyo ya uongozi wa nchi katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba.
Makada ambao wamekuwa wakishawishiwa kuwania nafasi hiyo ni Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo.
Wakati baadhi ya makada wengine wanaotajwa kutaka kuwania urais ndani ya CCM wakimlalamikia Lowassa, wachambuzi wa siasa wamekuwa wakihoji mpango wa Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, alipochapisha vitabu na kugawa kwa wajumbe wote wa mkutano mkuu, lakini makada wenzake wamekuwa kimya, hawajalalamikia kitendo chake hicho.
Mbali na hilo, pia anadaiwa kuwa alinunua simu za Gallaxy Sumsang zaidi ya 140, akazigawa kwa wajumbe wa Baraza la Vijana la CCM (UVCCM) Zanzibar suala ambalo bado hadi sasa hajalitolea ufafanuzi.
Naye Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, ambaye anatajwa kuwapo katika mbio za urais, alikuwa akitembea na mabango ya kuonyesha watu wakimwomba agombee jambo ambalo lilimfanya aandikiwe barua na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kusitisha ziara zake ambazo zilitajwa kuwa za kampeni za kuwania urais.
 Wafuasi wa Mwigulu pia wanadaiwa kuandika katika mawe makubwa katika barabara nchi nzima kwamba yeye ndiye Rais 2015.
Jana, Lowassa amejibu mapigo na kusema hawezi kuwajibu wanaosema anawalipa wanaomshawishi kuwania nafasi hiyo, kwani kufanya hivyo ni kuwapa sifa wasizostahili na wanachofanya ni upuuzi na uongo.
Kauli hiyo imekuja baada ya jana baadhi ya vyombo vya habari, kumnukuu Makamba, ambaye ametangaza nia ya kuwania urais akisema kuna watu wanatumia vibaya umasikini wa Watanzania kwa kuwakusanya na kuwapa fedha ili waseme wanawashawishi wawanie urais.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kupokea ujumbe wa wachungaji 110 wa makanisa ya Kipentekoste kutoka sehemu mbalimbali nchini jana, Lowassa alisema hana uwezo wala sababu ya kuwagharamia watu wanaofika nyumbani kwake kumshawishi, na kwamba wengi wanafanya hivyo kwa mapenzi yao na Mungu wao.
HABARILEO
Mwongozo wa ada elekezi utakaondoa utata wa utofauti wa kulipa ada baina vyuo na vyuo nchini, unatarajiwa kukamilika na kuanza rasmi kutumika mwezi ujao.
Kwa sasa mwongozo huo umeshaandaliwa na kinachosubiriwa ni mfumo wa kompyuta utakaosaidia kukokotolea ada zitakazotumika katika vyuo vikuu nchini ambao ndio utakamilika rasmi Aprili mwaka huu.
Hayo yalibainishwa na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Anne Kilango, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Amina Makilagi (CCM), aliyetaka kujua mchanganuo wa ada baina ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) na endapo unaendana na hali halisi.
Akijibu swali hilo, Kilango alikiri kuwa kumekuwa na tatizo hilo la utofauti wa utozaji ada katika vyuo mbalimbali nchini kwa muda mrefu, na kwa sasa Tanzania ina vyuo vikuu 53 na taasisi 21 zinazotoa shahada.
Alisema ada katika vyuo vikuu vya umma ikiwa ni pamoja na UDSM na UDOM, zinatofautiana kati ya chuo na programu wanayosomea wanafunzi.
Alisema, mfano programu ya uhandisi UDSM ada yake ni Sh milioni 1.3 wakati UDOM programu hiyo ni Sh milioni 1.5 na katika programu za Sayansi na Ualimu UDSM inatoza ada Sh milioni 1.3 wakati UDOM unatoza Sh milioni 1.2.
Alisema kwa kuzingatia tofauti za kiasi cha ada kinachotozwa na vyuo vikuu nchini, Serikali ilifanya utafiti wa kina kwa kushirikisha wadau mbalimbali ili kuweza kupanga ada elekezi kwa programu zote zinazofundisha katika vyuo vyote vikuu.
“Mwongozo wa ada elekezi umekwishaandaliwa na kwa sasa Serikali inaandaa mfumo wa software wa kukokotoa ada zitakazotumika katika vyuo vikuu vyote nchini,” alisema.
Ni halali yako kupata kila stori inayonifikia mtu wangu, niko tayari kukutumia wakati wowote kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com

No comments:

Post a Comment