Monday, March 16, 2015

HADITHI SEHEMU YA (2)



Hadithi hii inaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha Tiba Asilia kilichopo Chuda Tanga, Mkombozi Sanitarium Clinic. Mabingwa wa magonjwa sugu yakiwemo ya Kisukari, Figo, Saratani na mengi mengineyo. Wapo Chuda Tanga. simu 0654 361333

NILIJUA NIMEUA (2)

Nikadhani ataanza tena kulalamika kutaka kupunguziwe kiasi cha pesa. Lakini haikuwa hivyo, alifungua mkoba wake akatoa noti ya shilingi elfu tano na kuniambia.

“Shika”

Niligeuka nikaipokea kisha nikamfungulia mlango.

Akashuka haraka na kukimbilia kwenye baraza ya ile nyumba. Wakati anabisha mlango nikaiondoa teksi.

Nilirudi katika egesho langu lililokuwa karibu na hospitali ya Ngamiani.

Nililipendelea egesho hilo kwa maana. Kwanza lilikuwa karibu na hospitali ambapo mara kwa mara kunakuwa na wagonjwa wanaohitaji huduma ya teksi. Pili nilikuwa peke yangu na tatu kulikuwa na mahoteli mengi yaliyokuwa karibu na hapo na kufanya nipate wateja wengi.

Wakati naliegesha gari nilisikia mlio wa simu ndani ya gari. Nikashituka na kudhani ilikuwa simu yangu. Lakini niligundua haikuwa simu yangu. Simu yangu haikuwa na mlio kama huo  niliousikia.

SASA ENDELEA

Nikatega masikio yangu ili nijue mlio huo ulikuwa unatokea wapi. Nikapata jibu. Mlio huo ulitoka nyuma yangu. Nikageuza kichwa na kutazama nyuma. Ndipo nilipoiona simu ikiita kwenye siti.

Mara moja niligundua kuwa yule msichana niliyempakia alisahau simu yake. Ilikuwa simu ileile aliyokuwa akiitumia wakati nimempakia.

Sikuweza kujua ni nani aliyekuwa anapiga. Iliwezekana alikuwa  yeye mwenyewe, aliamua kupiga baada ya kugundua kuwa aliisahahu simu ndani ya teksi yangu. Au alikuwa ni mume wake ingawa sikuwa na hakika kama alikuwa na mume.

Nikajiuliza niipokee ile simu au nisiipokee? Nikapata jibu kuwa nisiipokee kwa vile sikujua nani anapiga na isitoshe haikuwa ikinihusu.

Baada ya kuita kwa muda simu ikakatika lakini baadaye kidogo simu ikaita tena. Nikaiacha iite.

Kwa vile nyumba aliyoingia yule msichana ninaifahamu nitampelekea wakati wowote, nikajiambia.

Hata hivyo sikupata amani kwani simu ilikuwa ikiita kwa mfululizo. Ufumbuzi ulikuwa niizime au niipeleke kwa mwenyewe haraka. Kwa vile nilishindwa kuizima niliamua niwashe teksi nimrudishie mwenyewe.

Mvua sasa ilkuwa imeacha kabisa. Nilifika katika mtaa aliokuwa akiishi yule msichana. Tangu natokea katika mtaa huo niliona msichana amesimama kwenye baraza ya ile nyumba akiwa amejaa wasiwasi. Nilipokaribia zaidi niligundua kuwa alikuwa ni yule msichana  niliyempakia.

Niliposimamisha teksi mbele ya ile nyumba aligutuka, akanikodolea macho ya tashiwishi.

Mara moja akashuka kwenye baraza na kuja kwenye mlango wa teksi wa dereva.

“Kaka umeniletea simu yangu?”  akaniuliza kwa matumaini.

Kwa kutaka kumshitua a mimi nikamuuliza.

“Simu gani?”

“Jamani nilisahau simu yangu kwenye siti. Simu yenyewe niliinunua juzi tu shilingi laki tatu”

Nilipoona amehamanika nilimwambia.

“Hebu angalia kwenye siti uliyokuwa umekaa”

Akasogea  mlango wa nyuma na kuchungulia kwenye dirisha.

“Si ile pale!” akasema huku akifungua mlango.

Aliingia ndani ya teksi akaichukua ile simu na kutoka.

“Asante kaka. Kumbe ulikuwa unanitania!”

Sote tukacheka. Huzuni ilikuwa imeshamtoka.

“Wewe ni muaminifu sana. Nitakuwa nachukua teksi yako kila siku” akaniambia.

“Kwaheri, nakwenda zangu” nikamuaga.

“Ulikuwa umeniletea simu yangu. Asante sana kaka, endelea kuwa na moyo huo huo”

“Asante bibie”

Wakati natia gea niondoe gari sauti yake ikanisitisha.

“Nipe namba yako. Nitakuhitaji tena siku nyingine”

Nikamtajia namba yangu.

Je nini kitaendelea? Usikose kuendelea  na hadithi hii kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com

No comments:

Post a Comment