Tuesday, March 24, 2015

NILIJUA NIMEUA SEHEMU YA (4)


 
NILIJUA NIMEUA
 
ILIPOISHIA
 
Baada ya kusubiri kwa dakika kumi hivi nikaona wasichana wawili wakifungua milango ya teksi yangu na kujipakia.
 
“Habari ya saa hizi?” Mariam akanisalimia.
 
“Nzuri” nilimjibu huku nikiirudisha gari kinyume nyume ksha nikabadili gea na kuondoka.
 
Wakati teksi ikiwa katika mwendo Mariam aliniambia.
 
“Mimi ninakwenda barabara ishirini na mwenzangu anakwenda Kange. Sijui utaanza wapi?”
 
Eneo la Kange liko karibu kilometa tano nje ya jiji. Kwanza niliwaza gharama ya mwendo wangu hadi huko kisha nikamwambia.
 
“Nitakupeleka wewe kwanza”
 
Kwa vile hawakuniuliza itakuwa kiasi gani sikuona haja ya kuanza mimi kuwaambia. Nikanyamaza kimya.
 
SASA ENDELEA
 
Nilimpeleka Mariam barabara ishirini. Niliposimamisha teksi aliniuliza.
 
“Ni kiasi gani?”
 
“Unauliza kiasi cha kukuleta hapa au cha kwenda mpaka Kange?”
 
“Kange atakulipa mwenyewe. Niambie gharama ya kunileta hapa”
 
“Ni elfu sita”
 
“Punguza, fanya tano. Mimi ni mteja wako wa kila siku”
 
“Haya nipe”
 
Mariam akafungua pochi na kutoa noti ya shilingi elfu tano akanipa. Akafungua mlango wa teksi na kushuka.
 
Aliagana na mwenzake na kwenda kubisha mlango wa nyumbani kwao. Nami nikaanza safari ya kuelekea Kange.
 
Nilipofika Kange Nilimuuliza msichana anakwenda mtaa gani, akaniambia nikate kushoto. Nilipokata kushoto akanielekeza mtaa ambao anaoishi.
 
Nilipofika katika mtaa huo alinionyesha nyumba aliyotaka nimpeleke. Ilikuwa nyumba nzuri kuliko aliyokuwa anaishi Mariam.
 
“Unanidai kiasi gani?” Msichana akaniuliza niliposimamisha teksi.
 
“Nipe elfu kumi”
 
Msichana hakubishana. Alifungua pochi yake akatoa noti ya shilingi elfu kumi na kunipa. Akafungua mlango na kushuka.
 
Alikwenda kwenye baraza ya ile nyumba na kupiga simu.
 
Nilimsikia akisema.
 
“Asiya nifungulie mlango”
 
Nikaiondoa teksi na kumuacha hapo hapo.
 
Wakati narudi jijini nilikuta gari limeegeshwa kando ya barabara. Taa zake za nyuma zilikuwa zinawaka. Wakati nalikaribia gari hilo niliona mtu aliyekuwa kando yake akinipungia mkono kunisimamisha.
 
Wazo nililolipata kwanza ni kuwa gari hilo lilikuwa limeharibika na kwamba mtu aliyekuwa akinipungia mkono ama alikuwa anataka msaada au alikuwa anahitaji huduma ya teksi yangu.
 
Kwa vile nilikuwa kwenye mwendo wa kasi nililipita gari hilo na kwenda kusimama mbele. Hapo hapo mawazo yangu yakabadilika. Niliwaza kwamba huenda gari hilo liliegeshwa kwa hila lionekane limeharibika kumbe ni majambazi wanaosubiri magari yasimame waanze kupora watu.
 
Nilikuwa nimechelewa kufikiria hilo. Nilikuwa nimeshasimamisha teksi na jamaa aliyenisimamisha alikuwa ameshafika kwenye dirisha la teksi yangu!
 
Chini ya siti yangu ya dereva, siku zote huweka parange (sime ya kimasai) kwa ajili ya kujihami endapo kutatokea tatizo la kuvamiwa na mtu au watu wenye nia mbaya.
 
Kwa vile sikuwa na uhakika kuwa mtu huyo aliyenisimamisha alikuwa na nia mbaya au nzuri, tayari nilishapeleke mkono wangu wa kulia kuushika mpini wa parange iliyokuawa chini ya siti niliyokalia.
 
Nilikuwa nimejiweka tayari, kama atakuwa na nia mbaya niweze kukabiliana naye.
 
 
ITAENDELEA kesho na usipitwe na uhondo huu wa kusisimua kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com

No comments:

Post a Comment